Wednesday, March 26, 2014

Warioba afunguka,atoa ufafanuzi wa baadhi ya hoja za taarifa yake


Mwenyekiti wa Bunge Maalumu la Katiba, Samuel Sitta (kulia) akiongoza kikao cha kwanza cha Kamati ya Uongozi ya Bunge hilo, mjini Dodoma jana. Na Mpigapicha Wetu

Afafanua utata ulioibuliwa katika taarifa yake mbele ya Bunge la Katiba.

Dar es Salaam. Wakati Ikulu ikitangaza kwamba Rais Jakaya Kikwete amevunja Tume ya Mabadiliko ya Katiba, tume hiyo imetoa ufafanuzi wa baadhi ya maeneo ya Rasimu ya Katiba.

Taarifa ya Ikulu iliyotolewa jana, ilieleza kuwa Tume ya Jaji Joseph Warioba ilivunjwa tangu Machi 19, ikiwa ni siku moja baada ya kuwasilisha Rasimu ya Katiba bungeni mjini Dodoma.

Wakati taarifa ya Tume ya Warioba ilitolewa jana jioni, Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais, Ikulu ilikuwa imeshatoa taarifa ya kuvunja tume hiyo mapema jana ikieleza kuwa shughuli za tume hiyo zilikoma tangu  Jumatano iliyopita.

“Kwa mujibu wa kifungu cha 31 cha Sheria ya Mabadiliko ya Katiba, Rais wa Jamhuri ya Muungano alivunja rasmi Tume ya Mabadiliko ya Katiba tarehe 19 Machi, 2014 kwa Tangazo la Serikali Na.81 la tarehe 21 Machi, 2014,” ilisema taarifa hiyo ya Ikulu.

Hata hivyo,  Jaji  Warioba aliliambia gazeti hili jana kuwa hadi wanakutana juzi kwenye kikao cha mwisho cha tathmini walikuwa hawajapokea barua ya kuvunjwa kwa tume yake.

“Barua ya Ikulu tumeipokea leo. Tulikuwa hatuna taarifa kwamba tume yetu imevunjwa hadi tulipopokea barua leo (jana). Tulifanya kikao chetu cha mwisho cha tathmini jana (juzi),”  alisema Warioba alipozungumza na Mwananchi jana jioni.

Warioba pia alithibitisha kwamba taarifa ya ufafanuzi (imechapishwa ukurasa wa 37) ni ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba.

Taarifa hiyo ya Tume ya Warioba imetaja baadhi ya sababu za kupendekezwa kwa muundo wa serikali tatu kuwa, ni pamoja na Serikali ya Muungano kutokuwa tena na nguvu upande wa Zanzibar na Rais kupokwa baadhi ya madaraka aliyopewa kikatiba.

Ufafanuzi wa Tume

Taarifa hiyo ya tume ilisema: “Waasisi walituachia mambo 21 (ukiacha usajili wa vyama) kwenye orodha ya Muungano. Katika kipindi cha miaka ishirini iliyopita yamepunguzwa. Mambo yote yaliwekwa kwa utaratibu uliowekwa na Katiba lakini yameondolewa kinyume na Katiba.”

Iliongeza: “Sehemu zote mbili ziliamua kuachia baadhi ya mambo yake kuwa chini ya Serikali ya Muungano, sasa sehemu moja inaondoa mambo yake. Kwa hiyo Serikali ya Muungano itakuwa inashughulikia zaidi mambo ya upande mmoja.”

Kasoro nyingine iliyotajwa na tume hiyo ni hatua ya waasisi wa Muungano kuwa waliacha Bunge lenye madaraka nchi nzima, lakini sasa ni lazima sheria linazotunga zipate idhini ya Baraza la Wawakilishi kwa upande wa Zanzibar.

“Waasisi waliacha Rais akiwa na madaraka kamili.  Madaraka hayo yamepunguzwa bila kufuata utaratibu wa Katiba. Waasisi walituachia Mahakama ya Rufani yenye madaraka kamili. Madaraka haya yamepunguzwa. Waasisi waliunganisha nchi mbili ikawa moja.  Sasa tunazo nchi mbili,” ilisema taarifa hiyo na kuongeza:

“Hii ndiyo inafanya wananchi wa Tanzania Bara waamini Zanzibar ni huru katika mambo yao.  Wanaona ina mamlaka kamili kushughulikia mambo yake na imechukua rasilimali zake.  S

erikali ya Muungano imebaki na mamlaka na rasilimali za Tanzania Bara.”

Taarifa hiyo ilisema wakati wabunge wa Zanzibar wanashiriki kuamua mambo ya Tanzania Bara, wabunge wa Tanzania Bara hawana nafasi ya kushiriki katika kuamua mambo ya Zanzibar.

Tume hiyo ilisema ilikuwa vigumu kwa Zanzibar kurudi kwa hiyari kwenye hali ya awali, ikiwa ni pamoja na kufuta kipengele cha nchi mbili kwenye Katiba yake, hivyo waliamua kupendekeza mfumo wa serikali tatu kama hatua ya kuzingatia malalamiko ya Tanzania Bara.

Tume iliona kwamba pamoja na mambo haya kufanywa kinyume na Katiba ya Muungano, hali ibaki hivyo hivyo. Lakini kwa kufanya hivyo basi nayo yasipuuzwe.  Hivyo Tume nayo ikapendekeza Serikali ya Tanganyika iundwe.

Hali ilivyo

Tume hiyo imevunjwa huku kukiwa na mjadala mkali kuhusu hotuba ya Jaji Warioba katika Bunge Maalumu pamoja na ile ya Rais Kikwete aliyoitoa wakati akizindua Bunge hilo, Machi 21, mwaka huu.

Kutokana na hotuba hizo kukinzana, hasa kuhusu aina ya muundo wa Muungano unaotakiwa, baadhi ya wajumbe wa Bunge Maalumu walipendekeza Jaji Warioba apewe fursa ya kuitwa bungeni kutoa ufafanuzi wa masuala mbalimbali na pengine kujibu baadhi ya hoja zilizoibuliwa na Rais Kikwete.

Tume ya Mabadiliko ya Katiba iliundwa kwa mujibu wa kifungu cha 5 na 6 cha Sheria ya Mabadiliko ya Katiba, Sura ya 83 kwa Tangazo la Serikali Na.110 la 2012.

Wajumbe wake 30 waliteuliwa na Rais Kikwete kwa kushirikiana na Rais wa Zanzibar, Dk. Ali Mohamed Shein.

Chanzo: Mwananchi

No comments: