Wednesday, April 9, 2014

Watu wenye ulemavu watengewe bajeti`

`

Diwani wa Kata ya Ngarenaro, Isaya Doita, (Chadema), amezitaka halmashauri kutenga bajeti kwa ajili ya watu wenye ulemavu  kupata mahitaji yao badala ya halmashauri hizo kutenga asilimia 10 kwa ajili ya wanawake na vijana pekee.

Aidha, watoto wenye ulemavu wa kutosikia, wameiomba jamii kuachana na tabia ya kuwaficha majumbani badala yake wawapeleke mashuleni kwa ajili ya kupata elimu na kujikomboa kimaisha.

Akizungumza na watoto wenye ulemavu pamoja na wananchi mbalimbali waliokusanyika kuwasikiliza   viwanja vya Soko Kuu jijini Arusha.

Alisema wakati umefika sasa kila kata kutambua watu wenye ulemavu ili waweze kutengewa  bajeti yao na kupata misaada mbalimbali waweze kuinuka badala ya kuonekana ni mzigo ndani ya familia zao.

Alisema ikiwa halmashauri inatenga asilimia 10 yaani asilimia 5 inakwenda kwa kinamama na tano inakwenda kwa vijana huku jamii yenye ulemavu ikiwa haitengewi bajeti .

Naye mwakilishi wa kutetea haki za watoto pamoja na watoto wenye ulemavu mkoani Arusha, Hafsa Mgaza, aliiomba jamii kuacha tabia ya kunyanyasa watoto hususan wenye ulemavu kwani kila mtu ni mlemavu mtarajiwa bali walindwe na kuheshimiwa kama jamii nyingine zenye mahitaji.

Pia alisisitiza kuwa si jambo jema kumuona mlemavu akinyanyasika na mwenye viungo akimwangalia.

Aidha, aliiomba serikali pamoja na taasisi mbalimbali kuhakikisha wanapojenga majengo yanakuwa ni rafiki kwa jamii hiyo hususan vyooni kwani baadhi yao hupata taabu wanapohitaji kwenda msalani na maeneo mbalimbali kwa ajili ya mahitaji yao.

Ofisa Maendeleo ya Jamii Mkoa wa Arusha, Blandina Mkini, alisema serikali itaendelea kushirikiana na jamii hiyo katika kuhakikisha haki zao zinalindwa na kutoa rai kwa jamii kuacha tabia ya kuwabaka watu wenye ulemavu.

CHANZO: NIPASHE

No comments: