Tuesday, November 12, 2013

Uhusiano kati ya Zimbabwe na China wanoga



Serikali ya Zimbabwe, imetia saini mkataba na benki ya serikali ya China kuinua hadhi ya mradi wake wa kuzalisha kawi ya maji katika bwawa la maji la Kariba.
Waziri wa fedha wa Zimbabwe, Patrick Chinamasa, alisema kuwa benki hiyo hutoa mkopo wa takriban dola milioni tatu hadi ishirini kwa mradi huo ambao utasaidia kumaliza tatizo la uhaba wa umeme huku serikali ya China nayo ikitoa ufadhili wa ziada.
Zimbabwe imekuwa ikiimarisha uhusiano wake na China hasa baada ya Marekani na Ulaya kuiwekea nchi hiyo vikwazo.

Waziri Chinamasa alisema kuwa mkopo huo utalipwa na Zimbabwe pamopja na riba ya asilimia mbili kila mwaka kwa miaka ya kwanza tano na kisha kulipa mkopo utakaosalia kwa miaka 20.
Pesa hizo zitatumiwa kuongeza uwezo wa bwawa la kuzalisha kawi ya maji kwa megawati 300.
Zimbabwe huzalisha kawi yenye megawati 1,200 kwa kawaida kila siku ikilinganishwa na mahitaji ya megawati 2,100 kila siku.

Ili kukabiliana na uhaba wa umeme wakati mahitaji ni makubwa, baadhi ya sehemu za mji husalia bila umeme kwa hadi masaa kumi hususan katika miji mikubwa.
Zimbabwe imeendelea kuimarisha uhusiano wake na China baada ya kutofautiana na nchi za Magharibi.

Marekani na Ulaya ziliiwekea nchi hiyo vikwazo, ikiwemo vya usafiri pamoja na kupiga tanji mali zake Rais Robert Mugabe na washirika wake baada ya uchaguzi wa mwaka 2002, ambao waangalizi wa Ulaya walisema ulikumbwa na visa vya wizi wa kura na kwamba Mugabe hakushinda kwa njia halali.

No comments: