Monday, November 4, 2013

Kerry ataka demokrasia na utulivu Misri



Waziri wa mambo ya nje wa Marekani John Kerry na mwenzake wa Misri Nabil Fahmy
Ikiwa ni ziara yake ya kwanza kutembelea Misri tangu kung'olewa madarakani kwa Rais Mohammed Morsi, Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani, John Kerry ametaka kumalizwa kwa aina zote za ghasia na kutaka kuwepo maendeleo ya kidemokrasia nchini Misri.

"Historia imeonyesha kuwa demokrasia inakuwa imara zaidi na kustawi kuliko njia nyingine yoyote ile," ameuambia mkutano wa waandishi wa habari mjini Cairo.
"Kwa kuwa na utulivu unakuja utalii na uwekezaji, kwa vyote viwili, zinakuja fursa za ajira kwa wananchi wa Misri."

Amesema, Misri ni mshirika "muhimu" wa Marekani.
Mwezi uliopita Marekani ilisitisha kubwa ya msaada wa dola bilioni 1.3 za Kimarekani, ambazo nchi hiyo imekuwa ikiipatia Misri. Misri ilikasirishwa na hatua hiyo ya Marekani.
Bwana Kerry amesema uamuzi huo ni taswira ya sheria ya Marekani" lakini msaada uliokuwa ukielekezwa moja kwa moja kwa wananchi, umeendelea kutolewa.

Uhusiano wa mataifa haya mawili umekuwa wa kihasama tangu kupinduliwa kwa Rais wa Kiislam Mohammed Morsi mwezi Julai, huku utawala mpya ukifanya msako dhidi ya waandamanaji. Mamia ya watu wameuawa tangu wakati huo.
Bwana Kerry amesema amekuwa na mazungumzo na waziri wa mambo ya nje wa Misri Nabil Fahmy kuhusu kumalizika kwa aina zote za ghasia nchini Misri.

"Vitendo vyote vya ugaidi nchini Misri lazima vikomeshwe- vitendo vyote", amesema.
Bwana Kerry yuko nchini Misri, ikiwa ni mojawapo ya nchi anazozitembelea katika eneo la Mashariki ya Kati na kaskazini mwa Afrika.
Chanzo: BBCSwahili

No comments: