Saturday, August 31, 2013

Kingunge Anaangalia Miaka 50 Nyuma, JK Anaangalia Miaka 50 Mbele !



Ndugu zangu,
Ndugu Kingunge Ngombale Mwiru ni mmoja wa wanasiasa ninaowaheshimu sana. Nimemsikia Kingunge tangu nikiwa na miaka saba.
Lakini, kama ilivyokuwa kwa Mwalimu Nyerere, hakuwa malaika, Kingunge naye ni mwanadamu kama wengine. Si malaika.

Nimeyasikia mawazo ya Kingunge juu ya Serikali Tatu na hata Uraia wa Nchi Mbili. Ni mawazo yake, nayaheshimu, ingawa, kwa mtazamo wangu, Kingunge hayuko sahihi kwenye yote mawili.

Na hapa nitalizungumzia hili moja tu la mapendekezo ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba juu ya muundo wa Muungano wa Serikali Tatu.
Kimsingi haya ni mapendekezo yenye kutokana na maoni Wananchi. Hivyo, Tume imewasilisha tu. Si mapendekezo ya Jaji Warioba au wajumbe wake.

Hii ni tofauti kubwa na mazoea ya ' Ukale' ya Mzee Kingunge ambayo hata sasa anataka yafuatwe; kuwa jambo kubwa la muundo wa Muungano liachiwe Chama Cha Mapinduzi na vikao vyake.

Ni jambo jema kwa mwanadamu kujifunza kutokana na historia, lakini, si jambo jema kwa mwanadamu kuwa mtumwa wa historia. Ni bahati mbaya, kuwa Mzee wetu mpendwa, Kingunge Ngombare Mwiru, anataka tubaki kwenye utumwa wa historia. Hatutaki.

Na hakika Mzee Kingunge anapaswa kuelewa, kuwa nchi hii ni zaidi ya Chama cha Siasa. Na chama cha siasa kilicho madarakani hakiongozi mawe. Na hata kama kingekuwa kinaongoza tumbiri, bado kingekumbwa na changamoto ya uwepo wa tumbiri wenye kutaka mabadiliko, kulingana na mahitaji ya wakati.

Tukubali, kuwa yalifanyika makosa makubwa ya kiuongozi huko nyuma. Ni pale masuala makubwa ya kitaifa kuachwa maamuzi yake kufanywa na kundi dogo la watu kwa kutumia nyadhifa za uongozi wa chama. Kwenye masuala makubwa ya nchi Chama kiliamua juu ya vichwa vya watu bila kushirikisha mawazo ya wananchi wenyewe, iwe kwa kupitia kura za maoni au kukusanya tu maoni ya makundi wakilishi. Huo ni msingi wa manung'uniko mengi ya sasa.

Kwangu mimi, Jakaya Kikwete ni mwanamageuzi wa kweli ambaye, kama kiongozi, ameonyesha ujasiri mkubwa wa kuzipa mgongo fikra za ukale na kuiangalia zaidi nchi na mustakabali wake kwa miaka mingi ijayo. Anafanya hivyo bila kujali nani au chama gani kitakuwa madarakani.

Wakati Mzee Kingunge na wahafidhina ( wasiotaka mabadiliko) wengine ndani ya mfumo uliopo wanatoka mahandakini huku wakihaha kujaribu kuurudisha nyuma mshale wa mabadiliko chanya kwa jamii , Jakaya Kikwete anaonekana, kuwa sio tu amesimama imara katika kuhakikisha mshale wa saa ya mabadiliko chanya kwa nchi unakwenda mbele, bali, unakwenda mbele kwa kasi.

Ni imani yetu, Wananchi walio wengi, kuwa Jakaya Kikwete hatakatishwa tamaa wala kuyumbishwa katika kukamilisha ajenda yake njema ya mabadiliko chanya kwa jamii ya Watanzania kuelekea miaka 50 ijayo.

Mzee Kingunge aelewe pia, kuwa wakati umebadilika. Kuwa ya mwaka 1974 alipojiunga na TANU ni tofauti na ya sasa, mwaka 2013. Huu ni wakati wa kiongozi kuonyesha uwezo wa kusoma alama za nyakati. Hivyo, kujitahidi kuendana na mabadiliko ya nyakati.

Hiyo pia ndio tafsiri ya kuwa ' Kiongozi wa Kisasa na Kimaendeleo'- A modern and progressive leader. Jakaya Kikwete kwa sasa yumo kwenye kundi hilo.

Na wenzake ndani ya CCM wakimsaidia katika kazi yake, basi, ni fursa pia kwa Chama chao kuiteka tena mioyo ya Wananchi wengi, mijini na vijijini. Maana, kati ya ambayo yanawachosha wananchi ni kukosekana kwa mawazo ya usasa na ya kimaendeleo kutoka kwa miongoni mwa viongozi wa CCM. Ni moja ya sababu ya chama hicho kupungukiwa na mvuto hususan kwenye kundi kubwa la vijana.

Na hakika, hata kama hatuoni leo, historia itakuja kumkumbuka Jakaya Kikwete kama mmoja wa viongozi Wana-Mageuzi ndani ya Chama chake CCM, na nchi kwa ujumla.
Maggid.
Iringa.
MAKALA HII IMEANDIKWA NA MAGGID
Chanzo: mjengwablog.com

IGP aibiwa upanga wa dhahabu



Jeshi la Polisi limeingia katika kashfa nzito baada ya mkuu wake, Inspekta Jenerali Said Mwema, kuibiwa upanga wa dhahabu ambao ni mali ya Shirikisho la Wakuu wa Majeshi ya Polisi wa nchi za Kusini mwa Afrika (SARPCCO).

Upanga huo wenye uzito wa takriban kilo tatu na wenye thamani ya zaidi ya fedha za Tanzania Sh600 milioni, ni kielelezo kwa nchi inayokabidhiwa uongozi wa SARPCCO.
Mwaka jana Tanzania ilikuwa mwenyekiti wa SARPCCO, ambapo upanga huo ulikabidhiwa kwa IGP Mwema na Jenerali Magwashi Victoria ‘Riah’ Phiyega, ambaye ni Kamishna wa Taifa wa Polisi wa Afrika Kusini aliyekuwa amemaliza muda wake kwa wakati huo.

Hilo ni tukio la pili la wizi la mali zinazohusu ofisi ya IGP, ambapo mwaka jana ndani ya ofisi hiyo kuliibwa kompyuta ndogo (laptop), ikiwa na taarifa muhimu za kipolisi. Hadi sasa hakuna taarifa za kupatikana kwa kompyuta hiyo.
IGP Mwema alikabidhiwa upanga huo Septemba 5, 2012, katika mkutano saba wa SARPCCO uliofanyika Zanzibar na kuhudhuriwa na wakuu wa majeshi ya Polisi kutoka nchi 13, pamoja na mashirika ya kimataifa.

Upanga huo ambao unakwenda sambamba na bendera ya SARPCCO, ni moja ya vielelezo vya nchi iliyochaguliwa kuwa Mwenyekiti wa shirikisho hilo, ambaye moja kwa moja anakuwa ni Mkuu wa Jeshi la Polisi katika nchi husika.
Kwa mujibu wa taratibu za SARPCCO, vielelezo hivyo hutakiwa kuwekwa ofisini kwa kiongozi husika, ikiwa ni alama ya kila mgeni atakayeingia ofisini hapo kutambua uwepo wa wadhifa huo wa kimataifa.

Uchunguzi wa gazeti hili ulibaini kuwa IGP aligundua kutoweka kwa upanga huo wiki iliyopita, wakati akijiandaa kwenda kuukabidhi kwa mwenyekiti mpya wa SARPCCO, ambaye ni IGP wa Namibia.

Taarifa za ndani ya jeshi hilo zilibaini kuwa, IGP alilazimika kuondoka bila upanga huo alipokwenda Namibia wiki iliyopita kuhudhuria mkutano wa nane wa SARPCCO, uliofanyika Jumapili iliyopita mjini Windhoek.

Kwa mujibu wa uchunguzi, IGP Mwema alikabidhi upanga unaofanana na huo ambao siyo wa dhahabu, alioazimwa kutoka kwa Mkuu wa Jeshi la Polisi la Namibia, Inspekta Jenerali, Luteni Jenerali Sebastian Ndeitunga, na kukabidhiwa kama ishara ya kukabidhiwa uenyekiti wa SARPCCO kwa kipindi cha mwaka mmoja.
Uchunguzi ulibaini kuwa IGP Mwema alitoa ahadi ya kurejesha upanga halisi ndani ya kipindi cha mwezi mmoja, au Serikali ya Tanzania italazimika kutengeneza mwingine kulipa uliopotea.

Uchunguzi wa gazeti hili unaonyesha kuwa kashfa hiyo ametupiwa Mkuu wa Polisi Zanzibar, Kamishna Mussa Ali Mussa pamoja na dereva wake, ikidaiwa kuwa upanga huo baada ya kupokewa na IGP Mwema, Septemba mwaka jana uliwekwa kwenye gari la kamishna huyo.

Kamishna Mussa ndiye alikuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Maandalizi ya Mkutano wa Saba, na pia ofisa mwenyeji kwa wajumbe wa mkutano huo uliofanyika Zanzibar.
Hata hivyo, taarifa zingine zilidai kuwa IGP Mwema naye analaumiwa kwa kutofuatilia kwa karibu zana za kazi, kwani baada ya kuupokea alitakiwa kuhakikisha unakuwepo ofisini kwake kama alama ya uenyekiti wake.

Gazeti hili lilipowasiliana kwa njia ya simu na Mkuu wa Polisi Zanzibar, Kamishna Mussa Ali Mussa kuhusu madai hayo alisema, kitara (upanga) hicho ni kweli kimepotea, lakini yeye hahusiki kwa kuwa kila kitu kina utaratibu wake.

“Ni kweli kitara kilikabidhiwa kwa afande IGP na mimi nilishuhudia kikikabidhiwa, na ni kweli kitara hakijulikani kiliko, lakini mimi sihusiki na kupotea kwake. Ni kweli mimi nilikuwa ofisa mwenyeji wa mkutano huo, lakini siku hiyo zilitolewa zawadi nyingi, watu walipewa mikoba, kwa hiyo mtu akipoteza mkoba wake niulizwe mimi?” alihoji Kamishna Mussa.
Alisema kila kitu kina utaratibu wake na kwamba taarifa kwamba yeye amehojiwa kutokana na upotevu wa kitara hicho au kuna kamati imeundwa, hazina ukweli.
“Sijawahi kuona kamati hiyo. Kamati hiyo kwanza imeundwa na nani na inatoka wapi? Hayo maneno yanatengenezwa na watu wa nje,” alisema Kamishna Mussa.
Alisema kinachofanyika hivi sasa ni kukitafuta ili kiweze kurejeshwa kunakohusika.
Taarifa zingine zilidai hata bendera ya mezani ya mwenyekiti wa SARPCCO, aliyokabidhiwa sambamba na upanga huo nayo kuna hatihati ilipotea.

Msemaji wa Jeshi la Polisi nchini, Advera Senso alipotakiwa kuzungumzia suala hilo alisema aulizwe kamishina wa polisi Zanzibar.
“Suala hilo muulize Kamishina wa Zanzibar ndiye anayejua,” alisema Senso.
Uchunguzi unaonyesha kuwa maofisa katika ofisi ya IGP na ile ya Kamishna wa Polisi Zanzibar, wamehojiwa akiwamo Kamishna Mussa, na kwamba upelelezi mkubwa umekuwa ukiendelea ndani ya jeshi hilo.

Hata hivyo, juhudi za gazeti hili za kutaka kufahamu uamuzi wa SARPCCO katika ofisi yake ya uratibu iliyopo kwenye ofisi za Makao Makuu ya Kanda ya Polisi wa Kimataifa (INTERPOL), Harare, Zimbabwe, hazikuzaa matunda baada ya baruapepe iliyotumwa kwa ofisa mratibu wa SARPCCO ambaye pia ni mkuu wa ofisi ya Kanda ya INTERPOL, C. Simfukwe kutopata majibu.

MAGAZETINI LEO JUMAMOSI 31-08-2013 NA Chiwambo's Blog





Thursday, August 29, 2013

DRC: Askari wa Tanzania Wa Umoja wa Mataifa auwawa,



Habari kutoka eneo la mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo katika mkoa wa Kivu ya kaskazini zinasema askari mmoja wa kikosi cha kuingilia kati cha Umoja wa mataifa kutoka Tanzania, ameuwawa.

Askari wengine watano wamejeruhiwa wakati wanajeshi wa serikali ya Kongo wakiungwa mkono na wale wa Umoja wa mataifa, walipokuwa wakipambana na waasi wa kundi la M23. John Kanyunyu na ripoti kamili kutoka Beni. Kuskiliza ripoti hiyo bonyeza alama ya spika za masikioni hapo chini.

Mwandishi: John Kanyunyu
Mhariri: Josephat Charo

MAGAZETINI LEO ALHAMISI 29-08-2013 NA Chiwambo's Blog






MWALIMU NYERERE ENZI ZA UHAI WAKE


Obama ahutubia maelfu Washington Akiwa Kwenye Maadhimisho ya Miaka 50 “I HAVE A DREAM”



Rais Barack Obama, Mkewe Michelle Obama, marais wa zamani Jimmy Carter na Bill Clinton Agosti 28, 2013

Akizungumza na maelfu ya watu waliohudhuria maadhimisho ya miaka 50 tangu maandamano ya kutetea haki za kiraia kufanyika jijini Washington, rais Barack Obama jana Jumatano alisema 'kazi haijamalizika' ya kutetea haki na usawa kwa wamarekani wote.

Miaka 50 baada ya Mchungaji Martin Luther king Jr. kutoa hotuba ya kihistoria na ya kusisimua akisema; "I have a dream" wakati wa ubaguzi mkubwa wa rangi Marekani, rais wa kwanza mweusi Marekani alisimama katika ngazi zile, zile alizosimama kwenye mnara wa kumbukumbuku wa Lincoln Memorial.

Bw. Obama alielezea wasifu wa Dr.King pamoja na kujitolea kafara kwa walioshiriki maandamano makubwa ya Washington miaka 50 iliyopita. Alisema kutokana na maandamano yao, sheria ya haki za kiraia ilipita. Na kwa sababu waliandamana sheria ya haki za kupiga kura ilitiwa saini na kwa sababu hiyo hiyo wasichana na wavulana weusi wanaweza kuishi maisha yao kikamilifu bila kuwa watumwa wa mtu mwingine.

Rais Obama aliendelea kusema na kwa sababu waliandamana, hata White House imebadilika huku maelfu ya watu wakimshangilia. Bw. Obama alisema maandamano hayo yalileta haki sio tu kwa wamarekani weusi lakini kwa watu wa rangi nyingine Marekani na duniani waliokuwa na kiu cha kuwa huru.

Alisema mengi yamebadilika tangu maandamano hayo ya mwaka wa 1963 lakini bado kuna kazi kubwa ya kufanywa. Alisema kuna mwanya mkubwa kati ya matajiri na maskini miongoni mwa watu wa rangi mbalimbali Marekani na migawanyiko mikubwa ya kisiasa hapa Washington inayofanya ndoto ya Martin Luther King Jr. kuonekana kuwa mbali sana kutimia.

Rais Obama alisema Marekani ina chaguo, ama kuendelea na msukumo huu mkubwa wa kidemokrasia, au kuzembea na kukifanya kizazi kijacho kuishi bila matumaini au kujikakamua na kufanya mabadiliko ya kuleta usawa na haki kwa wote.

Orodha ya waliotoa hotuba katika maadhimisho hayo ilikuwa ndefu, na ilijumwisha mwana wa kike wa Dr. King, mchungaji Bernice King, marais wa zamani Bill Clinton, Jimmy Carter, wacheza sinema maarufu na hata watangazaji mashuhuri wa televisheni. Mbunge John Lewis mmoja wa viongozi wa maandamano ya kutetea haki za kiraia mwaka wa 1963 alisema ingawa kuna maendeleo, ubaguzi wa rangi ungali umejikita katika jamii ya wamarekani.