Friday, April 4, 2014

YANGA YAKANUSHA CHUJI, YONDAN, KASEJA KUSIMAMISHWA

Na Baraka Mpenja , Dar es salaam
0712461976
MABINGWA watetezi wa ligi kuu soka Tanzania bara wanatarajia kushuka dimbani jumapili ya wiki hii kuwakabili maafande wa JKT Ruvu kwenye uwanja wa Taifa jijini Dar es salaam.

Kikosi cha Yanga chini ya kocha mkuu, Mhoalanzi Hans Van der Pluijm kimeingia kambini jana jioni katika Hoteli ya Kiromo, huku kikiendelea kufanya mazoezi katika Uwanja wa Boko Beach Veterani.

Yanga waliopo nafasi ya pili kwa kujikusanyia pointi 46, pointi 7 nyuma ya Azam fc wenye pointi 53, watakuwa wanacheza mechi ya raundi ya 23 jumapili, huku wakisubiri kiporo chao dhidi ya Kagera Sugar aprili 9 mwaka huu uwanja wa Taifa, jijini Dar es salaam.

Mechi iliyopita jijini Tanga, Yanga walipoteza mchezo kwa kipigo cha mabao 2-1 dhidi ya wenyeji wao, Mgambo JKT na kuweka rehani ubingwa wao msimu huu.
Yanga wamebakisha mechi nne na kama watashinda zote watafikisha pointi 58 ambazo Azam fc pekee ndio wataweza kuzifikia kama watashinda mechi zao tatu zilizosalia.

Hata hivyo taarifa njema kwa mashabiki wa Yanga ni kuwa Mlinda mlango Deoragtias Munish "Dida" aliyekuwa majeruhi kwa takribani wiki mbili, ameshapona majeraha na ameungana na wenzake kambini tayari kwa maandalizi ya mchezo huo.

Katika hatua nyingine, Yanga kupitia tovuti yao rasmi wamekanusha taarifa zinazosambazwa na baadhi ya vyombo vya habari kwamba wachezaji wake, kiungo, Athuman Idd, beki Kelvin Yondani na Mlinda mlango, Juma Kaseja wamesimamishwa kutokana na timu kufungwa na Mgambo JKT.

"Taarifa hizo hazina ukweli, wachezaji hao hawajafukuzwa na wapo wanaendelea na mazoezi pamoja na wenzao". Alifafanua taarifa ya Yanga.

Pia Yanga wameviomba vyombo vya kutoa taarifa za ukweli na sio kupotosha jamii na mwisho wa siku kuwapa usumbufu viongozi kufanya kazi ya kukanusha.
Mchezo wa jumapili utakuwa mgumu kwa timu zote kutokana na kusimama maeneo mawili tofauti kwenye msimamo wa ligi kuu.
Yanga wapo nafasi ya pili na wanapambana kutetea ubingwa wao walioutwaa msimu huu.

Wataingia katika mchezo huo wakiwa na kumbukumbu ya kuwafunga JKT Ruvu mabao 4-0 katika mechi ya mzunguko wa kwanza mwaka jana.
Haitakuwa kazi nyepesi kwa Yanga kumfunga aliyekuwa kocha wake msaidizi ambaye kwasasa ni Kocha mkuu wa JKT Ruvu, Fredy Felix Minziro.
Minziro na kikosi chake wapo nafasi ya 9 kwa kushuka dimbani mara 23 na kujikusanyia pointi 28 kibindoni.

Maafande hao wataingia uwanjani wakiwa na kumbukumbu ya kuibuka na ushindi wa mabao 3-1 mechi iliyopita dhidi ya Vibonde, Rhino Rangers kwenye uwanja wa Azam Complex.

Mechi ya jumapili ni muhimu kwao kwasababu wanahitaji zaidi pointi ili kujiweka mazingira mazuri ya kubakia ligi kuu.
Uzoefu unaonesha kuwa timu zilizopo katika hatari ya kushuka daraja huwa zinacheza kwa kujituma zaidi, na ndio maana Mgambo JKT walipambana na Yanga ndani ya dakika zote 90 na kushinda.

Kwa jicho la harakaharaka, unaweza kuwapa asilimia kubwa Yanga kuwa watashinda mchezo huo, kutokana na mazingira yao.
Kupoteza au kutoa sare kutazidi kuwaweka Yanga mazingira magumu zaidi ya kutetea ubingwa wao.

Matokeo yanayowafaa pekee ni ushindi, kwasababu moto wa Azam fc kueleka kutwaa ubingwa ni mkali sana.
Itakuwa mechi muhimu kwa Yanga, na kocha mkuu Pluijm atahitaji kutuliza akili zake kwani sasa matokeo hayatabiriki.

Haikuwa rahisi kuamini kama Mgambo wangewafunga Yanga waliokamilika pale Mkwakwani, lakini mpira una matokeo ya ajabu wakati fulani.
Yanga wanatakiwa kuingia jumapili kwa tahadhari kubwa kwasababu kiwango cha sasa cha JKT Ruvu si cha kubeza. Wanaweza kufanya lolote na kuwaharibia zaidi wanajangwani.

Chanzo:Shaffihdauda.com

No comments: