Monday, November 4, 2013

Wananchi waanzisha kijiji msituni



*Wanapeperusha bendera ya rangi nyekundu
KIKUNDI cha watu wasiofahamika, kimeanzisha kijiji kisicho rasmi katikati ya Msitu wa Hifadhi ya Taifa ya Kazimzumbwi uliopo Wilaya ya Kisarawe, Mkoa wa Pwani. Katika maeneo yao ya makazi, wananchi hao wametundika bendera mbili, moja ikiwa na rangi nyekundu na nyingine ina rangi ya bluu ambazo hazijafahamika zinaashiria nini.

Moja ya majukumu ya wananchi hao, yanatajwa kuwa ni kuhifadhi watu kutoka nje ya Tanzania wakiwamo wanaotoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC).

Wageni hao huwatapeli wananchi mbalimbali hasa hasa wanaotoka Dar es Salaam, ambapo huwauzia mashamba ndani ya msitu huo kwa maelezo kwamba msitu huo ni mali yao.

Uchunguzi uliofanywa na Rai Jumatatu kwa kushirikiana na timu ya Mtandao wa Asasi za Mazingira Tanzania (MANET) kwa siku kadhaa, umegundua Serikali ya Wilaya ya Kisarawe ina taarifa za kijiji hicho lakini imeshindwa kuchukua hatua kutokana na sababu ambazo hazina msingi wowote.

Katika maeneo yao ya makazi, wanakijiji hao wameweka vibao viwili vilivyoandikwa kwa herufi kubwa maneno yanayosomeka; MJI MPYA NZASA II ILALA kibao kingine kinasomeka; KILIMO KWANZA ambacho kiko katika barabara inayoelekea kwa mmoja wa viongozi wao, aliyefahamika kwa jina la Jackson Rwehumbiza.

Baadhi wa wananchi na viongozi wa Kijiji cha Maguruwe kilichopo Kata ya Msimbu, Tarafa ya Sungwi jirani na msitu huo, wanasema watu wanaoishi katika kijiji hicho wamekuwa tishio kwa maisha yao pamoja na mazingira yanayowazunguka.

Mmoja wa wananchi hao, Shaaban Kulinangwa ambaye ni mkazi wa kijiji hicho, aliiambia Rai Jumatatu, kwamba tangu kikundi hicho kianzishe makazi ya kudumu msituni humo, amani imetoweka na mara nyingi wamekuwa wakitishiwa maisha na pia wanawake hubakwa pindi wanapopita katika msitu huo.

Kwa mujibu wa Kulinangwa, mwaka jana yeye na wenzake 14 walipokuwa wakifyeka nyasi na miti kwa ajili ya kukabiliana na moto, walivamiwa na kutekwa na kikundi cha watu zaidi ya 20 wanaosemekana ni wakazi wa kijiji hicho cha msituni.

“Tulivamiwa na kutekwa wakati tunapalilia mpakani mwa msitu na kijiji ili kujihami na moto na wakati wa tukio hilo, tulivamiwa na watu hao ambapo walituvua nguo, waliturusha kichura na wakatunyang’anya fedha tulizokuwa nazo.

“Nakumbuka Mkuu wa Wilaya ya Kisarawe wa wakati huo ambaye ni Mama Karamagi, ndiye alitusitiri na kutupatia nguo, lakini watu hao mpaka leo hawajakamatwa,” alisema Kulinangwa.

Naye, Mwenyekiti wa Serikali ya Kijiji cha Maguruwe, Sultan Nkumba, alisema taarifa za watu hao kuanzisha kijiji msituni, ziko wilayani lakini hakuna hatua zozote zilizochukuliwa.

“Hali ya msitu ni mbaya, wajanja wamejimilikisha ardhi humu msituni, ni wababe na wanalima na kufanya watakavyo, wanawinda wanyama, wanakata miti ovyo, wanafanya biashara ya kuuza msitu kwa kujimilikisha mashamba na kuwauzia watu wa Dar es Salaam.

“Sisi tumechukua hatua zote, lakini Serikali imekaa kimya, tunadhani kuna watu wanafaidika na hali hiyo kwani watu hao kutwa nzima wanachoma moto msitu, tukijaribu kwenda kuzima wanatutishia kwa mapanga, mishale na silaha nyingine, Serikali inasikia, lakini haichukui hatua, kuna nini hapo? Alihoji.

Akizungumza na Rai Jumatatu, mmoja wa wakazi hao wa msituni, Alistides Kyamani, alisema wanaishi msituni kwa mujibu wa sheria na kwamba wanajishughulisha na kilimo kama sehemu ya kutimiza kauli mbiu ya Kilimo Kwanza.

DC azungumza

Mkuu wa Wilaya ya Kisarawe, Fatma Kimario, alipokuwa akizungumza na Rai Jumatatu mwishoni mwa wiki, alisema anakitambua kijiji hicho kwa kuwa kiliwahi kutembelewa na Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya hiyo.

“Mimi na kamati yangu ya ulinzi na usalama tulikwenda katika eneo hilo na kushuhudia hiyo bendera nyekundu.

“Tulipozungumza nao, walituambia hawawezi kuondoka vinginevyo wauawe. Kwa hiyo, ninachoweza kusema ni kwamba, kitendo cha kupeperusha bendera nyekundu ni cha hatari, nasema huo ni uhalifu na tishio la amani, ninadhani wanafanya hivyo ili kujihami.

“Vikundi vya wakulima tunavijua, lakini mbona hatujasikia vinatundika bendera? Hili hapana kwa sababu kikundi hicho kimetafuta mbinu za kujihalalishia kuishi katika msitu huo kinyume na Sheria ya mwaka 1954, inayotambua mipaka halali ya Msitu wa Kazimzumbwi,” alisema Mkuu wa Wilaya.

Hata hivyo, alisema suala hilo limekwishatatuliwa na wizara zinazohusika, kinachosubiriwa ni tamko rasmi la Serikali pamoja na kufanya mkutano mkubwa wa hadhara kuwaambia wananchi hao waliojianzishia kijiji chao msituni waondoke kabla vyombo vya dola havijatumia nguvu kuwahamisha.
Chanzo: Mtanzania

No comments: