Sunday, March 30, 2014

MICHEZO: YANGA SC HATARINI KUKOSA MWANA NA MAJI YA MOTO, MBEYA CITY WAWANIA NAFASI YAO

Na Prince Akbar, Dar es Salaam
YANGA SC sasa wapo hatarini kukosa mwana na maji ya moto- hiyo inafuatia Mbeya City kuilaza Prisons bao 1-0 jioni ya leo Uwanja wa Sokoine, Mbeya na kurejea rasmi kwenye mbio za ubingwa wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara.

Bao pekee la Mbeya City leo limefungwa na Paul Nonga dakika ya kwanza tu ya mchezo na sasa timu hiyo ya Halmashauri ya Jiji la Mbeya inatimiza pointi 45 baada ya kucheza mechi 23.

Yanga SC baada ya kufungwa na Mgambo JKT mabao 2-1 Uwanja wa Mkwakwani, Tanga leo inabaki na pointi zake 46 za mechi 22, wakati Azam FC ipo kileleni kwa pointi 53 za mechi 23 baada ya kuifunga Simba SC mabao 2-1 leo.

Ikiwa sasa inaizidi pointi moja tu Mbeya City, Yanga SC inarejea Dar es Salaam kucheza na JKT Ruvu na baadaye Kagera Sugar kabla ya kucheza na JKT Oljoro na Simba SC.

Matokeo mengine ya leo, Kagera Sugar imelazimishwa sare ya bila kufungana na Ruvu Shooting, Mtibwa Sugar imeifunga mabao 3-1 Coastal Union na JKT Ruvu imeichapa 3-1 Rhino Rangers.

 Chanzo: Bin Zubery

No comments: