Tuesday, November 5, 2013

Makinda aeleza kasoro kisheria



Dodoma. Spika wa Bunge, Anne Makinda amesema Sheria ya Marekebisho ya Sheria ya Mabadiliko ya Katiba 2013 ambayo ilipitishwa na Bunge katika mkutano uliopita, ilikuwa na kasoro nyingi ambazo zingekwaza kuanza kwa Bunge Maalumu la Katiba.
Kutokana na hali hiyo, Spika Makinda ameliambia Mwananchi kuwa kulikuwa na ulazima wa kufanya marekebisho katika sheria hiyo hata kama Rais Jakaya Kikwete asingekutana na vyama vya siasa na kukubaliana kuleta marekebisho katika kikao cha Bunge kinachoendelea hivi sasa.

Licha ya Makinda kutokuwa tayari kuweka wazi kasoro hizo, gazeti hili limebaini kuwa mambo hayo hayatofautiani sana na yale yaliyobebwa kama ajenda na vyama vya upinzani vilipokutana na Rais Kikwete, hivyo kuwezesha kuanza mchakato wa sheria hiyo kupitiwa upya.

“Labda nikwambie hivi katika muswada ule uliopitishwa siwezi kusema kilitokea nini, lakini kimsingi kuna administrative issues (masuala ya kiutawala) nyingi ambazo kama sheria ikibaki ilivyo, hata Bunge la Katiba haliwezi siyo tu kufanya kazi, bali hata kuitishwa,”alisema Makinda.

Uchunguzi wa gazeti hili umebaini kuwa Ofisi ya Bunge tayari imewasilisha mapendekezo yake Serikalini ikiainisha maeneo yapatayo kumi yenye kasoro zinazopaswa kufanyiwa kazi.
Katibu wa Bunge, Dk Thomas Kashililah alikiri kwamba ofisi yake imewasilisha mapendekezo yake Serikalini, lakini kama ilivyokuwa kwa Makinda hakuwa tayari kuingia undani wa mapendekezo hayo.

Juzi Serikali ilikuwa ikifanya majadiliano ya mwisho na wawakilishi wa vyama vyenye wabunge kuhusu marekebisho yanayopaswa kufanywa katika sheria hiyo, ambapo Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge), William Lukuvi alisema muswada huo ungewasilishwa jana kwa Katibu wa Bunge.

Dk Kashililah alisema walibaini upungufu kwenye sheria hiyo baada ya muswada kupitishwa na Bunge Uchunguzi wa Mwananchi umebaini kuwa Ofisi ya Bunge imefanya uchambuzi wa kina kuhusu umuhimu wa kuendelea kuwapo kwa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, tofauti na uamuzi wa awali wa kuvunjwa kwa tume hiyo.
Chanzo: Mwananchi

No comments: