Wednesday, March 26, 2014

SIASA TZ: UTEUZI KAMATI ZA BUNGE: SITTA APINGWA

MJUMBE wa Bunge Maalumu la Katiba, Profesa Ibrahim Lipumba, amekataa uteuzi wa nafasi ya ujumbe kwenye Kamati ya Uongozi uliofanywa na Mwenyekiti wa Bunge hilo, Bw. Samuel Sitta.

Alisema uteuzi huo hauna nia njema ya kupata Katiba Mpya na kudai Bw. Sitta, analiendesha Bunge hilo kwa matakwa ya Chama Cha Mapinduzi (CCM).
Prof. Lipumba alitoa msimamo huo bungeni mjini Dodoma jana baada ya Bw. Sitta, kutangaza majina matano ya wajumbe wa kamati hiyo ya uongozi.
Wajumbe hao ni Fakharia Hamis Shomari, Mary Chatanda, Prof. Lipumba, Amon Mpanju na Hamoud Abuu Jumaa.

Baada ya kutangaza majina hayo, mjumbe wa Bunge hilo Bw. John Mnyika, aliomba ufafanuzi kwa Bw. Sitta juu ya uteuzi huo na kudai kamati hiyo imekosa uwiano wenye sura ya kitaifa kwa pande mbili za Muungano ambazo ni Zanzibar, Tanzania Bara.

Pia Bw. Mnyika alisema, kamati hiyo pia haina mjumbe kutoka chama kikuu cha upinzani bungeni ambacho ni Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA).
Akitoa ufafanuzi wa madai hayo, Bw. Sitta alisema kamati hiyo imezingatia uwiano wa vyama na jinsia ambapo miongoni mwa wajumbe aliowateua mmoja ametoka Zanzibar, Bi. Faharia Hamisi Shomari na Prof. Lipumba angewawakilisha wajumbe wa kambi ya upinzani katika kamati hiyo.

"Si lazima kila chama kipewe nafasi ambazo zipo tano tu, sina ubaya na CHADEMA wala chama kingine chochote cha siasa ila nimejitahidi kufanya uteuzi kwa kuzingatia uwiano bila upendeleo hivyo naomba wajumbe turidhike," alisema Bw. Sitta.
Hata hivyo, Prof. Lipumba alisema hataweza kuingia katika kamati hiyo kama chambo akiwakilisha kambi ya upinzani kwani tangu awali, nia yake ya kujiunga na Chama cha Wananchi (CUF), ni kuiunganisha Zanzibar na Tanzania Bara.

"Jinsi  mchakato huu unavyokwenda ni wazi kuwa hakuna nia njema ya kupata Katiba ya wananchi, hivyo siwezi kuingia katika kamati kama mjumbe... nitapambana katika kamati yangu namba 10 ambayo inaongozwa na Bi. Anna Abdallah na ndani ya Bunge hili ili kujenga hoja.
"Nawaachia wenzangu muweze kuendelea na mipango yenu ya kulifanya Bunge hili kuwa la Chama Cha Mapinduzi (CCM), lakini kwa kweli, nimesikitishwa na mpango mlionao," alisema.

Naye mjumbe wa Bunge hilo, Bw. Kangi Lugola, alimwomba Bw. Sitta kubatilisha uteuzi wa wajumbe wa kamati hiyo kwa kuwatoa wajumbe ambao ni wanachama wa CCM na kuwaweka wajumbe kutoka upinzani ili kuondoa manung'uniko yaliyopo.
"Ni ukweli usiopingika kwamba, CCM tuko wengi hivyo nilitegemea dhana ya kutomeza wadogo isingekuwepo, ungeweza kuteua wajumbe watano kwa kuangalia jinsia na makundi Maalumu lakini asiwemo mjumbe wa CCM hata mmoja.

"CCM ni gari kubwa, tukiliacha likaserereka bila kukanyaga breki mara kwa mara, tutasababisha ajali nyingi sana katika utungaji wa katiba, wana CCM tusijenge hofu kwa sababu ya wingi wa wapinzani kuingia katika kamati ya Uongozi," alisema.

Alimshauri Bw. Sitta, kuondoa manung'uniko kwa kubatilisha uteuzi wake, kuchagua makundi mengine na kama kuna dhana ya Tanganyika kutomeza Zanzibar, kwa nini kusiwe na dhana ya CCM kutowameza watu wachache katika Bunge hilo?
Aliongeza kuwa, wajumbe wa Bunge hilo wamempa heshima na dhamana kubwa Bw. Sitta katika kuliongoza Bunge kwa kuzingatia weledi, umakini na umahiri wa kuhakikisha hakuna mzozo kwenye kutunga Katiba Mpya waitakayo Watanzania.

Akitoa ufafanuzi zaidi, Bw. Sitta alimshukuru Prof. Lipumba kwa uamuzi wa kukataa uteuzi huo na kusema ni haki ya mjumbe kupokea uteuzi huo au kuukataa kutokana na imani yake.
"Unapoteuliwa ni hiari yako kuipokea nafasi hiyo au kutoipokea, nashukuru Prof. Lipumba kwa kuamua kusema ulichokiona wewe ni ukweli na kukataa uteuzi wa Mwenyekiti," alisema Bw. Sitta.

Aliongeza kuwa, yaliyotokea yameshatokea kwani ni vigumu kufurahisha nafsi ya kila mmoja kwa lile analotaka lifanyike, hivyo hoja ya kuchagua wapinzani pekee katika kamati hiyo pia utakuwa ubaguzi kwa wengine hivyo ataendelea kutenda na kusimamia haki za Bunge hilo.

Mjumbe mwingine, Bw. James Mapalala alisema anatambua wingi wa CCM katika Bunge hilo ila kwa upande wake, hajaona faida ya wapinzani kuwepo bungeni kwani ni udhalilishaji.
Aliviomba vyama vyenye wajumbe wengi kama CCM katika Bunge hilo, viheshimu uchache wa wengine kwani wote wapo bungeni kwa ajili ya kupata Katiba Mpya ya Jamhuri ya Muungano si katiba ya chama fulani.

Alisema CCM imepoteza heshima na kuonesha dharau kwa wajumbe wengine wanaotoka vyama vingine vya siasa na makundi ambapo wajumbe kutoka chama tawala, wanatumia mabavu kufanya maamuzi ambayo yangepaswa kushirikisha wajumbe wote.
"Natoa mfano, jana (juzi), wakati tukitaka kuchagua Mwenyekiti kwenye kamati yangu namba moja, kuna mtu alikuja, kukaa kwenye kiti na kusema kuwa yeye ndio Mwenyekiti.

"Nilisimama kuhoji nani aliyemchagua ila wakasimama watu wengi na kusema huyo tumemchagua huku wakipiga makofi nikawa sina la kufanya ila nikasema sitopiga kura.
"Sisi tunaotoka vyama vidogo, tunapaswa kupewa heshima kama wajumbe wengine waliopo humu... tunaomba haki ya kuheshimiwa hata tukitoa mawazo yasiyozingatiwa," alisema Bw. Mapalala.

Naye Bw. David Kafulila, alisema katika moja ya nukuu ya Bw. Sitta, aliwahi kusema kati ya vipaumbele vyake ni kuweka usawa katika Bunge, lakini kauli yake kuwa wajumbe wa CCM ndio wengi katika Bunge hilo si jambo sahihi.

Alimshauri Bw. Sitta, kujipa muda na kufikiria uteuzi wake wa wajumbe watano katika kamati hiyo kwani hali si shwari kwani Bunge hilo limechukua sura ya nchi si chama.
Mchungaji Peter Msigwa, alisema ni kitu cha aibu kama wakifanya maamuzi ya kupitisha Katiba na wananchi wakayakataa hivyo suala la vyama lisiwepo katika Bunge hilo ili kupata Katiba bora.

Bw. James Mbatia, alisisitiza suala la Katiba liwe la Jamhuri ya Muungano na kumtaka kila mjumbe avae uhusika kama mwananchi wa Tanzania ili kukamilisha mchakato huo.
Naye Bw. Vincent Mzena, aliwasihi wajumbe kutoka CCM kutoonesha hisia zao za moja kwa moja ndani ya Bunge hilo kutokana na wingi wao kwani wajumbe wengine wanajiona wanyonge.

Aliwataka wajumbe wengine wasiotoka CCM, kutoogopa wingi wa wajumbe kutoka chama tawala bali wazingatie hoja ambazo watazitoa na kuzikubali kama zitakuwa za maana na kuzikataa kama zitakuwa hazina tija kwa Taifa.

Dkt. Ave-Maria Semakafu, aliwataka wajumbe wa Bunge hilo kuweka pembeni ushabiki wa vyama na kuhisi mambo bila kujua hatima yake na kama wajumbe wataona kuna mashaka katika uteuzi wa kamati hizo ni vyema wakatumia kanuni walizotunga ili kupata mwafaka wa jambo husika.

"Naomba tuache kuhisi, tukiona wanatuletea ratiba isiyoeleweka tutumie kanuni zetu kutengue baadhi ya kanuni zinazotuongoza ili tuweze kutengeneza mwafaka ambao utatuongoza na hatimaye kupata katiba bora," alisema Dkt. Semakafu.

Chanzo: Majira

No comments: