Tuesday, March 25, 2014

BABA AMUUA MWANAYE, AACHA UJUMBE MZITO

WATU wanne wamefariki dunia katika matukio tofauti mkoani Mbeya likiwemo la mkazi
wa Kata Migombani, Tarafa ya Tunduma, Bw. Juma Venance, kumuua kwa kumnyonga mtoto
wake mwenye umri wa mwaka mmoja na miezi saba, Henry Juma.

Akizungumzia tukio hilo, Kamanda wa polisi mkoani humo, Ahmed Msangi, alisema lilitokea
Machi 22 mwaka huu, saa 12 jioni katika Kata ya Migombani, Tarafa ya Tunduma, wilayani Momba.

Alisema mtuhumiwa baada ya kufanya unyama huo, alichukua mwili wa mtoto, kuulaza kitandani na kukimbia kusikojulikana akiwa
amefunga mlango kwa nje na kufuli.
Aliongeza kuwa, polisi na raia walivunja mlango, kuingia ndani na kukuta maiti ya mtoto ikiwa kitandani ambapo ndani ya chumba hicho kulikuwa na ujumbe ulioachwa na mtuhumiwa.

"Ujumbe huo ulisomeka hivi, “Unyama unyamani tutafute fedha kwanza niite J.M.A.K.A Gaidi,” alisema Kamanda Msangi na kuongeza kuwa, juhudi za kumtafuta mtuhumiwa zinaendelea
ili sheria iweze kuchukua mkondo wake.
Alitoa wito kwa mtu yeyote anayefahamu taarifa za mtuhumiwa huyo azitoe polisi ili aweze kukamatwa.

Katika tukio la pili, mwanafunzi wa Shule ya Msingi Chekechea Ilongo, Onesmo Haule (6), Mkazi wa Mahenje, amefariki dunia baada ya kugongwa na gari lenye namba T.597 BGU, aina ya Toyota Coaster, iliyokuwa ikiendeshwa na
Stanley Elia (44).

Kamanda Msangi alisema, tukio hilo limetokea Machi 22 mwaka huu, katika Kitongoji cha Ilongo, Wilaya ya Mbarali ambapo chanzo cha ajali hiyo ni mwendo kasi wa dereva ambaye amekamatwa.

Katika tukio lingine, mwanafunzi wa darasa la tatu Shule ya Msingi Kiwira, iliyopo Wilayani
Rungwe, Eva Mathias (11), mkazi wa Kijiji cha Ibiliro, amefariki dunia baada ya kusombwa na maji ya Mto Kiwira alipoteleza katika daraja lililojengwa kienyeji.
Kamanda Msangi alisema, tukio hilo limetokea Machi 20 mwaka huu, saa tatu asubuhi wakati

marehemu akiwa na dada yake aitwaye Vero Lucas (20), ambaye baada ya tukio alitoa taarifa

na ndipo juhudi za kumtafuta zilipoanza.

No comments: