Monday, March 31, 2014

AZAMU FC NJIA NYEUPE

WANALAMBALAMBA Azam FC jana walizidi kudhihirisha kuwa wabishi na kuzidi kujikita kileleni baada ya kuilaza Simba kwa mabao 2-1 katika mchezo wa Ligi Kuu ya Vodacom uliofanyika kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.

Wakati Azam FC ikizidi kubaki njia kuu na kulinda rekodi ya kutopoteza mchezo hata mmoja tangu ligi hiyo kuanza msimu huu, mabingwa watetezi Yanga, walichepukia Tanga na kujikuta wakishindwa kulimudu gwaride la Mgambo JKT kwa kukubali kichapo cha mabao 2-1 kwenye Uwanja wa Mkwakwani katika pambano lililotawaliwa na imani za kishirikina.

Katika Dimba la Taifa, kila timu ilianza kwa kasi na kushambuliana kwa zamu, ambapo dakika ya nane, Azam walilifikia lango la Simba na kumlazimisha kipa Ivo Mapunda kufanya kazi ya ziada kutokea na kumzuia Kipre Tchetche asifunge.

Simba walijibu mashambulizi dakika ya 12, kwa winga wake Ramadhani Singano ‘Messi’ kupiga shuti kali la mbali nje ya boksi na kudakwa na mlinda mlango, Aishi Manula.

Kutokana na kosa kosa hiyo, ndipo ilipobainika kuwa mashabiki wa Yanga walikuwa wakiishangilia Simba, tukio lililojibiwa kwa kuzomewa na mashabiki wa Simba.

Dakika ya 14, Mapunda kwa mara nyingine alifanya kazi ya ziada kupaa juu na kuokoa shuti la Khamisi Mcha ‘Vialli’ lililotokana na adhabu ndogo ‘free kick’.

Baada ya kosa kosa hiyo, Mcha alisawazisha makosa kwa kuifungia Azam bao dakika ya 17 kwa shuti jepesi ndani ya boksi, hivyo kuibua mgawanyiko miongoni mwa mashabiki wa Simba, ambao nusu walilishangilia.

Mashabiki hao walilishangilia kama ishara ya kushangilia anguko la Yanga, ambayo mashabiki wake walikuwa wakiishangilia Simba ili iifunge Azam na kuwajengea mazingira ya kutetea taji la Ligi Kuu.

Dakika ya 22, Singano alikosa bao la kuisawazishia Simba kwa shuti lake kupaa sentimita chache juu ya lango, kabla ya Amisi Tambwe naye kushindwa kufunga kwa kichwa, akiunganisha krosi ya Singano dakika ya 30.

Mcha, dakika 10 kabla ya filimbi ya mapumziko, aliikosesha Azam bao jingine, akishindwa kumalizia kazi maridadi ya Kipre.

Wakati mashabiki wakiamini mpira utaingia mapumziko Azam wakiwa mbele kwa bao 1-0, beki Joseph Owino aliisawazishia timu yake kwa kichwa dakika ya 45, akiitendea haki krosi ya Chanongo ambaye alikuwa mwiba kwa safu ya ulinzi ya Wanalambalamba.

Kipindi cah pili nacho kilianza kwa mashambulizi, kwa kila upande kusaka bao la ushindi, hivyo kushuhudiwa kosakosa kadhaa.

Kipindi cha pili, Azam waliingia kwa nguvu na dakika ya 57, walipata bao la pili lililofungwa na John Bocco ‘Adebayor’ kwa kichwa, akiunganisha mpira wa ‘tik tak’ ya Kipre iliyogonga mwamba na kurudi uwanjani.

Baada ya kufunga bao hilo, Azam ilionekana kupunguza kasi, hasa baada ya kutolewa Kipre ambaye alikuwa msumbufu katika safu ya ulinzi ya Simba.

Simba ikiwatumia vijana wake Chanongo, Mkude, Singano na wakongwe Uhuru na Tambwe, waliendelea kushambulia bila mafanikio.

Jitihada za Simba kusaka bao la kusawazisha nusura zizae matunda dakika ya 64, pale Tambwe alipokosa bao la kichwa akiwa na nyavu, kuunganisha krosi ya Chanongo.

Hadi mwamuzi Israel Nkongo akihitimisha dakika 90, Azam walitoka kidedea kwa mabao 2-1.

Kwa ushindi huo, Azam FC imefikisha pointi 53 na kuzidi kuitimulia vumbi Yanga iliyosalia na pointi 46.

Azam FC: Aishi Manula, Erasto Nyoni, Michael Gadiel, Aggrey Morris, David Mwantika, Kipre Balou, Himid Mao/ Bryson Rafael, Salum Aboubakar ‘Sure Boy’, Kipre Tchetche/ Bryan Umony, John Bocco na Khamis Mcha ‘Vialli’/Kelvin Friday.

Simba: Ivo Mapunda, William Lucian, Issa Rashid ‘Baba Ubaya’, Joseph Owino, Donald Musoti, Jonas Mkunde, Haruna Chanongo/Awadh Juma, Henry Joseph/Abdulhalim Humud, Amisi Tambwe, Uhuru Suleiman na Ramadhani Singano ‘Messi’/Badru Ally.

Jijini Tanga, Mgambo walianza kujipatia bao dakika ya kwanza, likifungwa na Fully Maganga.

Dakika ya 30, Mohamed Neto alilimwa kadi nyekundu na mwamuzi aliyejulikana kwa jina la Mahadhi, kwa madai ya kukutwa na kinachodaiwa kuwa ni ‘hirizi’ ndani ya nyeti zake. Hadi dakika 45, bao lilikuwa hilo moja.

Kupungua kwa Mgambo, kuliwaongezea nguvu Yanga ambao walizidi kuliandama lango la wapinzani wao na kufanikiwa kupata penalti dakika ya 52 baada ya beki mmoja kuunawa mpira eneo la hatari. Penalti hiyo ilifungwa na Nadir Haroub ‘Canavaro’. Matokeo yaliyodumu hadi mapumziko.

Kipindi cha pili, licha ya Mgambo kuwa pungufu, ilicheza mchezo wa kujihami na kushambulia kwa kushtukiza na dakika ya 64 Kelvin Yondani aliunawa mpira eneo la hatari na kuamriwa penalti iliyofungwa na Malimi Busungu.

Huko Mbeya, Tanzania Prisons ilizidi kukalia kuti kavu baada ya kukubali kichapo cha bao 1-0 kwa Mbeya City, likifungwa na Paulo Nonga, dakika ya pili.

Huko Kaitaba Kagera, maafande wa Ruvu Shooting walilazimisha sare ya bila kufungana na wenyeji Kagera Sugar.

Chanzo: Tanzania Daima

No comments: