Saturday, April 5, 2014

Okwi alipwa mshahara wa TP Mazembe

NA MWANAHIBA RICHARD
EMMANUEL Okwi ndiye mchezaji pekee anayewafunika wachezaji wote wanaocheza Ligi Kuu Bara kwa kuwa na mshahara mnono sawa na wachezaji wa klabu maarufu ya Afrika ya TP Mazembe. Mshahara anaolipwa straika huyo unatosha kumlipa Haruna Niyonzima na Mrisho Ngassa kwa mwezi.

Achana na hao njoo Simba, ukichukua fungu la dola 4,000 sawa na Sh 6.4 milioni za Kitanzania anazolipwa fowadi huyo zinatosha kulipa mishahara ya wachezaji watatu muhimu wa Msimbazi, Amissi Tambwe, Joseph Owino na Ramadhani Singano ‘Messi’.

Kiasi hicho anacholipwa Okwi ni zaidi ya fedha aliyokuwa akilipwa pia mshambuliaji wa zamani wa Simba, Felix Sunzu ambaye alikuwa analipwa Sh 5 milioni kwa wakati huo akiwa ndiye mchezaji pekee ghali kuliko wote.

Mshambuliaji huyo wa Yanga raia wa Uganda alisajiliwa na mabingwa hao wa soka nchini wakati wa usajili wa dirisha dogo akitokea SC Villa ya Uganda baada ya kutofautiana na timu yake ya Etoile du Sahel ya Tunisia alikouzwa na Simba msimu uliopita.

Usajili wa Okwi ulileta utata mkubwa ambao ulisababisha akose baadhi ya mechi mpaka ulipotolewa ufafanuzi kutoka Shirikisho la Soka la Kimataifa (Fifa) kwa kile kilichokuwa kinadaiwa kuwa ana mkataba na Etoile du Sahel.

Hivi sasa Okwi ameonekana kuanza usumbufu ndani ya klabu hiyo baada ya kudaiwa kuondoka kambini bila ya kutoa sababu za kufanya hivyo huku akiwa ameifungia Yanga mabao matatu pekee tangu ajiunge nayo.

Mbali na mchezaji huyo wachezaji wengine wanaofaidi mishahara minono kutoka Azam FC ni Kipre Tchetche, Kipre Balou, John Bocco, Agrey Morris, Briany Omony na Haruna Niyonzima wa Yanga ambao  wanapata Sh 4 milioni.

Beki Mbuyu Twite wa Yanga yeye anapata Sh 3.6 milioni huku beki wa Simba Joseph Owino ndiye anayeingiza fedha ndefu ndani ya klabu hiyo kwa kupokea mshahara wa dolla 2,000 sawa na Sh 3.2 milioni.

Yanga imeonekana kuwafunika wachezaji wa Simba kwani wachezaji wake wengi wanapata mishahara ya kuanzia Sh. milioni moja kupanda juu huku wachezaji wa Simba wengi wao wakianzia shilingi milioni moja kushuka chini.

Mwanaspoti limebaini kuwa wachezaji wazawa hakuna anayelipwa mshahara wake zaidi ya Sh 5 milioni walio wengi mishahara yao haizidi Sh 1 milioni ingawaje wachache wamefikisha Sh 4 milioni.
Chanzo: Mwanaspoti


No comments: