Wednesday, April 9, 2014

Necta kuongeza kiwango cha ufaulu sekondari

Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi,Jenista Mhagama.

Baraza la Mitihani la Tanzania (Necta), limejipanga kuongeza kiwango cha ufaulu kwa wanafunzi wa sekondari nchini kwa kusambaza vitabu vya tathimini ya uchambuzi wa ufaulu kwa kila mtihani uliofanywa.

Usambazaji wa vitabu hivyo utakafanyika kwa shule zote nchini ikiwa ni utekelezaji wa Mpango wa Matokeo Makubwa sasa (BRN) ili kuwawezesha walimu na wanafunzi kubaini makosa kwenye mitihani mbalimbali iliyofanywa.

Naibu Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Ufundi, Jenista Mhagama, akizindua vitabu hivyo mwishoni mwa wiki  iliyopita jijini Dar es Salaam, alisema vitaonyesha tathimini ya ufaulu kwa kila swali katika kila somo, matakwa ya maswali na jinsi watahiniwa walivyoyajibu kwa kupata au kukosa.

“Uchambuzi huu utawasaidia walimu  na wanafunzi kubaini makosa mbalimbali yanayofanywa na watahiniwa wakati wa kujibu maswali na hivyo kujifunza mbinu bora za kujibu maswali hayo, itasaidia kuboresha kiwango cha ufaulu cha watahiniwa kwa miaka ijayo,” alisema.

Alisema ni vema vitabu hivyo vikawekwa kwenye tovuti ili wadau wengi waweze kuvisoma kwa njia ya mtandao na kupata taarifa sahihi ya tathimini ya ubora wa elimu na hivyo kutekeleza mikakati mbalimbali ya kuboresha kiwango cha elimu.

Kaimu Katibu Mtendaji wa Necta, Dk. Charles Msonde, alisema jitihada za pamoja katika kuboresha ufundishaji na ujifunzaji zinahitajika ili kuongeza ubora wa elimu kwenye masomo yote kwa kuwa ufaulu kwenye masomo yote uko chini ya asilimia 50.

Alisema chini ya BRN, Wizara ilijiwekea mikakati tisa ya kutekeleza ambayo ni upangaji wa shule kwa ubora wa matokeo, utoaji wa tuzo kwa shule zilizofanya vizuri, kuwa na kiongozi cha usimamizi wa shule, upimaji wa kitaifa wa stadi za kusoma.

Naibu Waziri wa Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi) (Elimu), Kassim Majaliwa, alisema vitabu hivyo vitawasaidia walimu na wanafunzi kubainia mambo yenye changamoto katika ujifunzaji na ufundishaji na sababu za kuwafanya watahiniwa washindwe kujibu maswali.

Majaliwa aliwaagiza maafisa elimu wa mikoa, wilaya na kata kufuatilia matumizi ya vitabu hivyo na kuhakikisha kila shule inapata nakala  kwa kuwa ni nyenzo muhimu katika kufanya kazi.


CHANZO: NIPASHE

No comments: