Friday, April 6, 2012

MAPENZI NA MWANAHARAKATI

MAPENZI

Kila binadamu hupenda jambo fulani. Mapenzi ya mtu juu ya jambo yaweza kumvutia kiasi kwamba anaweza kupoteza welekeo wa maisha yake. Watu hupenda hadi kileleni. Hapa ndipo mtu aelewi hili wala lile. Hali hii si tu kwa vijana wanaoingia katika umri wa balehe bali hata kwa wale waliovuka umri huu. Kweli kila mtu anahaki ya kupenda. Na mapenzi haya yalianza pale binadamu walipoanza kuishi pamoja kama mke na mume au kama vitabu vyetu vya dini vinavyoelekeza, ambavyo ni Biblia na Koruhani.

Napenda kuwa muwazi sana juu ya aina ya penzi ninalozungumzia. Ni yale mahusiano ya kimwili yaliyopo kati ya mwanamke na mwanaume. Haya ndiyo mahusiano ninayozungumzia na sizungumzii yale ya watu wa jinsia moja. Mapenzi hayauzwi na ayachagui rangi wala kabila.Mapenzi ni kitu asilia ambacho humkuta mtu juu ya mtu mwingine ambaye anaweza kuwa mwanamke kwa mwanaume au kinyume chake. Na hawa kila mmoja hutokea kumpenda mwenzake mpaka kufikia kilele cha penzi.

Angalia mfano huu; umepita wapi na kutembelea mikoa mbalimbali au wilaya, tarafa, kata, vijiji na mitaa mingapi? Umekutana na wangapi wazuri (wanawake au wanaume), na ulimpenda yupi. Inawezekana kati ya uliowachagua hakuna hata mmoja kati ya wale uliokutana nao ukaridhia kuwa naye. Lakini ulikutana na kijana mmoja ambaye amekuvutia sana na mahusiano kuanzisha mpaka leo ni mke wako au mchumba wako. Hapo ndipo ninaposema “love is something natural” na si kitu cha kubahatisha tu.

Na ieleweke kwamba mke mzuri ni wako tu, na mume mzuri ni wako tu. Hakuna ubishi kwa hili. Na pale unapoona kuwa mke au mume wako si mzuri basi ulikosea wakati wa uchaguzi wako. Hapo huna budi kuonyesha unampenda kama kitabu hiki kinavyoeleza uk.2 & 3. Na ujue kwamba kila mtu ana haki ya kupendwa na mume, mke au mchumba wake. Penye upendo pana mapenzi ya kweli.

NINI MAANA YA MAPENZI?

Neno mapenzi ni pana sana. Na kila mtu huweza kufikiri kulingana na uelewa wake juu ya mapenzi kati ya mtu na mtu. Mapenzi ni ile hali asilia ambayo mtu anakuwanayo kwa mtu mwingine na inapaswa kuwa na makubaliano baina ya wahusika ambayo yaweza kuwa ya muda mfupi au muda mrefu. Wengine husema mapenzi ni ile hali ya mtu kuwa na mahusiano ya kimwili  na mwingine ikihusisha mwanamke na mwanamme.

Kipindi tulichopo sasa ni kipindi cha utandawazi. Si mtoto mdogo si wakubwa wote wanayafahamu mapenzi yalivyo. Kwa sasa imekuwa kawaida kwa kila mtu kuanza uhusiano hata kabla ya kufunga ndoa. Hii ndiyo ninayoita utandawazi. Watoto wadogo hupata habari hizi kupitia masimulizi kutoka kwa kaka na dada zao nyumbani au nje. Hii haikuwa tamaduni yetu, lakini sasa ni jambo la kawaida kwa mwanafunzi wa darasa la tano kukutwa na ujauzito. Lakini ni kwa mazingira hayahaya.

Kipindi hiki ndicho kipindi kigumu kwa vijana kujua yupi ni mke/mume mwema na yupi si mke/mume mwema. Athari hizi huwakuta sana akina dada ambao wakizidisha miaka ishirini na saba, yule ambaye alikuwa mume mzuri anampoteza ndani ya miaka 18 hadi miaka ishirini. Ndani ya miaka hii mwanamke huvutia na anaonekana kama ua linalovutia wadudu (Dr Isack Ndodi, 2011). Nakubaliana sana na maneno ya Dr. Ndodi akizunguma Channel 5 kati ya mwezi Mai hadi Juni, 2011.

Kuna ukweli uliopo juu ya hili. Ndani ya miaka hii mwanamke ujikuta anaingia katika majaribu yasiyo na msingi huku akijitahidi kutafuta mume mzuri kwake, na matokeo yake huishia kuchezewa na hatimae kukosa wote. Wanaume ndio wasababishaji wakubwa wa mke huyu asiolewe au asipendwe. Angalia mfano huu, mti ukichipuza maua utamuona mdudu wa kila aina akiwemo nyuki, nzi, kipepeo na wengine wemgi wakiingia na kutoka. Haya ndiyo yaliyopo kwa wanawake kwa kipindi hicho tajwa hapo juu.

Hapa lile neno langu love is something natural (mapenzi ni kitu cha asili) hutumiwa vibaya na badala yake mapenzi hupoteza umaana wake. Kwa kila mtu mwenye upendo wa kweli hawezi kumdarau mchumba au mke/mume wake. Na inapotokea vinginevyo ni makosa ya kibinadamu ambayo hutokea baina ya hawa wapendanao.

 

NINI MAANA KUPENDA AU KUPENDWA

Inawezekana si mara yako ya kwanza kusikia nini kupenda. Haya yamewai kuzungumzwa na msanii wa muziki Mwijuma Mumini. Neno kupenda lipo katika nyoyo za binadamu na uwezi kuona kwa macho. Kwa kifupi ni neno la kufikirika tu. Lakini utagundua kweli unapendwa na kupenda mara baada ya kukutana na mke, mume au mchumba wako. Matendo ndiyo yanayoonyesha kweli unapendwa au unampenda.

Kwa kawaida mtu anayetaka kuwa na mahusiano na wewe huanza kuonyesha kwa sura pamoja na maneno yaliyojaa utamu. Na mara uyasikiapo maneno hayo ndipo hamu na shauku ya kuendelea kuwa naye inakujia na hatimaye mwisho wa siku mnaamua kuwa na makubaliano. Kwa kuwa utamaduni wa baadhi ya jamii katika bara letu la Afrika unamnyima mwanamke kutamka neno nakupenda kwa mwanaume, basi hapo lugha itayotumika ni ile ya ishara ya kuweza kumvutia mwanaume kwa kila hali ili awe naye katika ukrasa wa mapenzi.
Na pale mwanamke anapotamka neno nakupenda “I love you” kwa mwanaume, inaonekana mwanamke yule ni mmalaya wa hali ya juu. Hii ni tofauti na nchi za Magharibi ikiwemo Marekani ambako mwanamke au mwanaume ana uwezo wa kuomba uhusiano wa kimapenzi. Kwa Tanzania kulikuwa na neno “USIONE SOO SEMA NAYE”. Hili neno lilikuwa zuri kuwapa utambuzi wanawake wa kiafrika kuweza kuomba uhusiano wa kimapenzi kwa mwanaume ampendaye na si kutegemea afuatwe.


Tabasamu zito, na tabia ya mwanamke huanza kuonyesha kuwa ni bora au mzuri kuliko za wengine. Lingine ni kwamba maneno ya kumsifu mtarajiwa yanakuwa mengi. Mara umependeza, mara leo tutoke out (kwenda kupumzika eneo fulani kama vile maeneo ya starehe au sehemu yeyote waipendayo watarajiwa). Na hapo ndipo mmoja kati yao huanza kutamka neno linalostahili ili kuwezesha mahusiano, na kuna wengine hufikia kutamka hata kama ni siku ya kwanza kuonana/kukutana. Haya ni baadhi tu ya mambo yanaoonyesha kuwa mtu anapenda au anapendwa kabla ya kuanza mapenzi motomoto.

 

MWANZO WA MAPENZI

Mapenzi huanza na moto wa hali ya juu. Kila mmoja anataka na kupenda kukaa wote muda wote. Kila neno linalozungumzwa na mmoja wao huonekana zuri na la thamanmi sana. Hapo ndipo mke au mwanaume anaweza kuamua kutoloka kwao na kumfuata mwenzi wake. Hapa wapendanao hujikuta kama wapo nchi nyingine. Maneno ya utamu kama neno nakupenda hutamkwa kwa sana tena kwa mkazo kwa wakati wote.

Kila mmoja huona amefika sana. Na mara nyingi mtu awezi kuamini jambo lolote analoambiwa na mtu mwingine. Haya yameonekana sana katika Tamthilia zinazopendwa na vijana wengi kama zile za nchi za Magharibi. Mfano ni ile iliyogusa nyoyo za watu wengi maalufu kwa jina la “Malichui” au AN ENGEL. Na LOVE TO DEATH.

Penzi hufikia kileleni na wengine huanza hatua za utambulisho kwa wazazi. Kwa sasa utambulisho huu hufanya na mototo mwenyewe. Hii ni tofauti na miaka ile ya nyuma ambapo mume au mke huchaguliwa mke au mume na wazazi wake. Haya ndiyo mambo ya sasa. Kila kitu uwekwa wazi na wapendanao wenyewe.

Kwa wale wanaobahatika kuweza kufunga harusi uweza kufunga harusi na wangine huishia njiani bila mafanikio kutokana na sababu mbalimbali zilizo nje au ndani ya uwezo wao. Sababu ni nyingi hivyo mwandishi hakuweza kuzitaja zote lakini uk 4 & 5 zinajieleza wazi.

 

KUTENDWA

Hili ni neno lililoibukia siku za hivi karibuni na kuonekana kuwa na umaarufu sana miongoni mwa vijana. Watu hutumia neno hili wakimaanisha kuachwa na mwenza au mpenzi pasipo kutarajia kutokana na matendo aliyofanyiwa. Hii ndiyo tafsiri yake. Ni mara nyingi sana jambo kama hili limewatokea wapendanao. Wangine husema amemwagwa au amebwagwa chini. Hii ni misemo ya vijana wetu wa siku hizi. Inawezekana kwa wengi, na si wewe tu umewai kusikia neno hili la kutendwa. Si geni kiasi kwamba mtu anaweza kutoelewa kinachoozungumzwa.

 

MAMBO MAKUU YANAYOSABABISHA KUTENGANA KWA WAPENDANAO

  1. Kutofanya uchaguzi ulio sahii wa mke/mume au mchumba. Vijana wengi siku hizi hujilaumu sana juu ya chaguo la mwenza wake. Ukikosea mwanzo ujue utaoa na kuacha mke zaidi ya mmoja. Pakifikia mahali unaanza kutamani wanawake/mwanaume wa nje na kumsahau wako wa ndani ujue ni ishara kwamba hukufanya chaguo zuri ujana wako.
  2. Wazazi kutopendezwa na mke/mume. Hapa wazazi nawazungumzia wale wanaopenda kuingilia mambo ya ndani ya watoto wao. Kuna watu wanaitwa mawifi, hawa ndio chokochoko kubwa la mke na mume kutengana. Watatumia maneno ya uzushi na unafiki ili mradi mke au mume yule waachane. Mwisho ndoa au uchumba unavunjika.
  3. Utofauti wa dini. Hili ni suala la mdahalo karibu dunia mzima. Inapotokea mume na mke wameanzisha uchumba, na kila mtu ana dini yake, mwanzo wa penzi hakuna aneyekumbuka nini athali kwa hapo baadaye. Muda unasonga, na kila mmoja anahitaji afunge ndoa au pingu za maisha au wazazi wafahamu, hapa kila mmoja anaanza kukumbuka utofauti wao. Kutokana na imani kali au kutokuwa na uelewa mwanzo,wanaweza  kutengana ili kulinda maslahi ya dini au dhehebu la kila mtu. Hii mara nyingi hutokea kama mmoja wao ni Mkristo au Muislam. Katika ndani ya ukristo kuna misingi inayoongoza kanisa la SABATO. Hapa pia hawaruhusu muumini kuoa au kuolewa nje ya dhehebu hili   vinginevyo anatengwa na kanisa.
  4. kutofikia kilele wakati wa tendo la ndoa. Hakuna ndoa inayoweza kudumu kama tendo la ndoa halifanyiki. Au kama linafanyika ni kwa kulidhika mmoja tu na mwingine asitosheke. Hii ni sahemu muhimu sana inayomfanya mke au mume aweze kuwa na mahusino na mtu mwingine ili aweze kujitosheleza. Kila mmoja hupenda atosheke, na inapotokea vinginevyo migogoro huanzia hapo na hatimae kuvunjika kwa penzi lao. Zao la hili ni kutoroka kwa mke/mume au mchumba na kuanzisha uhusiano na mtu mwingine hatimaye penzi kuvunjika.
  5. Tabia ya uzinzi kupindukia. Hapa nazungumzia tabia ya umalaya ya mwanamke au mwanaume nje ya mpenzi wake. Hawa ni watu ambao uzaliwa na genes za aina hiyo na wamerithi kutooka kwa wazazi. Hivyo kwa mtu aliyorithi inakuwa ni rahisi zaidi kutoka nje ya ndoa yake na kwenda kufuata wengine ili mradi atimize malengo yake. NB. Tumetoa njia za kutatua hili tatizo katika kitabu hiki.
  6. Maneno au mawasiliano. Namna mke na mume wanavyozidisha mawasiliano, ndivyo wanovyoongeza uhai wa penzi lao. Kwa zamani barua zilikuwa ndio chombo cha mawasiliano kama mmoja wao aliishi mbali. Lakini kwa sasa ni njia ya simu za mkononi. Inapotekea mawasiliano yanapungua kati ya mume na mke kinachofuata ni kusauliana. Kila mmoja atapata wazo la kuwa na mwingine na hatimaye kuanzisha mahusiano mapya na yule ambaye hakupenda kuwa naye. Usipokuwa makini juu ya hili lazima mutatengana tu. Pia suala la mawasiliano linaweza kuwa namna lugha inavyotumika baina ya wapendanao. Kwa mfano lugha ya dharau na ubabe wakati wote.
  7. Wivu. Hakuna penzi linaloweza kudumu kama hakuna wivu. Na wivu huo uwe wa kiasi ambacho akiwezi kuathili penzi lao. Kuna watu wana wivu kupindikia. Hili ni tatizo kubwa, na hakuna mtu anayependa afanyiwe wivu kiasi kwamba hadi mtu anakosa uhuru. Pakifikia mahali hapa wapendanao huanza kutoa maneno ya siri kwa jirani na mwishowe kutengana kwa wependanao. Hapa pia inaambatana na hali ya kutokuwa na imani na mwenza wako.
  8. Kuwa na mahusiano ya hali ya juu na mtu wa jinsia tofauti pamoja na utani. Mtu ukishaolewa, kuoa au kuwa na mchumba ni bora zaidi upunguze mahusiao na ya kupindukia na watu wa jinsia nyingine. Hali ya utani unaoambatana na kushikana, kubusiana pamoja na kuelezana maneno ya kimapenzi kwa wale ambao si mpenzi wako husababisha mgogoro na mwenza wako. Vinginevyo ndoa au uchumba ule utaelekea mahali pabaya na mwisho kuvunjika kwa penzi.
  9. Kusikiliza maneno ya watu. Kuna watu hupenda kuchonganisha wanawake au wanaume wa watu kwa maslai binafsi. Kwa kawaida watu hawa wapo kwa ajili ya kuona wapendanao wanagombana. Hivyo basi, kusikiliza maneno ya hawa watu kwa jina maalufu wambea inapelekea kubadili kwa mwenendo wa mweza na hatimaye kuwa mwisho wa penzi.
  10. Ugumba/utasa. Hii ni ile hali ya mmoja kati ya wapendanao kutokuwa na uwezo wa kuzaa. Yaani kwa mwanaume kushindwa kutoa mbegu zinazoweza kusababisha kutungwa kwa mimba, na kwa mwanamke kushindwa pia kutoa mayai yenye uwezo wa kupokea mimba. Hali hii huwaathiri sana wanawake ambapo mke huonekana mzigo katika nyumba. Wangine wanafikia mahali wanawaambia wapenzi wao kuwa “wanajaza choo tu”. Hii kauli lazima ipigwe vita sana. Madhara ya kauli zinazofanana na hii, yule mwenye kizazi huamua kumwacha yule asiye na kizazi na kwenda kuanzisha uhusiano mpya na mtu mwingine.

Hizo ni baadhi ya sababu za kimsingi zinazochangia uvunjifu wa ndoa au uchumba. Ukweli ni kwamba sababu zipo nyingi lakini zinazoumiza sana vichwa vya watu ni hizi.Hivyo kila mtu anapaswa kuwa makini juu ya mambo haya yaletayo mzozo katika penzi husika.

 



NAMNA YA KUTATUA NA KUEPUKANA NA MAMBO YAWEZAYO KUSABABISHA KUTENGANA

Kufanya uchaguzi sahihi wa mchumba. Kila mtu anashauriwa kuchagua mchumba anayekufaa. Si kila mwanamke au mwanaume ni mzuri kwako na kuanza maisha kama wanandoa. Jaribu kutafakari na kupata ushauri wa watu walio karibu naye ili upate juu ya tabia aliyonayo. Ukiona ni mzuri unaweza kuanza hatua za kufunga harusi.
Si vizuri kuparamia mwanaume au mwanamke unayekutana kwenye basi au kwenye mitandao ya kijamii kama facebook. Kweli watu wanamaneno matamu na mazuri sana, lakini walio wengi ni wababaishaji wa mapenzi. Jiulize swali dogo tu, ameonana na wanaume au wanawake kama wewe wangapi. Jibu ni wengi, hivyo kuwa mtulivu, siku ikiwadia utampata mzuri zaidi ya huyo (simahanishi mtengane na mume/mke au mchumba uliyenaye sasa kama mulianzisha uhusiano kupitia njia hizi).

Wazazi hawana budi kupewa elimu ya kutosha juu ya mke/mume au mchumba wako. Mwenye haki ya kuchagua mchumba ni wewe na sio wazazi wako. Wewe ndiye unayefahamu unampenda kiasi gani. Jaribu kuwashauri hadi wakuelewe kwa nini unataka kuwa na huyo mchumba wako. Hapa hauna budi kupunguza hasira kwani wazazi wengine wana tabia ile ya kuhukumu mtu mara tu baada ya kuanza kuongea naye.
Kama wapendanao hamna budi kuendelea kushirikiana nao kwa karibu, na mwisho wa siku hali waliyonayo itatoweka na badala yake uhusiano wenu utaendelea kukua. Usiwatamkie maneno makali wale wote wanaokupinga juu huyo mchumba wako. Kwa kufanya hivyo uhusiano wenu utadumu maisha milele.

Ni muhimu kuweka makubaliano juu ya dini za wapendanao. Hili ni jambo linaloumiza sana vichwa vya watu ulimwenguni. Suala hili ni suala la mdahalo usio na mwisho, na uhishia tu pale wapendanao wanapoamua kufuata majibu na mapatano yao.Kama mke/mume wako ni dini tofauti na yako, basi nakushauri muanze kupanga mikakati pale tu mutapoamua kuanza uhusiano wenu. Mweleze ukweli huyo mchumba wako juu ya dini yenu na mnavyoishi kule kwenu. Baada ya hilo muendelee kupanga hatima ya kizazi chenu na athari zipi zitawapata na mutatatua vipi hizo changamoto zote. Changamoto ambazo huathiri sana ni hatima ya watoto. Hapa kama msimamo haupo juu ya maamuzi yenu basi tambueni huo utakuwa mgogoro usio na mwisho. (Hapa nazungumzia tu kwa wale walio na wanaotarajia kuingia kwenye uchumba).
Kwa wanandoa kama walifanya maamuzi bila kujijua basi nashauri waendelee kufuata utaratibu wao na pale inaposhindikana muwaone wataalamu wa masuala ya mahusiano katika jamii wakiwemo watu wa ustawi wa jamii au taasisi zinazohusika na masuala ya utatuzi wa migogoro ya kifamilia au baraza la wazee.

Ni vizuri kumfikisha mwenza wako kileleni. Wanaume walio wengi hushindwa kuwafikisha wake zao kileleni. Hii yote inatokana na kushindwa kujua namna gani ya kumwandaa mke au mchumba wake ili afikie kileleni. Walio wengi wanaamini wakishafikia hatua ya kupezi mara mbili wanaona wamemfikisha mke kileleni. Nakushauri usome kitabu kilichoandikwa na Dr Paul Nelson. Mara nyingi husikika siku ya jumatano katika RFA (Radio Free Africa) kuanzia saa tano usiku.
Utajua namna ya kumfikisha mke wako au mume wako kileleni. Pia kuna wanaume ambao hukosa kufikia kileleni. Hii husababishwa na mke kutojua namna ya kumfikisha mume kileleni. Hivyo kupitia kitabu cha Dr Paul Nelson utaweza kujua sehemu zipi zinapaswa kuguswa ili kumfikisha kileleni mpenzi wako. Kitabu kinachozungumzia namna ya kumfikisha mpenzi wako kinaandaliwa. Kwa wale wapenzi wa facebook munaweza kutembelea ukrasa wangu wa facebook au Arasachi The Centre of Learning”
Kikiwa tayari muda wowote utakiona sokoni. Kitakuja na kichwa cha habari kisemacho “unafahamu namna ya kumwandaa mpenzi wako?”. Kulingana na mwili wa mwanamke ulivyo, unaweza kufanya tendo la ndoa hata masaa mawili na asifikie kileleni. Mke au mume akifanya vizuri juu ya hili hawezi kumtamani mume au mke mwingine kwa sababu utakuwa umemjenga kisaikolojia.

Ni vizuri kujizuia tabia ya umalaya kabla na baada ya kuanzisha uchumba. Hakuna mwenza anayependa kuona mke/mume wake anatabia ya umalaya. Wengi huzaliwa nayo na kurithi kutoka kwa wazazi. Na wengine hujengwa na makundi mchanganyiko katika jamii zikiwemo taasisi za kufundishia.
Kwa mfano Vyuo vikuu nchini Kenya au nchi za Magharibi ni kawaida kuwaona wanafunzi wakishikana sehemu mbalimbali za miili yao wakiwa maeneo tofauti tofauti ya shule au chuo chao (hawa ni wanalika “peer group”).
Muhusika hauna budi kujizuia kwa kuwa naye karibu yule mpenzi wako. Na inavyotokea unaishi naye mbali basi mtembeleane wakati wa likizo na kupata muda wa kuongea pamoja. Pia jiepushe kwenda maeneo ya starehe kama vile baa na ufukweni ukiwa pekeyako pindi mpenzi wako yuko mbali nawe. Kwa kufanya hili tabia yako utakuwa umeizuia na kuiacha kabisa.

Mawasiliano lazima yadumishwe. Mwanzo wa penzi mawasiliano huwa ni ya hali ya juu kwa sababu kila mmoja hupenda amjue vizuri mpenzi wake. Hii yote hutokea kwa sababu ya upendo walionao kwa kila mmoja kwa mwenza wake. Siku zinavyosonga mawasiliano huanza kufifia au kuongezeka kutegemeana na lugha inayoyumika. Hali ya kufifia mara nyingu hutokea tu mara baada ya kuanza zoezi zima la mapenzi kwa siku ya kwanza au kipindi maalumu.  Baadhi ya wanaume hukosa hamu ya kuendelea kuwa naye kama mpenzi wake. Lakini baada ya siku chache mkizidi kuwasiliana hali inarudi kama kawaida. Hii hutokea sana kwa wanaume, na kama kwa wanawake ni kwa kiasi kidogo sana. Hapa ndipo utapoona yule uliyempenda umetengana ghafla.
Mukifikia hatua hii mnapaswa kuendelea na mawasiliano. Kwani kitendo cha kutengana ghafla huwaumiza sana wanawake kwa sababu inaonekana lengo kubwa ni kumchezea na kumwacha. Ili kudhibiti hali hii mnatakiwa kudumisha mawasiliano na kuendelea kuwa karibu sana na baada ya wiki moja hali itarudi na kuwa na hamu ya kuwa na wewe muda wote. Hapo ujue kuwa hali imeshatoweka na sehemu iliyobaki ni ya kuendelea kujipangia mikakati juu ya mahusiano yenu ili kudumisha penzi lenu. (hali hii ni kwa baadhi tu ya watu na hutokea kama mke au mume hakuweza kumfikisha kileleni mwenza wake au hutokea asilia tu au kwa kupenda iwe hivyo





HATUA ZA KUJUA PENZI LINAPOTEZA UELEKEO.

Hatua kuu zinazoonyesha penzi limepoteza uelekeo ni hizi zifuatazo:-
1.      MAWASILIANO KUWA DUNI
2.      USO KUONESHA KUWA HAPENDI KUONGEA
3.      HASIRA ZA MARA KWA MARA
4.      MANENO YASIYOFAA HUANZA KUZUNGUMZWA
5.      KUDAI KUTENGANA
1. MAWASILIANO KUWA DUNI
Mapenzi ni sawa na jani la mti. Huendelea kuwa na mawasiliano na shina kwa kusaidiana na matawi. Ila siku ikifika jani hudondoka. Hii utokea pale jani linapochoka na maisha ya kujishikiza. Haya ndiyo sawa yaliyopo kwetu wanadamu. Mwanzo uanza kwa kasi sana na mwisho hufifia kwa mawasiliano. Mtu anaweza kukata mawasiliano kwa sababu zake binafsi zikiwemo hizo za hapo juu.

Kama mawasiliano yalikuwa ni mara tano kwa siku (kwa wale walio mbali, mfano masomoni, au katika harakati zingine za kutafuta maisha), basi mawasiliano huanza kushuka hadi mara mbili na mwisho wa siku mawasiliano hukaka kabisa. Hapa kila mmoja akiulizwa swali kwanini hali hii, husema nilibanwa na kazi ndio maana sikuweza kukutafuta a kukupigia simu (kama wapendanao wana sim za mkononi au mezani).
Kwa walio kwenye ndoa mawasiliano pia yanakuwa nyuma kidogo. Kama alikuwa anakusalimia kwa kukumbatiana, hapa hali huwa tofauti kabisa. Muda mwingine kila mtu na kazi yake. Kila mtu shuka yake, na kukicha kila mtu kivyake.

Hili uathari sana pale mmoja wa wapenzi anapokuwa na mpenzi mwingine. Yule ambaye ulidhani umemchagua anakuja ;kuwa sumu kwako. Unapenda umwone yeye hataki. Unapenda umpe zawadi yeye hataki, unapenda kwenda naye kwenye kumbi za starehe yeye hataki, na pale anaposema uwasiliane naye basi roho huweka pembeni. Utagundua kuwa analazimishwa aongee.

Ikifikia hatua hii na kama ulimpenda kweli, basi ongeza jitihada za kutaka kuwa naye, wasio na imani hufikia mahali wanasema nitaendelea kukaa bila kuoa. Kauli hii ni udanganyifu tu. Akisahau yale yaliyomtokea, huamua kusaka mke au mume mwingine. Unapoona hali hii imeanza jaribu kujilazimisha kuwa karibu naye sana. Na pale unavyoona hali ni mbaya zaidi basi mweleze rafiki yake wa karibu ambaye humwamini kwa kila jambo.

Au unaweza kumweleza mtu anayeheshimika ili asikilize kilio chako na mwisho wa siku utaona mafanikio. Hii ni kwa wote wachumba na hata kwa wanandoa kufanya hili.

Kwa wanandoa ni muhimu wawaone pia wezee wa busara ambao wanaaminika na kukubalika na jamii. Ikishindikana basi waende katika ofisi ya kata au ustawi wa jamii kwa msaada zaidi.

 

 

2. USO HUONYESHA KUWA HAPENDI KUONGEA

Ni hali ya kawaida kuona mke au mume kuonyesha kuwa hapendi kuongea na wewe. Sababu kubwa anayo moyoni na hataki kuisema. Uso mara nyingi unakuwa na asili ya mkunjo kwa wanawake. Na kwa wanaume sura inakuwa na asili ya makunyanzi. Hapo ujue kuwa hali ni mbaya sana. Hapo hata ukimsemesha huona kama unajisumbua tuu. Na kama ataamua kusema ni kidogo tu na mwisho huedelea kukaa kimwa.

Pia hata majibu yake uteyaelewa tu. Ni ya unyonge hivi, na sauti ya chini isiyo na mvuto au ushawishi kwa mwenza. Ikifikia hatua kama jalibu kumnunulia zawadi mzuri, kumbusu, kumwambia maneno ya upendo kama vile; oooo mpenzi wangu….nakupenda sana…….leo umependeza sana….. Kweli mimi nimechagua mke mzuri au mume mzuri sana……kwani najivunia sana kukuona na kuwa na wewe muda wote.

Wakati mwingine unaweza kwenda kumsaidia kupika, kuosha vyombo na hata kumwambia mkaoge pamoja. Utaona jinsi anavyoanza kubadilika mpenzi wako. Hapa hakuna mchawi bali ni namna tabia yako ulivyomwonyesha. Hali hii haiwezi kwisha ghafla kama kimbunga bali huenda taratibu na mwisho wa siki hali hujirudia. Kwa hali ya kawaida huchukua siku 14-22. Uendelea kumwambia maneno yenye baraka na busara bila ya kukata tamaa. Uwe na imanii ya hali ya juu kwani majibu utayokutana nayo si ya kawaida, lakini mwisho wa siku hali itarudi kuwa ya kawaida kabisa.

 

                                   3. HASIRA ZA MARA KWA MARA.

Hatua hii mpenzi wako huanza kuchukia kila jambo utendalo. Utende jema yeye kwake ni baya. Utajiongelesha ni kama unamuongezea hasira. Hapa ndipo watu huchukua hatua ya kujiua wenyewe kisa mpenzi wake amesaliti. Mfano wa majibu utayokutana nayo ni kama haya:-
  1. Mbona hivi mpenzi?
  2. Mimi nifanyaje?
Wewe yanakuhusu nini?
Umepata hasara gani mimi kufanya hivi?
Fanya utakavyo?
Mimi ndio kila kitu?
  1. Kwa nini yamefikia hapo?
  2. We ujui?
Hizi ni baadhi ya changamoto utazokutana nazo wakati wa maojiano yako na mpenzi wako. Usimpige kisa majibu ya mkato. Kama mwanaume hali ikizidi kuwa ni kelele tu, basi kaa kimya au ondoka na kwenda kufanya shughuli zingine. Utavyorudi atashindwa anzie wapi.

Kama ni upande wa mwanamke yanamtokea haya basi fanya hivi:- kaa kimya kwa muda, atakaa kimya mpenzi wako. Kasha usisite kumwandalia mumeo chakula cha kutosha na kizuri. Hata kama ali usichoke kuandaa. Mpe maneno matamu mkiwa kitandani na kujaribu kumgusagusa sehemu mbalimbali za mwili. Hapa mwanaume ujanja unaisha hapo.

Kama hizo njia zinachukuwa muda mrefu basi anza kwa kumuomba msamaha. Hata kumpigia magoti usione aibu. Piga huku ukionyeshwa kuwa hali hile upendezwi nayo. Ni ya bahati mbaya. Hakirudi katika hali ya kawaida na siku nyingi kupita anza kushusha makombola kwa njia ya utani kuwa pale mume wangu kosa lilikuwa lako. Kama muelewa ataweza kijirekebisha ipasavyo na mwisho wa siku penzi litarudi kama siku ya kwanza ya penzi lenu.

 

4. MANENO YASIYOFAA HUANZA KUZUNGUMZWA

Hii ni hatua ya nne ambayo inahitaji uvumilivu wa hali ya juu. Mpenzi wako huonekana mchungu kupita kiasi. Utaona kama kuna watu wanamfundisha kuongea maneno haya. Ukweli ni kwamba ukishaona mke wako, mara nyingi yeye na wenzake (rafiki wa makundi), hana muda wa kukaa akuandalie chakula au kuzungumza naye masuala ya kifamilia au uhusiono (kwa mwanamke aliye kwenye ndoa) basi tambua kwamba rafiki zake wamemfundisha na ujue kuna jambo linaendelea ambolo mwisho wake ni kutengana.

Kwa mchumba basi utaona maneno ya ovyo ovyo ili mradi umwambie sasa mimi na wewe basi. Atafanya kila namna awezavyo mutengane. Hii huweza kuwa mwanaume ndio kisa au mke mwenyewe ndio kisa. Akishindwa hapa anaamua kuchukuwa maamuzi magumu sana ambayo hutasahau tena maishani. Kama vile kumpigia mpenzi wake mpya na kuanza kuongea naye bele yako.

Hivyo yawezekana atakuwa amekuheshimu, anamkumbatia na kumkiss ili mradi uhuzunike kwa hili kasha mtengene ili awe huru. Hali hii huwa ni mbaya zaidi kama mtu umepemnda. Hivi ni sawa na wanavyofanya wanaume walio wengi katika uchumba na ndoa. Ukimuuliza namba hii uliyosevu Juma mbona inaonyesha ni ile ya Asha atakuambia ni rafiki yangu.

Ukiendelea kumbana atakuambia ni ya mke wangu. Sasa wewe unasemaje au unataka nini? Haya utokea kwa wote walio kwenye ndoa na wale walio hatua ya uchumba bila kujali mume au mke au mchumba.Haya ndiyo yanayojili sehemu hii iwapo utashindwa kutatua hizo hatua tatu za mwanzo.

Namna ya kutatua sehemu hii ni kutumia zile njia elekezi ya hatua ya kwanza. Kubwa zaidi hapa ni kuomba msamaha kwa kile kinachovumilika, na kile ambacho akivumiliki ni kwenda kwa washauri nasaha kama vile maafisa ustawi wa jamii kwa manufaa ya wote. Wao watakusaidia vizuri hata kama uko peke yako na mwenza wako anakataa kwenda huko. Utamsahau na kuiona dunia ni tamu zaidi ya sana na utasema mwenyewe ulichelewa wapi kipindi yanatokea haya.

 

                           5. KUDAI KUTENGANA

Kama mnavyojua, mti uota, ukua, utengeneza majani yenye mvuto pamoja na maua, huishi na hatimae mwisho kufa. Katika hatua hii mpenzi wako utaona ni kero kwako, yaani hakufai hata kidogo. Kama una imani ndogo utatamani uondoke uende mbali ambako hutamwona tena. Hapa hakuna jinsi, hata mahakama huamua kutenganisha ndoa kama walioana. Hapa usipofanya kama atakavyo mpenzi wako unaweza kuishia hata gerezani au kuchukua uamuzi wa kumpiga.

Kweli inauma sana kumwona mke/mume au mchumba unayempenda anataka mutengane. Wengine huamua kujinyonga, wengine kunywa sumu, wengine wanaamia baa na kuweka makazi yao. Mmoja hakikataa hakuna jinsi, mwache aende kwa usalama.

Jinsi ya kutatua hili ni kwamba unapaswa kukubaliana na tatizo lililotokea. Kwani kinachotokea kwa wenzako hata wewe ipo siku yatatokea kwako. Katika maisha ya binadamu kuna kupenda na kutendwa, hivyo kutengana ni moja ya sehemu ya maisha. Jaribu kutembelea sehemu zenye mkusanyiko wa watu. Lakini usinywe pombe, na kama ulikuwa unakunya unaweza kuacha kabisa angalau kwa miezi kadha na usitembelee sehemu za pombe.

Unaweza kwenda disco na sehemu nyinginezo mzuri kama vile kwenye mpira, kucheza puru, drafti, bao na hata karata. Hali yako itarudi kama zamani. Utajiona wa kawaida (hii ni kama kwa mwanaume). Ukikutana naye usimwone kama ni adui ako mkubwa, kwani yaliyotokea ni majaribu ya dunia. Na pale mkaapo kwa muda mrefu na kuona kuna umuhimu wa kurudiana basi murudiane kwa moya mmoja.

Kwa wanawake huchukua muda mrefu kama tendo lilifanywa na mume wake. Na tatizo lenyewe kama vile kumfumania mume au mchumba wake wakiwa katika chumba kile kile anacholala yeye na mwanamke mwingine. Kwa mwanamke huona ni unyama. Kwa hili, mke huyu kurudiana naye itachukua muda mwingi kwani lile swala humrudia mara kwa mara akilini mwake. Na kama alimpenda sana bwana wake huamua asikuone kamwe.

Lakini hakuna jambo lisilo na mwisho. Mume unapaswa kwenda kuomba msamaha kwa yule mke wako uliyemwacha. Kukataliwa kwa mara ya kwanza ni jambo la kawaida, kwani lile jambo litaendelea kumrudia. Jifanye kama usikii, fanya hivi zaidi ya mara tano hadi kumi. Mke wako au mume wako ataanza kukuonea huruma na hatimae kuwa nawe pamoja.
NB: ieleweke kwamba si kila unayemfanyia tukio baya ataweza kukusamehe. Ni wachache wenye nyoyo kama hizo. Bora ubadilike na kutunza utu na uthamani wako mapema. Kwa kufanya hili maisha utayaona kama maji ya kunywa.

 

NANI HUANZA KUMWACHA MWENZAKE KATI YA MKE AU MUME


Kuhusu nani anayepaswa kumwacha mwezake lipo katika sehemu mbili ambazo ni:-

A/ kwa wanandoa
Katika zama hizi za utandawazi anayepaswa kumwacha mwenzake ni yeyote kati ya mke au mume chini ya ushahidi na usimamizi wa mahakama. Kila mmoja anayo haki hiyo. Kinachofanyika ni kwamba mhusika apitie hatua zote za kuachana au kuvunja ndoa yao.

B/ kwa wachumba
Hapa ndipo linapoanzia tatizo. Kila mmoja hutaka aanze mwenzake ili apate ya kusema. Mwanamke anafanya vituko ili mchumba wake aseme basi kuanzia leo mimi si mchumba wako. Na mwanaume naye husubili kutoka kwa kwanamke aseme mimi basi. Hapa ni usanii tupu kwa sababu hakuna anayezifahamu ndoa hizi zaidi ya marafiki. Na ikifikiwa kujua wazazi basi ujue muda umekwenda sana.

Nilichogundua ni kwamba, hawa wachumba utengana tu pale anapopata mchumba mwingine anayeridhika naye. Kuna baadhi wanakuwa na wachumba kwa ajili ya kupeleka siku ili ziende “part time cohabitation”. Na mwingine anakuwa amejitoa mhanga katika hili. Kwa mchumba asiyehitaji kuwa na wewe dalili ni zile zile na ndio hatua zenyewe za kuvunjika kwa uhusiano.

Hapa kuna ndoa za siku moja yaani usiku wanapatana asubihi kila mtu kivyake. Mtu huyu mbinu anayoingia nayo ni ya kumwonea huruma sana, lakini saa chache tu baadaye hali ni mbaya. Kila ukimgusa mchungu kama pilipili.

Kuna ule uchumba wa muda mrefu “permanent cohabitation”. Ambao watu hukaa zaidi ya miezi mitatu. Hapa wapendanao huachana kwa ugomvi au kupata kwa mke au mume mwingine ambaye anaonekana anamfaa. Kipindi kingine mmoja kati ya wapendanao huweza kumwacha mweza wake kutokana na kushindwa kufikia muhafaka juu ya jambo fulani.


HALI BAADA YA KUTENGANA

Kwa walio wengi hapa hali hubadilika na kuwa tofauti na mwanzo. Lakini ukweli ni kwamba hutokea hali za aina kuu mbili ambazo ni hali ya maelewano na hali ya kutoelewana au uhasama.

A/ Hali ya kutoelewana
Hapa kama wapenzi hawakubahatika kuwa na mtoto basi kila mtu huanza kumchukia mwenzake na kufikia hatua ile hata kutosalimiana. Ieleweke kuwa hii ni kwa baadhi ya watu tu. Na kama mlikuwa na watoto basi mawasiliano hukata kwa muda mfupi na baada ya kupita siku kadhaa huanza kuwasiliana kama mwanzo ijapokuwa kila mmoja hapendi iwe hivyo. Hii hutokea kwa sababu kila binadamu ana kichaa. Na kichaa uweza kuondoka na hali ikarudi kama ya zamani.

Kipindi hiki mwenza wako yupo tayari hata kukuondoa duniani, na kwa kuwa sheria humbana, hutamani kwenda mbali sana ili mradi asikuone au msionane. Maisha huendelea, na kama hatatokea mtu ambaye anaweza kumweka sawa (counceling) busi hutokea ile hali ya chuki juu ya jinsia fulani.

Kama alikuwa ni wa ofisini basi utaona mambo yanageuka na kuanza kuwa mkali kwa ile jinsia tofauti. Hapa kama ni mwajili mkuu basi anauwezo hata wa kukukaripia kama mtoto au kukufukuza kazi kabisa ndani ya masaa 24.

Ushauri wangu ni kwamba, ukiona hali hii imeanza kutokea kwa mfanyakazi mwenzako au mwajiliwa mwenzako, au yule mpenzi uliyemwacha na hata ndugu yako, naomba uwe naye karibu sana hata kama maneno unayopewa ni ya kukatisha tamaa. Endelea kumsaidia kazi ndogo ndogo, kufanya mazoezi ya viongo, kutembelea maeneo mbaalimbali na kumshauri mutembelee zile ofisi za ushauri nasaha kwa ajili ya kuweza kumrudisha hali yake kuwa ya kawaida kama mwanzo kabla ya kupatwa tatizo la kutengwa.

Inachukuwa muda mrefu sana kukubaliana na wewe kuwa mpenzi wako au rafiki yako mpendwa au hata ndugu yako kukuelewa kuwa ana tatizo. Hapa hujikuta kila jambo analofanya na kuamua liko sahihi. Usikate tamaa juu ya majibu unayopewa. Yatumie majibu hayo kama changamoto kwako. Mtu ambaye huweza kumsikiliza mtu wa namna hii ni yule tu aliye karibu naye tu.

Hali hiyo huweza kutoweka mapema kutegemea na wale walionae karibu wanavyomshauri mlengwa. Ikumbukwe kwamba si kila rafiki ana maneno ya busara kwako. Huyo rafiki yako ndiye mbaya wako wa kesho. Leo anakupenda na kesho anakugeuka. Na si kila rafiki ni mbaya kwako. Unatakiwa kuangalia rafiki yupi ni bora zaidi na anayekufaa ili akusaidie wakati wa shida badala ya kukuangamiza.

B/ Hali ya maelewano
Hapa wapendanao huendelea kuwasiliana vizuri kama kipindi cha penzi lao. Hali inakuwa tofauti kidogo lakini mawasiliano ni mazuri. Hii hutokea pale mke au mume au mchumba wameachana kwa njia ya amani.

ATHARI ZA KUPENDA KUPITA KIASI
Ni vyema kujua mpenzi wako anakupenda kiasi gani. Na kila mtu ni siri yake mwenyewe kujua anampenda mwenzi wake kwa kiasi gani. Kumpenda mke au mume au mchumba wako ni jambo jema sana. Muonyeshe namna upendavyo kwa maneno, pamoja na tabia yako.

Kuna jambo moja ambalo mtu yeyote apendezwi nalo kuona mume, mke au mchumba akilitenda ambalo ni kuonyesha dharau ikiwemo kuona maneno anayozungumza hayana mantiki yeyote “prejudice”. Akigundua mwezi wako ujue kuwa hali ya penzi lenu linaelekea kubaya. Si vizuri kuendekeza hali hii kama umezaliwa nayo au kurithi kutoka kwa wazazi. Inapaswa ujizuie.

Hakuna mapenzi ya kweli kama hakuna upendo. Katika maisha ya sasa ni muhimu sana kuonyesha namna unavyompenda mke/mume wako. Watu hupenda sana kiasi kwamba hata kufikiri suala lingine inakuwa ngumu hasa suala la kimaendeleo, badala yake huitaji kukaa na mweza wake muda wote na kumfuata kila aendako. Na wengine ufikia mahali hadi anaharibu kazi. Kila kazi hufanya ili mradi aonekane amefanya kazi.

Kwa kawaida imezoeleka kuona mke au mwanamke ndiyo anayependa sana kuliko mume wake. Kiukweli ni kwamba wote wana haki ya kuonyesha kila aina ya upendo alionao kwa mweza wake.

Zifuatazo ni athari za kupenda kupita kiasi kwa wapenzi:-
-Kushindwa kutekeleza majukumu ya kila siku ikiwemo ya kiofisi kwa wafanyakazi.
-Siku ya kutendwa ikiwadia basi kwa aliyetendwa ni rahisi kupata mshtuko wa moyo (stress) au kujiua.
-Kutosalimiana kwa muda mrefu.
-Kushindwa kusaidiana kwa namna moja au nyingine hasa yale yaliyo nje ya mpaka.


Nadhani umejifunza mengi sana katika kitabu hiki. Ni jukumu lako kubadilika na kuwa katika mstari mnyoofu. Mpende mke/mume au mchumba wako lakini usipitilize kiwango kiasi kwamba unapoteza welekeo wa maisha yako. Utaumia na kushindwa kufanya maamuzi yako kwa wakati husika.



Maoni yenu ni muhimu sana kwangu. Unaweza kutuma kwa anuani zifuatazo:-.

MAWASILIANO


facebook account- AUSI CHIWAMBO
twitter account- ACHIWAMBO
Arasachi the center of Learning, on facebook
Phone No. 0753 110740
                  0652 403792





Kazi hii imeandaliwa na




CHIWAMBO, A. R. (2011/2012) 

BA SOCIOLOGY AND SOCIAL WORK

TEOFILO KISANJI UNIVERSITY (TEKU).




















No comments: