Sunday, November 3, 2013

Pakistan yashutumu kuuawa Hakimullah



Kiongozi wa Taliban Pakistan Hakimullah Mehsud aliyeuawa kwa ndege isiyo na rubani
Pakistan imepinga vikali shambulio lililomuua kiongozi wa kikundi cha Taliban cha Pakistan, Hakimullah Mehsud.
Kiongozi huyo wa Taliban nchini Pakistan aliuawa katika shambulio la kutumia ndege isiyo na rubani.

Waziri wa mambo ya ndani wa Pakistan Chaudry Nisar Ali Khan amesema kifo cha Hakimullah Mehsud kimeharibu jaribio la serikali ya Pakistan la kuwa na mazungumzo ya amani na wapiganaji wa Taliban.

Ujumbe wa serikali ya Pakistan ulikuwa ukijitayarisha kukutana na wawakilishi wa Taliban katika mji wa Waziristan, kaskazini mwa nchi hiyo.
Habari zinasema wapiganaji wa Taliban wako katika hatua ya kumchagua mrithi wa nafasi ya Hakimullah Mehsud.

Hata hivyo bado hajatajwa ni nani.
Majeshi ya usalama yamewekwa katika hali ya tahadhari ya hali ya juu nchini Pakistan.
Katika matukio yaliyopita, Taliban walifanya mashambulio ya kulipiza kisasi kutokana na kuuawa kwa makamanda wake.

Hakimullah Mehsud, ameuawa kwa kutumia ndege zisizokuwa na rubani, shambulio hilo lililenga gari alimokuwa anasafiria Mehsud, Kaskazini Magharibi mwa Waziristan.
Hakimullah Mehsud alijulikana sana mwaka 2007 kama kamanda wa mwasisi wa kundi la Baitullah Mehsud, alipowakamata wanajeshi 300 wa Pakistani .
Chanzo: BBCSwahili

No comments: