Friday, March 21, 2014

Jukata yamhadharisha JK

               Rais Kikwete akipitia hotuba atakayoisoma katika Bunge Maalum la Katiba alipokuwa katika ndege kuelekea mjini Dodoma jana. 
Na Raymond Kaminyoge, Mwananchi
Dar es Salaam. Jukwaa la Katiba Tanzania (Jukata), limemtahadharisha Rais Jakaya Kikwete asiingie kwenye mtego wa wanasiasa wa chama chake cha CCM wanaoiponda Rasimu ya Katiba iliyowasilishwa bungeni Jumatatu kwa kuwa ndiyo iliyobeba maoni ya wananchi.

Wasiwasi wa Jukata umekuja baada ya baadhi ya viongozi wa Serikali na makada wa CCM, anachokiongoza kutoa kauli za kuipinga Rasimu hiyo hadharani.

Akizungumza na waandishi wa habari jana, Makamu Mwenyekiti wa Jukata, Hebron Mwakagenda alisema Rais Kikwete kesho (leo), atalihutubia Bunge Maalumu la Katiba na akiikashifu Rasimu hiyo atakuwa amejikashifu mwenyewe kwa sababu tume hiyo ipo kisheria.

“Mambo yaliyomo kwenye Rasimu hiyo si ya Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Joseph Warioba na wajumbe wenzake, bali ni maoni ya wananchi hivyo yanatakiwa kuheshimiwa,” alisema.

Mwakagenda alisema kazi iliyofanywa na Tume hiyo iheshimiwe na wabunge waendelee kuiboresha kabla haijapigiwa kura ya maoni na wananchi.

Akizungumzia kuchaguliwa kwa Mwenyekiti wa Bunge Maalumu la Katiba, Samuel Sitta na Makamu Mwenyekiti  Samia Sululu Hassan, Mwakagenda alisema utendaji wao wa kazi unahitaji kufuatiliwa kwa karibu kwa sababu wote ni mawaziri wa Serikali na makada wa CCM.

“Licha ya viongozi hawa kusifika kwa uadilifu, kwa nafasi zao za uwaziri kuongoza Bunge Maalumu la Katiba kunawaweka katika mtego wa kuingiliwa katika utendaji wao,” alisema na kuongeza:

“Jukata kwa niaba ya Watanzania inaahidi kuwafuatilia viongozi hawa wakati wote wa kuongoza Bunge Maalumu la Katiba kwa kuwashauri, kuwaonya na kuwarekebisha watakapokosea.”

Kuhusu tabia ya kuzomeana, alisema  kitendo hicho kinalivuruga Bunge na kusababisha wabunge kuacha kujadili masuala waliyotumwa na wananchi.

No comments: