Sunday, March 30, 2014

Erdogan akabiliwa na mtihani wa utawala wake

Waziri mkuu wa Uturuki Recep Erdogan, anayekabiliwa na maandamano na kashfa za rushwa, anakabiliwa na mtihani muhimu Jumapili(30.03.2014) wakati wapigakura milioni 50 watapiga kura katika uchaguzi wa serikali za mitaa. Akitukuzwa kuwa ni "Sultan" na waungaji mkono wake nchini humo na akionekana kama "dikteta" na mahasimu wake wakubwa, Erdogan amefanya kampeni kwa wiki kadha pamoja na wagombea wa kiti cha meya, na kuufanya uchaguzi huo kuwa ni kura ya maoni kuhusu utawala wake wa miaka 11.

Matokeo, hususan katika mji mkubwa wa Istanbul na Ankara, yataathiri hali yake ya baadaye wakati akilenga kugombea kiti cha urais mwezi August, ama abadilishe sheria za chama na kugombea kipindi cha nne akiwa kama waziri mkuu mwaka ujao.
                           Waziri mkuu Erdogan katika mkutano wa kampeni

Akabiliwa na mzozo wa ndani
Miezi 10 iliyopita imekuwa ya mzozo mkubwa kwa Erdogan, kiongozi ambaye amesifiwa nyumbani na nje ya nchi hiyo kwa kuuendesha ukuaji wa uchumi wa nchi hiyo na kubadilisha hiyo ambayo iko katika bara la Ulaya na Asia kuwa mhusika mkubwa katika uchumi wa dunia.

Lakini tabaka la watu wa kipato cha kati wanaoishi mijini ambao hawahusishi dini kuwa ni msingi wa maadili limetengwa tangu polisi ilipokandamiza kwa nguvu wapinzani katika bustani ya Gezi mjini Istanbul, na kuzusha wiki kadha za mapambano ya mitaani ambayo yamesababisha watu wanane kupoteza maisha na wengine kwa maelfu wakiwa wamejeruhiwa.

Maandamano mjini Ankara
Ukandamizaji huo wa nguvu ulizusha hali inayoongezeka ya kiongozi wa kimabavu ambaye anataka kuwa mtawala pekee, wakati akipoteza washirika wake wa zamani, hususan kiongozi wa kidini ambaye anaishi hivi sasa katika jimbo la Pennyslvania nchini Marekani Fethullah Hulen, ambaye ni hasimu yake mkubwa.

Chama cha AKP katika uchaguzi nchini Uturuki
Wasaliti wa ndani
Erdogan amemshutumu imam huyo mwenye umri wa miaka 73, pamoja na wafuasi wake katika jeshi la polisi na mahakama nchini Uturuki , kwa kuhusika na wimbi la udukuzi na uvujaji katika mitandao ya kijamii na kufichua rushwa na mazungumzo ya ngazi ya juu kuhusu usalama wa nchi ambapo viongozi walikuwa wakizungumzia kuanzisha hatua za kijeshi dhidi ya Syria.

Jibu la serikali , hususan kuzuwia mtandao wa kijamii wa Twitter na YouTube katika wiki zilizopita, umezusha shutuma kali kutoka washirika wa Uturuki wa umoja wa NATO pamoja na makundi ya haki za binadamu. "Tutatowa somo kubwa kwa Pennyslvania, kwa wale ambao wanadukua mawasiliano ya simu," ameapa Erdogan katika mkesha wa uchaguzi. "Ni wasaliti ... ni majasusi..tutashinda tena, Mungu akijalia!"

Wakati uchaguzi ukikaribia , Erdogan mara kwa mara alisema kuwa "yeyote atakayeshinda katika mji wa Istanbul atashinda Uturuki". Kutokana na kulakiwa kwa hamasa kubwa meya wa zamani siku ya Jumamosi, wakati wafuasi wake wakimshangiria kwa sauti kubwa, wengine wakipanda juu ya miti kuweza kupata kumuona , chama chake cha Justice and Development AKP kinaonekana kuwa na nafasi nzuri ya kuendeza nafasi yake ya ushindi katika uchaguzi.
Mwandishi : Sekione Kitojo / afpe

Mhariri: Sudi Mnette
DW Swahili

No comments: