Monday, November 4, 2013

Wabunge kuzibwa midomo




na Mwandishi wetu, Dodoma
WABUNGE wanaotumia nyaraka za siri za serikali, Bunge au taasisi yoyote ya umma kulipua mabomu mbalimbali ndani na nje ya Bunge, kuanzia sasa 'watakiona cha moto' iwapo watakutwa nazo.

Mbali na nyaraka hizo, pia watakumbana na kibano iwapo watazomea au kufanya vurugu zitakazosababisha kuahirishwa kwa shughuli za Bunge.
Vibano hivyo vinatokana na mwongozo wa kanuni za maadili ya wabunge ambazo zinatarajiwa kupitishwa wakati wowote kuanzia sasa.

Tanzania Daima limedokezwa kuwa mbunge atakayekutwa na nyaraka za siri zinazohusu utendaji wa serikali bila kibali cha mamlaka husika, atahesabika ametenda kosa na atachukuliwa hatua.

Chanzo kimoja kimelidokeza gazeti hili kuwa kanuni hizo zinamzuia mbunge kutumia taarifa zozote atakazozipata kwa wadhifa wake wakati akitekeleza shughuli za Bunge au kamati kwa ajili ya kujinufaisha, kujipatia fedha au kujipatia umaarufu.
Pia inaelezwa kuwa mbunge haruhusiwi kutoa taarifa zozote za siri za Bunge anazozifahamu bila idhini ya mamlaka husika.
Tanzania Daima limeelezwa kuwa kanuni hizo zinakataza mbunge kumtuhumu mwenzake kwa jambo lolote bila ya kuwa na ushahidi.

Baadhi ya wabunge waliozungumza na Tanzania Daima, wamebainisha kuwa kanuni za maadili hayo zinalenga kuwaziba midomo wanaonekana kutumia nyaraka mbalimbali kuibua madudu yanayofanywa na serikali, taasisi au idara zilizopo chini yake.
Waliongeza kuwa kanuni hizo zina lengo la kurejesha nyuma dhana ya Bunge kuisimamia serikali, na badala yake zinajenga mazingira ya serikali kulimeza Bunge.

Walibainisha kuwa mwongozo wa kanuni za maadili ya wabunge utaisaidia serikali iendelee na madudu yake ambayo katika siku za hivi karibuni yamekuwa yakianikwa bungeni na wabunge mbalimbali.
“Bunge linataka kuingia kwenye historia mbaya, yaani linajipa kazi ya kulinda uovu wa serikali, hii ni aibu sana. Sisi hatutakubali kupitisha mambo haya, tunasubiri siku ya kuyajadili,” alisema mmoja wa wabunge.

Chanzo kingine pia kimedokeza kuwa kanuni za maadili ya wabunge pia zinawazuia wabunge kujihusisha na vitendo vya udhalilishaji, unyanyasaji wa kijinsia baina yao au vitakavyowashushia hadhi katika jamii.
Tanzania Daima, limedokezwa kuwa wabunge hawataruhusiwa kujishirikisha na watu au vyombo binafsi kwa ajili ya kujipatia maslahi ya kifedha au mali yoyote inayoweza kuathiri utendaji wa kazi za Bunge.

Inasemekana baadhi ya mambo yaliyomo kwenye kanuni hizo ni yale yanayotajwa kwenye sheria za nchi, ikiwemo viongozi na watumishi wa umma kutoa tamko la mali walizonazo.
Jingine linalodaiwa kuwemo kwenye kanuni hizo ni mbunge anapaswa kuepuka mgongano wa maslahi, vitendo vya rushwa, kutokuwa na ubinafsi na kutopokea au kutoa zawadi kwa ajili ya kutekeleza majukumu yake.

Kanuni hizo zinadaiwa kumlazimisha mbunge kuweka wazi umiliki wa hisa kwenye kampuni, taasisi au asasi yoyote inayosimamiwa na kamati za Bunge.
Mbunge huyo pia atatakiwa kutoa taarifa kwa spika ili asipangwe kwenye kamati zinazosimamia taasisi hizo lengo likiwa ni kuepusha mgongano wa kimaslahi.
Pia kanuni hizo zinamtaka mbunge kushirikiana vyema na watumishi wa Ofisi ya Bunge, taasisi za umma, waandishi wa habari, asasi zinazojitegemea na makundi mbalimbali kwenye jamii.

Kanuni hizo pia zinaweka wazi kwamba uamuzi wowote ya vikao vya kamati ya uongozi utatolewa hadharani na spika au afisa yeyote wa Bunge kwa idhini ya spika.
Tanzania Daima lilizungumza na Naibu Spika Job Ndugai, juu ya kanuni hizo ambazo alisema bado hazijafikishwa bungeni kwa uamuzi, lakini anazikaribisha kwa mikono miwili.

Ndugai alisema amefurahishwa na kipengele kinachomtaka mbunge kuweka wazi umiliki wa hisa kwenye kampuni, taasisi au asasi yoyote inayosimamiwa na kamati za Bunge.
“Hizo kanuni zitatusaidia sana kwani kuna baadhi ya wabunge wamekuwa wakizizungumzia kampuni fulani kwa ubaya au mema, lakini kumbe wanamiliki hisa, sasa tutawatambua,” alisema.

Ndugai aliongeza kanuni hizo zikifikishwa bungeni zitajadiliwa kwa kina kama kuna vitu vya kuongeza au kupunguza na baadae zitapitishwa na kuanza kutumika rasmi.
Chanzo: Tanzania Daima

No comments: