Friday, April 4, 2014

Wajawazito Chalinze watumia trekta kwenda hospitali


WANAWAKE katika Kitongoji cha Makupani, Kijiji cha Saadani chumvi, wanalazimika kusafiri umbali wa kilomita 12  kwa kutumia trekta kufuata huduma ya kujifungua hospitalini.

Wakizungumza katika mkutano wa kampeni za mgombea ubunge wa Chalinze kwa tiketi ya CCM, Ridhiwani Kikwete, wakazi  hao walisema  wamekuwa wakikabiliwa na mazingira magumu kutokana na kukosekana kwa usafiri wa uhakika.

Walisema pindi mama mjamzito anapohitaji huduma hiyo nyakati za usiku, mwekezaji wa Kampuni ya Seasalt ndiye anayewasaidia trekta hilo kwa ajili ya kumsafirisha mgonjwa, hali ambayo ni ya hatari kwani kuna uwezekano wa kujifungua njiani.

Wananchi hao walimuomba mbunge atakayechaguliwa kuhakikisha anawapatia usafiri wa uhakika ili waweze kuondokana na kero hiyo.

Mwenyekiti wa kitongoji hicho, Mohamed Salum, alikiri kuwepo na changamoto hiyo na kusema inachangiwa na viongozi wa ngazi za juu kutotembelea eneo hilo.

Kwa upande wake, Ridhiwani aliwaomba wananchi  hao wamchague  ili waweze kushirikiana kutatua changamoto mbalimbali jimboni humo.

Chanzo: Tanzania Daima

No comments: