Saturday, September 21, 2013

Watu 20 wauwawa katika uvamizi wa jengo la maduka Nairobi


Watu wenye silaha wavamia jengo la maduka mji mkuu wa Kenya Nairobi (21.09.2013) na kuuwa takriban watu 20 na kujeruhi wengine zaidi ya 50 kwa kile serikali inachosema linaweza kuwa shambulio la kigaidi.

Wafanya manunuzi walikimbia jengo la Westgate. (21.09.2013).
Watu wengine wengi walikimbilia barabarani, madukani na sinema kusalimisha maisha yao.Kundi la wanamgambo wa Somalia la Al Shabaab lilikuwa limetishia kushambulia jengo hilo la maduka la Westgate ambalo ni mashuhuri kwa jumuiya ya wataalamu wa kigeni mjini humo.Lakini hakuna kundi lililodai mara moja kuhusika na shambulio hilo na Al Shabaab imekataa kuzungumzia shambulio hilo.

Helikopta za polisi zilikuwa zikizunguka juu ya anga ya eneo la jengo hilo wakati polisi wakisikika wakipiga makelele wakitaka watu watoke nje ya jengo hilo na huku watu wengi waliokuwa wakifanya manunuzi wakilikimbia jengo hilo.Moshi ulikuwa ukifuka kwenye mlango wa jengo hilo na watu walioshuhudia tukio hilo wamesema walisikia miripuko ya maguruneti.

Wengine wamesema wamewaona watu watano wenye silaha wakilivamia jengo hilo la maduka la Westgate na kwamba linaonekana kuwa ni shambulio na sio wizi wa kutumia silaha.

Milio ya risasi ilikuwa ikisikika kutoka hapa na pale ikiwa ni saa mbili baada ya mashambulio ya risasi kuanza wakati polisi ikilipekuwa jengo hilo wakiwasaka washambuliaji kutoka duka moja hadi jengine.

Watu wanashikiliwa mateka
Baadhi ya vituo vya televisheni nchini humo vimeripoti kwamba kulikuwa na watu waliokuwa wameshikiliwa mateka lakini hakuna uthibitisho rasmi kutoka serikalini.
Yukeh Mannaseh ambaye alikuwa ghorofa ya juu ya jengo hilo wakati mashambulizi hayo ya risasi yalipoanza amekaririwa akisema "Hawaonekani kama majambazi,hilo sio tukio la wizi". Ameendelea kusema kwamba "Inaonekana kama ni shambulio.Walinzi waliowaona wamesema walikuwa wakifyatuwa risasi ovyo."

Shahidi mwengine aliyejitambulisha kwa jina la Taha amesema amesikia milio ya breki za gari iliofuatiwa muda mfupi baadae na mripuko na milio ya risasi katika ghorofa ya chini ya jengo hilo.Mtu mwengine aliyenusurika katika shambulio hilo amesema amepigwa risasi na mtu mwenye sura ya Kisomali.

Baadhi ya watu waliokuwa wakifanya manunuzi kwenye jengo hilo walikimbilia ngazini na kwenye lifti na kujicha kwenye ukumbi wa sinema wa jengo hilo wakati wengine polisi iliwagunduwa wakiwa wamejificha chooni kwenye ghorofa ya kwanza ya jengo hilo.

Takriban watu 24 waliojeruhiwa walitolewa nje kwa machela na vigari vya kufanyia manunuzi.Wengi wa wahanga walikuwa na majeraha mengi madogo madogo waliyoyapata kutokana na vitu vilivyorushwa kutokana na mripuko.Wengine walitoka nje wakitembea wenyewe kwa miguu huko nguo zao zilizorowa damu zikifunika majeraha yao.

Shirika la Msalaba Mwekundu la Kenya limeliambia shirika la habari la Uingereza Reuters kwamba takriban watu 15 wameuwawa na kuna uwezekano wengine waliouwawa bado wangaliko ndani ya jengo hilo.Katibu Mkuu wa Chama cha Msalaba Mwekundu nchini Kenya Abbas Gullet amesema idadi ya maafa na majeruhi ni kubwa na ile waliyokuwa nayo ni ya wale walioko nje. Gullet alitowa kauli wakati milio ya risasi ilipokuwa ikiendelea kurindima ndani ya jengo hilo.

Kuna maafa ndani ya jengo
Kenya imekuwa ikilaumu kundi la al Shabaab na wafuasi wao kwa mashambulio kadhaa ya risasi, mabomu na maguruneti dhidi ya makanisa na vikosi vya usalama tokea jeshi la Kenya lilipoingia Somalia kusaidia kupambana na wanamgambo wenye mafungamano na kundi la Al Qaeda miaka miwili iliopita.

Al Shabaab huko nyuma ilitishia kushambulia majengo ya ghorofa refu mjini Nairobi na maeneo ya starehe na burudani vikiwemo vilabu vya usiku kucha na mahoteli ambayo hupendelewa na watu wa mataifa ya magharibi walioko katika mji mkuu huo. Lakini hadi sasa wameshindwa kufanya mashambulizi ya aina hiyo.

Mwanajeshi mmoja wa zamani wa Uingereza aliyekuweko katika eneo hilo amesema yeye mwenyewe binafsi aliyapapasa macho ya watu wanne na walikuwa tayari wamekufa akiwemo mtoto mmoja.

Amesema kuna mauaji makubwa kwenye jengo hilo.
Mwanamgambo mmoja wa jeshi la serikali alipoulizwa iwapo hilo lilikuwa ni tukio la wizi amejibu "Hapana huo ni ugaidi".Hata hivyo hakuna taarifa rasmi kutoka kwa polisi kuhusiana na dhamira ya washambuliaji hao.

Polisi imelizingira jengo na barabara zilioko karibu na jengo hilo lilioko kwenye kitongoji cha Westlands katikati ya mji wa Nairobi.Wizara ya mambo ya ndani imesema huenda hilo ni tukio la kigaidi na tayari jeshi la Kenya limefika katika eneo la mkasa kushirikiana na polisi kudhibiti hali hiyo.

Mwandishi : Mohamed Dahman/Reuters
Mhariri:Caro Robi
Chanzo: DW/De/Kiswahil

Mbowe, Mbatia, Profesa Lipumba wamvaa IGP


Mkuu wa Jeshi la Polisi, Inspekta Jenerali Said Mwema (kulia) akiagana na Wenyeviti wa Vyama vya Siasa, Profesa Ibrahim Lipumba wa CUF (kushoto)Freeman Mbowe wa Chadema (wapili kulia) na James Mbatia wa NCCR-Mageuzi, jijini Dar es Salaam jana. Picha Fidelis Felix

Dar es Salaam. Vyama vya siasa vya upinzani vya Chadema, CUF na NCCR-Mageuzi, leo vitafanya mkutano wa hadhara katika Viwanja vya Jangwani kuhamasisha wananchi wapinge kile wanachodai ni hujuma dhidi ya Mchakato wa Katiba Mpya.

Hatua ya kufanya mkutano huo, ilifikiwa jana baada ya wenyeviti wa vyama hivyo kumvamia Mkuu wa Jeshi la Polisi nchini (IGP), Said Mwema ofisini kwake wakipinga kitendo cha Kamanda wa Polisi Mkoa wa Dar es Salaam kupiga marufuku maandamano waliyokuwa wayafanye leo jijini humo.

Katika mkutano wao na IGP Mwema, viongozi hao walikubaliana maandamano hayo yasitishwe kwa sababu za kiusalama, lakini wafanye mkutano huo wa hadhara.
Wenyeviti hao wa vyama vya Upinzani, James Mbatia wa NCCR-Mageuzi, Freeman Mbowe (Chadema) na Profesa Ibrahim Lipumba (CUF), ambao walikutana na Mwema jana mchana.

Hatua ya viongozi hao ilitokana na tamko lililotolewa juzi na Kamanda wa Polisi wa Kanda Maalumu Dar es Salaam, Suleiman Kova kusitisha maandamano ya vyama hivyo yasifanyike.

Kova alitaja sababu za uamuzi huo kuwa ni kuhofia yatasababisha kusitishwa kwa shughuli za kiuchumi pamoja na kuwepo taarifa za kiintelijensia kwamba yatakuwa na vurugu.

Tamko hilo liliwakera viongozi wa vyama hivyo vitatu vilivyotangaza kushirikiana katika kupinga kile wanachodai ni uporaji wa haki ya wananchi kutunga Katiba yao.
Mazungumzo wenyeviti hao na IGP yalianza saa 6 mchana na kumalizika saa 11 jioni, ambapo walitoa taarifa ya pamoja kuhusu waliyokubaliana.

Akitangulia kutoa taarifa hiyo, kwa niaba ya wenzake, Mwenyekiti wa CUF, Profesa Lipumba alisema: “Tumekubaliana kesho tutafanya mkutano Viwanja vya Jangwani. Tumekubaliana kusitisha maandamano hadi Oktoba 5, (mwaka huu).”
Aliongeza kuwa wamekubaliana pia kwamba watafanya mkutano mwingine wa hadhara Visiwani Zanzibar, Jumatano ijayo.

Hata hivyo, katika taarifa ya pamoja, ulitokea kuhitilafiana kwa kauli, pale IGP Mwema alipokuwa akitoa ya upande wake.
Hali hiyo ilitokana na kauli ya Profesa Lipumba kusisitiza kuwa mikutano na maandamano ni haki ya msingi kwa vyama vya siasa na kwamba wanachopaswa ni kutoa taarifa kwa polisi na wala siyo kuomba kibali.

Awali, wakati Mwema akihitimisha taarifa hiyo ya pamoja alisema kuwa wanasiasa hao wanapaswa kuomba kibali cha maandamano hayo ya Oktoba 5.
Alisisitiza kuwa kazi ya polisi ni kuhakikisha usalama wa raia na mali zao, hivyo wanasiasa hao wanapaswa kuomba kibali na baada ya polisi kuchunguza watakuwa na mamlaka ya kuridhia au kukataa ombi lao.

Mwema alisema haoni haja ya kuwepo malumbano na wanasiasa hao katika suala hilo kwa sababu lengo lao ni moja nalo ni kudumisha ustawi wa jamii.
“Wote tunajenga nyumba moja, sioni sababu ya kugombania fito,” alisema Mwema.

Mzozo wa Katiba
Mzozo wa vyama vya siasa vya upinzani ulianzia kwenye Mkutano wa 12 wa Bunge uliomalizika hivi karibuni mjini Dodoma, lakini sasa umehamia nje ya Bunge na vyama hivyo vimetangaza azma ya kuanza kampeni ya kuuhamasisha umma kudai maridhiano kabla ya kuendelea na mchakato wa Katiba Mpya.

Viongozi hao wa upinzani wanadai kwamba wabunge wa CCM waliongeza baadhi ya mambo kupitia majedwali ya marekebisho.
Wanadai kuwa hali hiyo inatoa mwanya kwa Serikali inayoongozwa na CCM kupitia kwa rais kuwa na mamlaka zaidi ya uteuzi wa wajumbe husika.

Vyama hivyo viliazimia kuanza rasmi leo harakati za kuhamasisha umma kupitia maandamano na mikutano ya hadhara.
Ndoa hiyo ya wapinzani waliifunga, Septemba 15, kwa kuandika historia nyingine mpya kwenye tasnia ya siasa za Tanzania wakipinga Muswada wa Marekebisho ya Sheria ya Mabadiliko ya Katiba wa mwaka 2013.

Wanadai mapendekezo mengi yaliyomo katika Rasimu ya Katiba iliyotolewa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba, yalipendekezwa na vyama hivyo, hivyo havitakuwa tayari kuona maoni hayo pamoja na ya Watanzania wengi yakichakachuliwa.

Wanasema muungano wao ni mwanzo wa kuunganisha umma wa Watanzania kufanya uamuzi wa kunusuru utekaji madaraka na mamlaka ya nchi kutoka kwa wananchi.
Vyama hivyo vinadai kuwa vinaungwa mkono na makundi mbalimbali yakiwamo asasi za kiraia, taasisi za dini, vyama vingine vya siasa, wasomi na taasisi za elimu.

Makundi mengine ni pamoja na vyama vya wafanyakazi, jumuiya za wakulima, wafugaji, wavuvi, sekta binafsi, watu wenye ulemavu, jumuiya za wanawake, vijana na wastaafu.

Misimamo ya wenyeviti
Profesa Lipumba anasema wanachopigania ni kuurejesha mchakato wa Katiba Mpya mikononi mwa umma, anaongeza kuwa suala hilo kwa sasa limehodhiwa na CCM.
“Tunamshauri Rais Kikwete asisaini muswada huu, aurejeshe bungeni ufanyiwe marekebisho yenye kujenga kuaminiana na mwafaka wa kitaifa kwenye mchakato wa mabadiliko ya Katiba. Hatutakwenda kumwona, ila aurejeshe bungeni,” anasema Lipumba na kuongeza:

“Mchakato huu unahitaji uvumilivu, staha na hekima na usitawaliwe na nia mbaya, ubabe, mabavu, kejeli na dharau hasa kutoka kwa watawala. Misingi hii ikipuuzwa mchakato mzima unaweza kutumbukiza taifa letu katika mpasuko, migogoro na hata machafuko.”

Mbatia anasema historia ya nchi inaonyesha kuwa waasisi wa kutaka sauti, kauli na mawazo ya umma isikike katika kudai Katiba Mpya ni vyama vya upinzani.
“CCM ndio nini… Wanatakiwa kujua kuwa Tanzania kwanza vyama baadaye, vyama vya siasa vilivyokuwa vikitawala nchini Kenya, Zambia vimekufa, lakini nchi hizo bado zipo. CCM inaweza kufa, lakini Tanzania itaendelea kubakia” anasema na kuongeza;

“CCM wakisema wapinzani tunafanya vurugu wanakosea, hatuwezi kuangamiza wazo letu la kutaka Katiba Mpya, katika taifa hili Watanzania hawajawahi kuandika Katiba iliyotokana na mawazo yao.”

Mbowe anasema wameamua kuweka pembeni tofauti zao kwa ajili ya kudai Katiba Mpya ya Watanzania wote, kwamba hata wanahabari wanatakiwa kuweka pembeni itikadi za vyombo vyao vya habari vinavyomilikiwa na vyama vya siasa, kuwa wakweli katika kudai Katiba Mpya.

“Waandishi wa habari msiwe vipaza sauti vya watawala bila kutafakari kwa kina Tanzania ya miaka 100 ijayo itakuwaje, wanahabari mnaweza kutunyima Katiba Mpya au mkatunyima kama ikitumika vibaya,” anasema.

Anaongeza kuwa amani ya nchi inaweza kuvurugwa kama mchakato wa katiba utahodhiwa na chama kimoja cha siasa (CCM), “Ikiwa hivyo, sisi hatutakubali kuwa kondoo. Wanaohubiri amani watambue kuwa kuna misingi ya kuipata amani hiyo, amani inapatikana kunapokuwepo na haki.”

Huku akinukuu kitabu cha Mwalimu Julius Nyerere cha ‘Freedom and Unity’, anasema, “Ni rahisi mno kuliwasha taifa la watu ambao wamekwazika, taifa hili watu wamekwazika sana. Mchakato wa katiba unaweza kutibu majeraha makubwa ambayo yanalikabili taifa.”

Anasema fursa adimu ya kupata Katiba Mpya inapotezwa na bunge na CCM na anasisitiza kwamba wapinzani watatumia kila aina ya mbinu kuwaelewesha Watanzania kinachoendelea ili washiriki katika kuidai katiba iliyotokana na mawazo yao.

“Wapinzani hatutarudi nyuma na hatutakubali nchi kurejeshwa chini ya uongozi wa katiba ya sasa. Hilo wenzangu (wenyeviti wenzangu) naomba mnielewe, Chadema hatukubali na naomba na nyinyi msikubali, maana ndani ya CCM kuna kundi linataka kurudi katika katiba hii tunayoilalamikia,” alisema.

Anasema katika kitabu hicho, Mwalimu Nyerere alisema, ‘Kuna siku wananchi watachagua kifo kama viongozi hawatakuwa makini’, kwamba hoja ya kutaka Amani itaharibiwa na wale wenye dola, siyo vyama vya upinzani.
Chanzo: Mwananchi

KATUNI YA WIKI NA kipanya


Shahidi wa Mramba azua mvutano wa kisheria


 
Dar es Salaam. Shahidi wa Waziri wa Fedha wa zamani, Basil Mramba, Kamishna wa zamani wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Felician Busigara, jana alizua mvutano mkali kati ya mawakili wa mashtaka na wale wa utetezi.

Busigara ambaye ni shahidi wa pili wa Mramba, alipanda kizimbani katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, ili kumtetea Mramba katika kesi ya matumizi mabaya ya madaraka katika ofisi za umma na kuisababishia Serikali hasara.

Washtakiwa wengine katika kesi hiyo ni, Waziri wa zamani wa Nishati na Madini, Daniel Yona na Katibu Mkuu wa zamani wa Wizara ya Fedha, Gray Mgonja.
Wanakabiliwa na mashtaka ya kuisamehe kodi isivyo halali, Kampuni ya Ukaguzi wa Madini ya Alex Stewart (Assayers) ya Uingereza na kuisababishia Serikali hasara ya Sh11.7 bilioni.

Mvutano huo ulizuka baada ya upande wa mashtaka, kumpinga shahidi huyo, kutoa ushahidi wake kama mtaalamu wa masuala ya kodi, ukidai kuwa upande wa utetezi haukufuata taratibu za utoaji wa maoni kama mtaalamu.

Wakati akitoa ushahidi wake huku akiongozwa na Wakili Herbert Nyange, anayemtetea Mramba, Wakili wa Serikali Mkuu, Oswald Tibabyekomya, alikuwa akinyanyuka mara kwa mara na kuweka pingamizi shahidi huyo kutoa ushahidi kama mtaalamu.Mbali na Wakili Tibabyekomya kupinga, mahakama pia ilikuwa ikihoji sababu za shahidi huyo kutoa ushahidi kama mtaalamu.

Akiongozwa na Wakili Nyange, Busigara alidai kuwa sheria ya kodi ya mapato inamtaja mwenye mamlaka ya kusamehe kodi kuwa ni Waziri wa Fedha.

“Nyange kuna haja gani ya kumleta shahidi anayezungumzia sheria, sheria zipo katika vitabu, hata wakili unaweza kuzungumzia hizo sheria katika majumuisho yako, mashahidi wako wasituambie kuhusu sheria,” alihoji Jaji Rumanyika.

Shahidi aliendelea kutoa ushahidi kwa kusoma kipengele kimoja cha mkataba kati ya Alex Stewart na BoT, akidai kuwa mkataba huo ulionyesha kwamba atakayelipa kodi ni benki na kampuni itapata fedha yake baada ya kodi.
Jambo lililosababisha Jaji Rumanyika kuingilia tena kati.
Chanzo: Mwananchi

Shambulio la Nairobi lauwa watu kadha


Watu waliokuwa na silaha wamefyatua risasi mjini Nairobi, Kenya, kwenye eneo la maduka katika mtaa wa Westlands.
Walioshuhudia tukio hilo, wanasema kuwa maguruneti piya yalitumika.
Inaarifiwa watu watano wamekufa.

Mwandishi wetu mjini Nairobi anaeleza kuwa washambuliaji inaarifiwa walivaa vilemba kama vya al-Shabaab, lakini haikuthibitishwa kama wapiganaji hao wamehusika.
Polisi waliojihami kwa silaha wamezingira jengo la maduka liitwalo Westgate, katika mtaa wa Westlands, na kuna taarifa ya watu waliojeruhiwa wakitolewa hapo kwa machera.

Inaarifiwa kuwa watu wengi wamenasa ndani ya jengo.
Magari yaliyoegeshwa nje ya maduka yameharibika
Chanzo: Mjengwablog.com

MAGAZETINI LEO JUMAMOSI TAREHE 21-09-2013 NA Chiwambo's Blog






CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) kimemtaka Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Dk. Shukuru Kawambwa kujiuzulu



CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) kimemtaka Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Dk. Shukuru Kawambwa kujiuzulu kwa kushindwa kulipa madeni ya walimu nchini.


Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana pia ametoa muda wa miezi sita kwa Waziri huyo na Naibu wake Philip Mulogo kutekeleza hilo agizo hilo vinginevyo chama kitawatumia wabunge wake kuwatimua kwa nguvu.


Kwa mujibu wa taarifa za madeni zilizokusanywa na Chama cha Walimu Tanzania (CWT), hadi sasa walimu wanadai malimbikizo yao ya Sh bilioni 49 ambayo hajalipwa na Serikali.


Kinana alikuwa akihutubia mikutano ya hadhara jana katika wilaya za Bariadi na Busega.


Alisema CCM haiko tayari kuona walimu wakinyanyaswa wakati wana madai ya msingi.


Hivi sasa imejengeka tabia kwa baadhi ya mawaziri na watendaji wa wizara ya kuwadharau walimu na hata kuwanyanyasa huku wengine wakishusha utu na heshima ya walimu kwa kuwatukana, alisema.


Kinana ambaye yupo katika ziara ya mikoa ya Kanda ya Ziwa alisema kwa mawaziri kushindwa kutatua kero za walimu, imefika wakati wahusika waondoke wenyewe na wasipofanya hivyo chama kitawaagiza wabunge wake wawafukuze kwa nguvu.


“Ninatoa muda wa miezi sita kwa Waziri wa Elimu na wasaidizi wake wakiwamo watendaji kuhakikisha wanalipa madeni ya walimu haraka. Haiwezeni hii ni nchi ya watu wote wakiwamo walimu wadharauliwe na hata kunyanyaswa kwa maneno ya matusi


Hili hapana CCM haiko tayari kuona walimu kila siku wakipigwa danadana kutokana na uzembe wa watu waliokabidhiwa dhamana za kuongoza sekta ya elimu katika nchi yetu,” alisema.


MTANZANIA ilimtafuta Katibu Mkuu wa CWT, Ezekiah Oluoch ambaye alisema hadi sasa madeni ya walimu yamefikia Sh bilioni 49 ambayo ni malimbikizo ya mishahara na mapunjo.


Kila mara tunawaambia kuwa ni vema Serikali itafute Sh bilioni 100 katika fungu la dharura ili iweze kulipa madeni ya walimu na iachane nao lakini hawasikii,” alisema Oluoch.

Mbeya City Timu Inayong'aa waambiwa Karibu Dar es Salaam


 

UKIWA unapita Barabara ya Morogoro, labda unatoka Arusha, Morogoro, Iringa au Mbeya, ukishaumaliza Mkoa wa Pwani, utakutana na bango kubwa barabarani limeandikwa ‘Karibu Dar es Salaam’.

 Kama hiyo haitoshi utakutana na mabango mengine madogo madogo yakisomeka “Sasa umeingia Dar es Salaam’.
Baada ya Mbeya City kuwa vidume katika Mkoa wa Mbeya na hata kuikomalia Yanga, sasa si vibaya kama tukiikaribisha timu hiyo jijini Dar es Salaam kwa kusema “Karibu Dar es Salaam’.

Mbeya City wameingia Dar es Salaam kwa mara ya kwanza tangu waanze Ligi Kuu Bara.
Kila kona ya Dar es Salaam na Tanzania wanaizungumzia mechi yao dhidi ya Simba leo Jumamosi itakayopigwa Uwanja wa Taifa.

Licha ya kuwa imeshacheza mechi nne za awali, mashabiki wanaamini kuwa wikiendi hii ndiyo Mbeya City wanaanza ligi kwa kucheza mechi ya kwanza ngumu zaidi nje ya mkoa wake na ndani ya Dar es Salaam tena dhidi ya timu ngumu ya Simba.
Mbeya City ilishangaza wengi kwa kutoka sare ya bao 1-1 na mabingwa watetezi Yanga kwenye Uwanja wa Sokoine, wikiendi iliyopita mjini Mbeya kabla ya kulazimisha suluhu dhidi ya Mtibwa mjini Morogoro Jumatano wiki hii.

Mambo hayo yameongeza mvuto na hamasa kwa mashabiki kwenye mechi dhidi ya Simba, ambayo imebatizwa jina la ‘Karibu Dar es Salaam’.
Mbeya City iliingia Mkoa wa Pwani juzi Alhamisi na kupiga kambi ya muda kabla ya jana Ijumaa mashushushu wake kuanza kutua Dar es Salaam na baadaye wakafuatiwa na timu yenyewe.

Kocha Juma Mwambusi amesisitiza kuwa mchezo huo utakuwa mgumu lakini amewatengeneza kisaikolojia wachezaji wake kukabiliana na presha ndani na nje ya uwanja na wanaamini watapata matokeo mazuri.

Straika msomi na hatari wa Mbeya City aliyemfunga Ally Mustapha ‘Barthez’, Mwagane Yeya amepania kumtungua, kipa wa Simba, Abel Dhaira na kuandika historia katika Ligi Kuu Bara. Kiungo wa Mbeya City, Steven Mazanda amesema lazima wawafanye kitu mbaya Wekundu hao wa Msimbazi.

Mbali na tambo hizo za wachezaji, mashabiki wa Mbeya City kutoka Mbeya, wamesema watafurika kwa wingi Uwanja wa Taifa kuishangilia timu yao.
Yeya, ambaye ni mwalimu wa Shule ya Sekondari Iduda Uyole, aliliambia Mwanaspoti kuwa: “Mbeya City ni vijana wa kazi, kwetu matokeo ni jambo la mwisho. Lakini malengo yangu ni kuhakikisha napigana, kama niliweza kumfunga, Barthez hata Dhaira (Abel) atafungika tu.”

Straika wa Simba, Tambwe Amisi amesisitiza kuwa ameshazitambua klabu za Tanzania na sasa inamuwia rahisi kukabiliana na mabeki.
Mchezaji huyo amesisitiza kuwa haijui Mbeya City lakini anaamini hakuna timu ambayo haifungiki huku kocha wake msaidizi, Jamhuri Kihwelu ‘Julio’ akisema; “Simba imekamilika, vijana wako fiti sana na ni vipigo tu, hatuangalii jina la timu wala ushabiki sisi tunataka pointi tu.”

HOFU YA KIPIGO
Wachezaji wa Mbeya City wamekuwa na hofu kubwa huenda mashabiki wa Yanga wakawafanyizia kulipa kisasi cha basi lao kuvunjwa kioo wikiendi iliyopita katika Uwanja wa Sokoine mjini Mbeya.

Lakini hofu yao nyingine ni kucheza kwa mara ya kwanza kwenye Uwanja wa Taifa, ambao una uwezo wa kubeba mashabiki 60,000 tena na timu ambayo imeshinda mabao 6-0, Jumatano.

JEZI ZA MBEYA CITY
Kwa wauzaji wa jezi ni kwamba, jezi za Mbeya City ni dili kubwa jijini Mbeya na watu wanazishambulia kuliko za Simba na Yanga. Mbeya City klabu mpya, imejizolea wapenzi wengi wa soka na robo tatu ya watu wa Mbeya wanaishabikia klabu hiyo mpya ya Ligi Kuu Bara.

Mwanaspoti ilipita katika mitaa mbalimbali ya Jiji la Mbeya na kujionea uuzwaji wake. Mmiliki wa duka la vifaa la Mbaspo, Salum Haroun alisema: “Jezi za Mbeya City hapa ni dili kubwa. Hapa dukani kwangu zimeisha na watu wanaziulizia sana, ukileta tu hazikai.”

Naye mchuuzi wa barabarani, Jastine Kisongi alisema: “Asikwambie mtu, kwa sasa jezi za Mbeya City ndiyo zina dili hapa Mbeya, ukiwa nazo una uhakika wa kuuza tofauti na hizi za Simba na Yanga.”

MECHI ZA LEO JUMAMOSI
Mgambo vs Rhino
Prisons vs Mtibwa
Kagera vs Ashanti
Simba vs Mbeya City
Chanzo: Mwanaspoti

87 wauawa na Boko Haram Nigeria




Wapiganaji wa Boko Haram wamewaua watu 87 katika shambulio katika Jimbo la Borno nchini Nigeria.
Mashahidi wanasema kuwa wapiganaji hao waliteketeza nyumba kadhaa katika tukio hilo la kutisha mnamo Jumanne usiku.

Shambulio hili limetokea siku chache baada ya makabiliano makali kati ya jeshi na wapiganaji wa Boko Haram
Wanamgambo hao waliokuwa wamevelia magwanda ya jeshi, waliweka vizuizi barabarani nje ya mji wa Benisheik na kuwapiga risasi wale waliokuwa wanajaribu kutoroka.

Kwa mujibu wa taarifa za mashahidi , wapiganaji hao waliteketeza nyumba katika shambulizi hilo la Jumanne.

Kundi la Boko Haram, ambalo linapigania linachosema ni taifa la kiisilamu nchini Nigeria, limekuwa likifanya mashambulizi sawa na haya kuanzia mwaka 2009.
Jeshi linadai kuwa Agosti mwaka huu, kiongozi wa kundi hilo Abubakar Shekau na naibu wake Momodu Bama waliuawa , ingawa hakuna taarifa za kujitegemea kuthibitisha hilo.

Mawasiliano katika jimbo la Borno, yamekumbwa na hitilafu, tangu mwezi Mei, wakati hali ya hatari, ilipotangazwa katika jimbo hilo na majimbo mengine mawili.
Lakini mashambulizi yameongezeka sana hivi karibuni tangu jeshi kuanza kukabiliana na kundi hilo katika maeneo yaliyoathirika zaidi.

Friday, September 20, 2013

VINARA SIMBA KUWAKABILI MBEYA CITY VPL



Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) inaingia raundi yake ya tano kesho (Septemba 21 mwaka huu) kwa mechi huku vinara Simba wakiwakaribisha Mbeya City kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Uwanja wa Mkwakwani, Tanga utakuwa mwenyeji wa mechi kati ya Mgambo Shooting Stars na Rhino Rangers ya Tabora. Mtibwa Sugar itakuwa mgeni wa Tanzania Prisons katika pambano litakalochezwa Uwanja wa Kumbukumbu ya Sokoine jijini Mbeya.

Nayo Kagera Sugar itakuwa nyumbani kwenye uwanja wake wa Kaitaba mjini Bukoba kuvaana na Ashanti United ya Dar es Salaam katika mechi itakayochezeshwa na mwamuzi Jacob Adongo kutoka Mara.

Ligi hiyo itakamilisha mzunguko wa tano keshokutwa (Septemba 22 mwaka huu) kwa mechi tatu ambapo Azam na Yanga zitacheza Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam huku JKT Ruvu ikikwaruzana na Oljoro JKT kwenye Uwanja wa Azam Complex.

Ruvu Shooting inayokamata nafasi ya pili kwenye msimamo wa ligi itakuwa mgeni wa Coastal Union katika mechi itakayopigwa kwenye Uwanja wa Mkwakwani jijini Tanga.
Wakati huo huo, Ligi Daraja la Kwanza (FDL) inaendelea wikiendi hii kwa mechi kumi na moja. Kundi A kesho (Septemba 21 mwaka huu) kutakuwa na mechi kati ya Transit Camp na Green Warriors (Uwanja wa Karume, Dar es Salaam), Tessema na African Lyon (Uwanja wa Mabatini, Mlandizi).

Ndanda itacheza na Villa Squad kwenye Nangwanda Sijaona mjini Mtwara wakati keshokutwa (Septembe 22 mwaka huu) kutakuwa na mechi kati ya Polisi Dar es Salaam na Friends Rangers katika Uwanja wa Karume, Dar es Salaam.

Kundi B kesho (Septemba 21 mwaka huu) ni Mkamba Rangers dhidi ya Burkina Faso kwenye Uwanja wa CCM Mkamba, na Mlale JKT itakuwa mwenyeji wa Kurugenzi Mafinga kwenye Uwanja wa Majimaji mjini Songea. Keshokutwa (Septemba 22 mwaka huu) ni Majimaji na Kimondo katika Uwanja wa Majimaji.

Mechi za kundi C kesho (Septemba 21 mwaka huu) ni Pamba dhidi ya Polisi Dodoma (Uwanja wa CCM Kirumba, Mwanza), Stand United na Polisi Tabora (Uwanja wa Kambarage, Shinyanga) na Kanembwa JKT itacheza na Mwadui kwenye Uwanja wa Kawawa ulioko Ujiji. Keshokutwa (Septemba 22 mwaka huu) Polisi Mara na Toto Africans zitacheza Uwanja wa Kumbukumbu ya Karume mjini Musoma.
Boniface Wambura Mgoyo
Ofisa Habari
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF)

 

VINARA SIMBA KUWAKABILI MBEYA CITY VPL



Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) inaingia raundi yake ya tano kesho (Septemba 21 mwaka huu) kwa mechi huku vinara Simba wakiwakaribisha Mbeya City kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Uwanja wa Mkwakwani, Tanga utakuwa mwenyeji wa mechi kati ya Mgambo Shooting Stars na Rhino Rangers ya Tabora. Mtibwa Sugar itakuwa mgeni wa Tanzania Prisons katika pambano litakalochezwa Uwanja wa Kumbukumbu ya Sokoine jijini Mbeya.

Nayo Kagera Sugar itakuwa nyumbani kwenye uwanja wake wa Kaitaba mjini Bukoba kuvaana na Ashanti United ya Dar es Salaam katika mechi itakayochezeshwa na mwamuzi Jacob Adongo kutoka Mara.

Ligi hiyo itakamilisha mzunguko wa tano keshokutwa (Septemba 22 mwaka huu) kwa mechi tatu ambapo Azam na Yanga zitacheza Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam huku JKT Ruvu ikikwaruzana na Oljoro JKT kwenye Uwanja wa Azam Complex.

Ruvu Shooting inayokamata nafasi ya pili kwenye msimamo wa ligi itakuwa mgeni wa Coastal Union katika mechi itakayopigwa kwenye Uwanja wa Mkwakwani jijini Tanga.
Wakati huo huo, Ligi Daraja la Kwanza (FDL) inaendelea wikiendi hii kwa mechi kumi na moja. Kundi A kesho (Septemba 21 mwaka huu) kutakuwa na mechi kati ya Transit Camp na Green Warriors (Uwanja wa Karume, Dar es Salaam), Tessema na African Lyon (Uwanja wa Mabatini, Mlandizi).

Ndanda itacheza na Villa Squad kwenye Nangwanda Sijaona mjini Mtwara wakati keshokutwa (Septembe 22 mwaka huu) kutakuwa na mechi kati ya Polisi Dar es Salaam na Friends Rangers katika Uwanja wa Karume, Dar es Salaam.

Kundi B kesho (Septemba 21 mwaka huu) ni Mkamba Rangers dhidi ya Burkina Faso kwenye Uwanja wa CCM Mkamba, na Mlale JKT itakuwa mwenyeji wa Kurugenzi Mafinga kwenye Uwanja wa Majimaji mjini Songea. Keshokutwa (Septemba 22 mwaka huu) ni Majimaji na Kimondo katika Uwanja wa Majimaji.

Mechi za kundi C kesho (Septemba 21 mwaka huu) ni Pamba dhidi ya Polisi Dodoma (Uwanja wa CCM Kirumba, Mwanza), Stand United na Polisi Tabora (Uwanja wa Kambarage, Shinyanga) na Kanembwa JKT itacheza na Mwadui kwenye Uwanja wa Kawawa ulioko Ujiji. Keshokutwa (Septemba 22 mwaka huu) Polisi Mara na Toto Africans zitacheza Uwanja wa Kumbukumbu ya Karume mjini Musoma.
Boniface Wambura Mgoyo
Ofisa Habari
Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF)

 

Jaji Mutungi aiumbua CCM



HATIMAYE Msajili wa Vyama vya Siasa, Jaji Francis Mutungi ameanza kuonyesha makali, baada ya kukipa onyo kali Chama Cha Mapinduzi (CCM) na kukitaka kuacha mara moja kutumia viongozi wa kidiplomasia kwenye shughuli za kisiasa.

Hatua ya Jaji Mutungi, imekuja siku chache baada ya CCM kumtumia Balozi wa China, Dk. Lu Youping katika shughuli za kisiasa mkoani Shinyanga wiki iliyopita.
Taarifa iliyotolewa kwa vyombo vya habari mjini Dar es Salaam jana, ilisema suala la ushiriki wa raia wa kigeni ikijumuisha wanadiplomasia katika shughuli za kisiasa nchini, halikubaliki.

Alisema ofisi yake, inaunga mkono kwa dhati hatua iliyochukuliwa na Serikali kupitia Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, kukemea jambo hilo.

"Tamko la Serikali limezingatia sheria na wajibu wa wanadiplomasia, wakati wa uwepo wao hapa nchini, mimi nikiwa mlezi wa vyama vya siasa, ninakemea kitendo cha CCM kumshirikisha Balozi wa China katika shughuli za kisiasa," alisema Jaji Mutungi.

Alisema katika tukio hilo, CCM kuruhusu raia wa kigeni kutumia jukwaa lake ni dhahiri limezua hali ya taharuki kwa wananchi, japo sheria ya vyama vya siasa kwa upande wake iko kimya katika suala hilo.

"Naviasa vyama vya siasa kwa ujumla wake, kuzingatia na kufuata sheria na taratibu stahiki katika utekelezaji wa shughuli zao za kisiasa.

"Napenda kuujulisha umma kwamba, ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa kwa wakati huu ipo kwenye mchakato wa marekebisho ya sheria husika ya vyama vya siasa, ambayo imebainika kuwa na upungufu....lengo ni kukabiliana na changamoto zilizopo likiwemo suala hili," alisema Msajili, Jaji Mutungi katika taarifa yake aliongeza sasa hivi ofisi yake inaendelea kukusanya maoni ya wadau katika jitihada za kufanikisha marekebisho ya sheria hiyo.

Suala la CCM kumshirikisha Balozi wa China katika masuala ya kisiasa, lilizua mjadala mkubwa hali iliyosababisha CHADEMA kutoa tamko na kuandika barua ya malalamiko UN wakitaka aondolewe kwa kupoteza sifa za kuwa balozi, baada ya kuvunja mkataba wa Umoja wa Mataifa wa 1961 unaosimamia nchi na nchi.

CHADEMA waliandika barua nyingine kwenda Serikali ya China na Tanzania, wakitaka msimamo na hatua zitakazochukuliwa dhidi ya balozi huyo kuvunja mkataba huo ibara ya 41(1-3), kinachokataza balozi kujihusisha na siasa katika Taifa ambalo yuko.

Chadema imesema inalaani kitendo hicho na itachukua hatua kwenda Umoja wa Mataifa na pia kupata maelezo toka Serikali ya China kama imemtuma balozi huyo kujihusisha na mambo ya siasa za ndani za vyama au kuiwakilisha nchi.

Akijibu tuhuma hizo, Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM, Nape Nnauye alisema alichofanya balozi huyo ni kitendo cha kuungwa mkono, maana alikuwepo kwa nia ya kuangalia maeneo ya uwekezaji wa zao la Pamba katika Mkoa wa Shinyanga.

Alisema uwekezaji kutoka China, utasaidia kuondoa tatizo sugu la ajira, kupanda kwa bei ya zao la pamba ambacho kimekuwa kilio kikubwa cha wakulima pamoja na ujengwaji wa viwanda vya nguo na kuchuja mafuta.

Hivyo ni vema kumpongeza balozi huyo na kuunga juhudi za CCM za kuwatafuta wawekezaji wa nje, badala ya kusingizia uvunjaji wa Mkataba wa Vienna ili kupata umaarufu wa kisiasa:
chanzo mtanzania

MAGAZETINI LEO IJUMAA TAREHE 20-09-2013






HATIMAYE Tanzania imewekwa kando rasmi na nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC)



HATIMAYE Tanzania imewekwa kando rasmi na nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), katika kuunda Shirikisho la Kisiasa litakaloziongoza nchi hizo. (HM)

Tayari marais wa nchi hizo, Paul Kagame wa Rwanda, Yoweri Museveni wa Uganda, Uhuru Kenyatta wa Kenya na Pierre Nkurunzinza wa Burundi wamekwishafikia makubaliano ya kuanzisha mchakato wa kuandikwa kwa Rasimu ya Katiba ya Shirikisho la Kisiasa la nchi wanachama wa EAC, bila kuishirikisha Tanzania.

Waziri wa Serikali za Mitaa wa Rwanda, James Musoni, amekaririwa na vyombo vya habari vya nchi hiyo akieleza kuwa makubaliano ya kuanzishwa kwa mchakato wa kuandikwa kwa Rasimu ya Katiba ya Shirikisho la Afrika Mashariki, yalifikiwa Septemba 12 mwaka huu, mjini Kampala na marais wa Rwanda, Kenya na Uganda na hivi karibuni Rais wa Burundi ambaye alialikwa katika mkutano huo na kushindwa kuhudhuria, naye sasa amethibitisha ushirika wake katika shirikisho hilo jipya.

Gazeti la The Sunday Times la Rwanda, limemnukuu Waziri Musoni kuwa marais wa nchi hizo wamekubaliana kukamilisha rasimu hiyo ndani ya muda mfupi.

Musoni ambaye alikiri kushiriki katika mkutano wa marais hao ulioshirikisha pia maofisa waandamizi wa nchi hizo isipokuwa Tanzania, alisema uamuzi uliofikiwa katika mkutano huo ambao ni wa pili kufanyika, ni moja ya maagizo ya uamuzi uliofikiwa kwenye mkutano wa kwanza uliofanyika pia mjini Kampala.

"Tumekubaliana juu ya kanuni za kisheria na mpango mzima utakaotuongoza ili kupata Rasimu ya Katiba itakayoliongoza shirikisho hilo la kisiasa," alikaririwa Musoni.

Alieleza kuundwa kwa kikosi kazi maalumu kitakachojulikana kwa jina la High Level Task Force (HLTF), ambacho kitajumuisha wataalamu wa nyanja mbalimbali watakaoandika Rasimu hiyo kwa namna ile ile ya ulivyoandaliwa mpango wa Itifaki ya soko la pamoja la Jumuiya ya Afrika Mashariki.

Musoni alisema mawaziri wa nchi wanachama waliopangiwa kushughulikia shirikisho hilo, wanatarajiwa kuelezea mwelekeo wa mafanikio ya mpango huo katika mkutano mwingine uliopangwa kufanyika mwishoni mwa mwezi Oktoba huko Kigali Rwanda.

Kwa mara ya kwanza, marais Kagame, Museveni na Kenyatta walikutana kufikia makubaliano ya kuharakisha uundwaji wa shirikisho la kisiasa kwa nchi zao kwa kuondoa vikwazo vya kiuchumi na kuweka hati ya vitambulisho vya pamoja na ushirikiano wa kibiashara sambamba na kuzindua mradi wa ujenzi wa gati ya Bandari ya Mombasa.

Waziri Sitta ashangaa
Waziri wa Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Samuel Sitta, alipoulizwa kuhusu hatua ya nchi hizo kuanza kuitenga Tanzania kuelekea kwenye Shirikisho la Kisiasa, alisema Katiba ya Jumuiya ya Afrika Mashariki, ibara ya 7 (e) ya mkataba inaruhusu nchi wanachama kufanya jambo la haraka kama nchi nyingine zinachelewa kufanya hivyo.

Sitta alilieleza Jumatano kuwa, taratibu za Tanzania haziruhusu kibali cha utambulisho kutumika katika nchi zote wanachama, kwa sababu lazima raia wa nchi wanachama anapoingia Tanzania kufuata taratibu za uhamiaji.

Alisema licha ya hatua zinazochukuliwa na nchi wanachama wa EAC za kuitenga Tanzania katika baadhi ya mambo, itabakia na msimamo wake na haitakubaliana kuingia kwenye Shirikisho la Kisiasa huku masuala ya ushuru wa forodha, soko la pamoja na sarafu moja, hayajatengamaa.

"Huo ndio msimamo wa Tanzania, hivi vitu vinne vilikuwa bado havijakamilika, matumizi yake hayajaenda sawasawa na makubaliano ya kila nchi sasa wanaharakisha Shirikisho la Kisiasa, waache waende kwa sababu Katiba inawaruhusu na wana ajenda zao za siri.

"Hatuoni suluhisho katika suala hilo, ni vigumu kuanza kusuluhisha matatizo ya jumuiya kwa sasa kama ilivyo vigumu kusuluhisha matatizo ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar.

"Ukitazama sasa tunapambana kuendeleza Muungano na Zanzibar, hili la nchi zote nne litakuwaje? Mali zinatoka nchi nyingine, vivyo hivyo kwa upande wa bidhaa, kwa maana hiyo hatuwezi kufika kwenye shirikisho kabla hatujamaliza vikwazo hivi vingine," alisema Sitta.

Tanzania yailima barua EAC
Waziri Sitta pia alieleza kuwa Tanzania imeiandikia barua sekretarieti ya baraza la mawaziri wa nchi wanachama wa jumuiya ya Afrika Mashariki, ikilalamikia baadhi ya mambo yanayoendeshwa kwa usiri na baadhi ya nchi katika jumuiya hiyo.

Alisema barua alikabidhiwa katika kikao cha baraza la mawaziri kilichofanyika Agosti 28 mwaka huu, mkoani Arusha, ikitaka wahusika kuweka wazi mambo yanayoendelea ndani ya jumuiya kwa kuzishirikisha nchi zote.

Aidha, Sitta alieleza kuwa wakati barua hiyo ikiwa imekwishawasilishwa kwa Sekretarieti, viongozi ambao wamekubaliana kuanza mchakato wa kuandika Rasimu ya Katiba ya Shirikisho la Kisiasa, wanapaswa kutambua kuwa Katiba itakayopatikana itakuwa batili kwa sababu haikuamuliwa na wananchi wa nchi husika bali watawala. Chanzo: Mtanzania