Wednesday, April 9, 2014

WHO: uvumi wa maambukizi ya Ebola ukome

Shirika la Afya Duniani, WHO, limesema kuwa kuzuka kwa Homa ya Ebola Magharibi mwa Afrika ni mojawapo ya changamoto kubwa zaidi ambazo limewahi kukabiliana nayo.

Shirika hilo limesema kuwa italichukua hadi miezi minne kuthibiti ugonjwa huo. Wakati huohuo shirika la kutoa misaada ya matibabu ya bure, Medicins Sans Frontieres, limesema kuwa linaendelea kufanya mashauriano na viongozi wa kijamii katika Wilaya moja Kusini mwa Guinea, ambalo lilisimamisha shughuli zake baada ya vituo vyake kadhaa kushambuliwa na wakaazi wa eneo hilo.

Msemaji wa shirika hilo katika mji mkuu wa Guinea wa Conakry - Sam Taylor - amesema inaeleweka kwamba watu wana uoga mkubwa.
"Sio taharuki, kimsingi huu ni uoga. Na tunaelewa hilo. Ni ugonjwa wa kugovya na pia ni mpya nchini Guinea, na kuna uvumi unaosambaa na pia kuna habari za kuotosha zinazoenea; na tunachohitaji kuona kwa wingi sasa ni watu kwenda kwa jamii mbalimbali kueleza ugonjwa huu, jinsi unavyoenea, na jinsi usivyoenea," alisema Bwana Taylor.

Ugonjwa huo umewaua watu 111 katika nchi za Guinea na Liberia tangu uchipuke mwezi uliopita.

No comments: