Tuesday, November 5, 2013

Hoja ya Kigwangalla yapelekwa Kamati ya Haki, Maadili



Spika wa Bunge, Anne Makinda.PICHA|MAKTABA
Na Neville Meena,Mwananchi
Dodoma.Hoja ya kutaka kumng’oa madarakani Spika wa Bunge, Anne Makinda imewasilishwa katika Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge, gazeti hili limeelezwa. Hoja hiyo ni ile iliyoanzishwa na Mbunge wa Nzega, Dk Khamis Kigwangalla (CCM), ambaye jana aliitisha kikao cha wabunge wanaomuunga mkono ili kuweka mikakati ya kushinikiza hoja hiyo iwasilishwe bungeni. 

Katibu wa Bunge, Dk Thomas Kashililah alisema tayari wataalamu wake wameifanyia uchambuzi na kwamba, kwa mujibu wa Kanuni za Bunge madai ya mbunge huyo tayari yamewasilishwa mbele ya Kamati ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge kwa hatua zaidi.

“Tumefanya uchambuzi na ofisi yangu imeshaipeleka hoja yake katika kamati husika, kwa hiyo sasa mambo yote ni huko kwenye kamati,” alisema Dk Kashililah.
Wakati hayo yakiendelea, habari ambazo zilipatikana jana bungeni zinasema, huenda suala hilo likajadiliwa katika Kamati ya Uongozi ya Wabunge wa CCM na baadaye kwenye kikao cha wabunge wote wa chama hicho ili kulipatia mwafaka. 

Kulikuwa na taarifa kwamba, Dk Kigwangalla aliitwa na uongozi wa juu wa wabunge wa CCM kuhusu hoja yake hiyo, lakini alipoulizwa hakukiri wala kukanusha kuwapo mipango ya chama chake kuteka hoja yake hiyo.
Chanzo: Mwananchi

No comments: