Friday, March 21, 2014

Tanzania inaweza kuzipiku nchi za A. Mashariki kiuchumi


Waziri Wa Afrika Mashariki Mh. Sitta
Mtangamano wa Afrika Mashariki umekuwapo kwa muda mrefu tangu wakati wa ukoloni, nchi ya Tanganyika, Kenya na Uganda zikiwa makoloni ya Uingereza.


Uingereza ilirithisha nchi hizo kwa kuwa na mipango yake kisiasa, kiuchumi na kijamii.

Baada ya ukoloni mwaka 1967 nchi hizo ziliungana ili kuendesha uchumi uliotakana na miundombinu iliyoachwa na wakoloni.

Hata hivyo, kwa mara ya kwanza muungano huo haukufika mbali kwani mwaka 1977 Jumuiya ya Afrika Mashariki ilivunjika.

Sababu za kuvunjika kwa jumuiya hiyo zilikuwa ni za kisiasa na kiuchumi. Kisiasa, kwanza itikadi za nchi hizo zilitofautiana.

Kwa mfano, wakati Tanzania ilikuwa ikifuata sera ya Ujamaa na Kujitegemea, Kenya ilifuata sera za kibepari na Uganda ilikuwa ikifuata mfumo wa mchanganyiko.

Vilevile kulikuwa na tofauti kati ya viongozi; Rais wa Tanzania, Mwalimu Julius Nyerere hakupatana na Rais wa Uganda, Yoweri Museveni. Kuhusu sababu za uchumi, nchi za Uganda na Tanzania hazikuridhishwa na mgawanyiko wa rasilimali hasa ikidaiwa kuwa Kenya ilichukua sehemu kubwa ya uchumi hasa viwanda.

Baada ya kuvunjika kwa jumuiya hiyo, ilipita miaka 22 ndipo wazo la kuifufua likarejeshwa tena. Mwaka 1999, nchi hizo zilitia saini mkataba wa kuanzisha upya Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Jumuiya hiyo ililenga kufikia hatua kadhaa ikiwa ni pamoja na umoja wa forodha, soko la pamoja na, umoja wa sarafu na shirikisho la siasa. Mwaka 2007, wanachama wa jumuiya hiyo waliongezeka baada ya nchi za Rwanda na Burundi kujiunga.

Licha ya changamoto za hapa na pale, lengo ni kuhakikisha kuwa jumuiya hiyo haipasuki kama ilivyotokea mwaka 1977.

Nafasi ya Tanzania kung’ara

Licha ya nchi hizo kuwa chini ya mtawala mmoja wa kikoloni (mbali na Rwanda na Burundi), bado inaelezwa kuwa Tanzania ina nafasi kubwa ya kuendelea kiuchumi kuliko wanachama wengine wa Afrika Mashariki.
Akizungumza katika mjadala wa bajeti za Afrika Mashariki ulioandaliwa na taasisi ya utafiti wa jamii na uchumi (ESRF) juzi jijini Dar es Salaam, mwakilishi kutoka Wizara ya Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Dk Abdulla Makame anasema Tanzania ina kila sababu ya kuendelea kupitia ushirikiano huo.

“Tunazo fursa nyingi tu za kuendelea; tunayo ardhi kubwa na yenye rutuba, tunazo rasilimali ingawa kwa sasa kuna janga la ujangili wa meno ya tembo. Tuko pia kwenye eneo zuri la kijiografia.

“Tofauti na nchi nyingine za Afrika Mashariki, Tanzania inapakana na Kenya, Uganda, Rwanda, Burundi, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC), Zambia, Malawi na Msumbiji. Hakuna nchi nyingine ya Afrika Mashariki inayopakana na nchi wanachama wote kwa wakati mmoja,” Dk Abdulla.

Bajeti Jumuiya ya Afika Mashariki

Pamoja na kuwapo kwa fursa hiyo anasema bado bajeti ya Serikali hailingani na matakwa ya maendeleo ya Jumuiya ya Afrika Mashariki.

“Bajeti ya Taifa hailingani na malengo na mipango ya maendeleo ya Afrika Mashariki. Tungetarajia kuwa bajeti za maendeleo ya jumuiya ziwekwe moja kwa moja kwenye wizara husika,” anasema Dk Makame.

Anashauri waandaaji wa bajeti kuangalia vipaumbele vya jumuiya hiyo na kukamilisha sera yake.

“Tunayo Reli ya Kati iliyojengwa na Wajerumani wakati wa ukoloni. Ilitakiwa reli hii itumike kuleta maendeleo ya uchumi kwa Tanzania, lakini bado haina viwango vya kimataifa,” anasema Dk Abdulla.

Akijibu hoja hizo, Kamishna Msaidizi wa bajeti kutoka Wizara ya Fedha, Emmanuel Tutuba anasema tayari bajeti ya Serikali imeanza kutekeleza mahitaji ya jumuiya hiyo.

“Nikiangalia kwenye bajeti yetu naona kuna mambo mengi yameanza kutekelezwa na mengine yako ngazi ya kimataifa. Kwa mfano, sekta ya umeme, ukiangalia takwimu na uwekezaji wa Serikali utaona lengo ni kuuza umeme kwa nchi za Afrika Mashariki. Maendeleo ni mazuri hasa kwa umeme wa gesi kutoka Mtwara. “Hata ukiangalia upande wa kilimo, wenzetu wa NRFA walinunua mahindi mengi na kuyauza nchini Kenya, wanategemea kupata Sh8 bilioni.

“Hata ukiangalia viwanja vya ndege kwa mfano, wa Kigoma, umejengwa mahsusi kwa ajili ya kuunganisha Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, Rwanda na Burundi. Kwa hiyo tayari kuna utekelezaji wa bajeti kwa maendeleo ya Afrika Mashariki.”

Biashara imeongezeka zaidi
Naye Ofisa wa Shirikisho la Chama cha Wafanyakazi, Kilimo na wenye Viwanda (TCCIA), Adam Zuku anasema: “Tangu tumejiunga, ukubwa wa biashara umeongezeka tofauti na zamani, haijaridhisha, lakini inakwenda vizuri.

“Tunapozungumzia mtangamano huu wa sasa ni tofauti na wa zamani.

Mtangamano wa sasa ni wananchi zaidi kuliko zamani ambapo ilikuwa kwa viongozi pekee. Siku hizi mambo yanafanywa na wataalamu,” anasema. Anatoa mfano wa ukuaji wa biashara akisema hata mashirika ya viwango ya jumuiya hiyo sasa yanatambuana na kutoa maagizo yanayofanana.
 Chanzo: Mwananchi

No comments: