Tuesday, November 5, 2013

Mulugo, Prof. Mchome wapingana


 
na Happiness Mtweve
WIKI moja tangu Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Prof. Sifuni Mchome, atangaze mfumo mpya wa upangaji alama za matokeo ya wanafunzi wa sekondari kwa kufuta daraja sifuri na kuanzisha daraja la tano, naibu waziri ameibuka na kupingana naye.

Naibu waziri huyo, Philipo Mulugo, aliibua mkanganyiko huo bungeni jana, akisema si kweli kwamba serikali imefuta daraja la sifuri katika mitihani ya kidato cha nne kama ilivyoeleweka.
Kutokana na kukinzana huko, Spika wa Bunge, Anne Makinda aliiagiza serikali kuleta bungeni mabadiliko ya madaraja hayo ya ufaulu kwa  wanafunzi wa kidato cha nne na sita yaliyotangazwa hivi karibuni.

“Naibu Waziri nenda mtuletee kauli ya Serikali kuhusiana na utaratibu huo ili kuweza kupata majibu ambayo yanaridhisha,” alisema.
Awali akijibu swali la nyongeza la Mbunge wa Viti Maalumu, Catherine Magige (CCM), Mulugo alisema taarifa zilizoenea kwamba daraja la sifuri limefutwa si za kweli.

Katika swali lake, Magige alitaka kujua kama uamuzi wa serikali wa kushusha madaraja katika mitihani ya kidato cha nne lengo lake ni kuwaokoa wanafunzi wanaofeli.
“Serikali haijafuta divisheni sifuri na wala hakuna daraja la tano, yaliyopo ni la kwanza, pili, tatu, nne na sifuri kama kawaida,” alisema.

Alisema unamuzi wa kushusha madaraja uliofanywa haukuwa na lengo la kuwaokoa wanafunzi wanaofeli bali ni kuondoa mrundikano wa alama katika daraja moja.
Alisema serikali imeweka madaraja mapya kwa kutofautisha alama kumi kumi kutoka daraja moja kwenda jingine na kwamba hata hivyo alama za ufaulu bado ni 40 ambazo ni daraja la C.

Awali akijibu swali la msingi la Magige, Mulugo alisema serikali haina mpango wa kuanzisha programu maalumu hasa za ufundi kwa wanafunzi waliofeli katika mtihani wa kidato cha nne mwaka jana.

“Kwa mwaka 2013, jumla ya wanafunzi 60,507 wa kujitegemea, wamejisajili kufanya mtihani huo, watahiniwa 3,578 wakiwamo wasichana 2,020 na wavulana 1,558 waliofeli katika mtihani wa kidato cha nne mwaka jana wamejisajili kurudia mtihani huo,” alisema.
Alisema kwa sasa katika vyuo vya Ufundi Stadi kuna programu za fani mbalimbali za muda mfupi na muda mrefu ambazo wanafunzi waliomaliza elimu ya msingi na sekondari wanaweza kujiunga kwa vile mafunzo yatolewayo katika vyuo hivyo huzingatia stadi moja tu.

“Serikali imekuwa ikiongeza na kuboresha vyuo vya ufundi na kuweka mazingira rahisi kwa wanafunzi ili waweze kupata stadi mbalimbali,” alisema.
Mulugo aliongeza kuwa kati ya mwaka 2010 hadi 2012, serikali kupitia VETA imesajili jumla ya vyuo vya Ufundi Stadi 75 sawa na asilimia 75 na asilimia 10.8 ya vyuo 618 vilivyokuwapo.

Naibu waziri huyo alifafanua kuwa  katika kipindi hicho, jumla ya vyuo vinane sawa na asilimia 3.2 ya vyuo 248 vilivyokuwepo vilisajiliwa na NACTE.
Chanzo: Tanzania Daima

No comments: