Saturday, November 2, 2013

HATIMAYE TZ KWA HERI SIFURI KARIBU DIVISION V




Serikali imefanya marekebisho ya upangaji wa viwango vya alama kwa wanafunzi wa kidato cha nne, sita pamoja na matumizi ya alama endelevu ya mwanafunzi kwa ajili ya kuamua kiwango cha ufaulu wa wanafunzi.

Marekebisho hayo yametokana na maoni ya wadau wa elimu ambapo kwa muda mrefu sasa, upangaji viwango vya alama vinavyotumika katika mitihani ya kuhitimu kidato cha nne na sita, haufanani wakati mitihani yote ni ya sekondari.
Katibu Mkuu Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Profesa Sifuni Mchome, aliyasema hayo Dar es Salaam jana wakati akizungumza na waandishi wa habari na kufafanua kuwa, muundo huo utatumika kwa miaka minne.
\
"Utatumika kwa miaka minne kabla haujahuishwa ili kuupa muda wa kutosha kuona aina ya changamoto zinazojitokeza na jinsi ya kuzishughulikia," alisema Prof. Mchome.
Marekebisho hayo ni utekelezwaji wa Mpango wa Matokeo Makubwa Sasa katika sekta hiyo (Big Results Now), ambapo daraja sifuri, limefutwa na kuwekwa daraja ambalo litafahamika kama daraja la tano.

"Daraja la tano ndio la mwisho kabisa katika ufaulu, mabadiliko haya yatapunguza idadi ya wanafunzi wa wanaofeli kuanzia 2013 (kidato cha nne) na kidato cha sita 2014.
"Kuanzia sasa, daraja la kwanza I, litaanzia pointi 7-17, II (18-24), III (25-31), IV (32-47) na daraja la V (48-49)," alisema.

Awali, katika muundo wa zamani, daraja la I lilianzia pointi 7-17, ambayo haijabadilishwa, II (18-21), III (22-25), IV (26-33) na daraja sifuli lilianzia pointi 34-35.
Alifafanua kuwa, daraja la kwanza ni kundi la ufaulu ambao umejipambanua na bora sana, II ufaulu mzuri sana, III ufaulu mzuri na wastani, IV ufaulu hafifu na V ufaulu usioridhisha.

Aliongeza kuwa , alama endelevu mwaka 2013 kwa wanafunzi wa kidato cha nne, tayari zimewasilishwa Baraza la Mitihani nchini (NECTA), ambapo alama hizo zichangie asilimia 40 katika mtihani wa kidato cha nne mwaka huu.
Prof . Mchome alisema , wataalamu wa mifumo ya mitihani, watalifanyia kazi zaidi suala la madaraja liweze kutumika kwa ufanisi katika kipindi hiki cha mpito.

"Mabadiliko hayo yamefanyika ili kuendelea kuimarisha mfumo wa elimu, kuweka wazi taratibu mbalimbali kwa ajili ya mitihani na masuala mengine.
"Sera ya elimu na mafunzo ya 1995 imeelekeza kwamba, katika kuamua kiwango cha ufaulu wa mwanafunzi wa sekondari, alama za tathmini endelevu ya mwanafunzi zitachangia asilimia 50 na mtihani wa mwisho asilimia 50.

"Upande wa Zanzibar, alama hizi zimekuwa zikiandaliwa kwa mfumo wa asilimia 40 na mtihani wa mwisho asilimia 60," alisema na kuongeza kuwa, wadau wengi walishauri muundo uliopo sasa wa madaraja, uimarishwe na kuanza kutumia muundo wa wastani wa alama katika ufaulu (GPA) ambao ni rahisi kueleweka.
Alisema matumizi ya muundo wa GPA ni rahisi kukadiria uwezo wa mwanafunzi kielimu na kufanya maamuzi yakiwemo ya kuendelea na masomo katika ngazi mbalimbali za elimu.

"Kutokana na idadi kubwa ya wanafunzi walio katika mfumo wa elimu wapo katika ufaulu hafifu, Serikali imeona kuna mambo mengi ambayo hayana budi kuendelea kuimarishwa," alisema.
Mambo hayo ni pamoja na mfumo wa mitaala, walimu, mazingira ya kujifunzia, kufundishia, vitabu na vifaa vingine muhimu.
Katika hatua nyingine, Wizara hiyo imesema mtihani wa kidato cha nne na mtihani wa maarifa mwaka huu, unatarajiwa kufanyika nchini kote kwa siku 18 kuanzia Novemba 4 hadi 21.

Prof. Mchome alisema watahiniwa walioandikishwa kufanya mtihani huo ni 427,906 kati yao 367,399 wa shule 60,507 watahiniwa wa kujitegemea.
Aliwataka walimu, wasimamizi wa mitihani, wakuu wa shule, viongozi na jamii kuhakikisha mitihani inafanyika katika hali ya amani, utulivu na asitokee mtu akajaribu kuharibu taratibu kwani ni kosa la jinai na atachukuliwa hatua.

"Uharibifu wa taratibu hauna faida katika jamii kwani mitihani ya kidato cha nne ni muhimu katika Taifa kwa maendeleo ya jamii na sekta ya elimu.
"Natoa wito kwa kamati za mitihani mikoa yote, kuhakikisha taratibu zote za utunzaji, uhifadhi na usafirishaji wa mitihani zinazingatiwa," alisema.
Alisema hadi sasa maandalizi na usafirishaji mitihani hiyo ngazi ya Mkoa, yamekamilika pamoja na usalama wa mitihani ambapo hakuna uliovuja katika ngazi yoyote kuanzia NECTA, mikoa na halmashauri
Chanzo: Majira

No comments: