Tuesday, April 8, 2014

Msako wa wageni Kenya waendelea


Maafisa wa Polisi nchini Kenya wanasema wamekamata zaidi ya watu elfu tatu katika msako dhidi ya wageni nchini humo .
Msako huo ulianza Ijumaa, baada ya mashambulizi ya gurunade wiki iliyopita katika eneo la Eastleigh linalokaliwa zaidi na wasomali katika mji mkuu Nairobi.
Wengi wa waliokamatwa ni wasomali .

Inspekta mkuu wa polisi , David Kimaiyo, amesema kuwa watu 450 bado korokoroni asili mia kubwa yao ikiwa katika uwanja wa michezo wa Kasarani huku waliosalia wakiruhusiwa kwenda zao baada ya kuchunguzwa na maafisa
wa usalama na wale wa uhamiaji kubaini uhalali wao .

Umoja wa Mataifa, makundi ya kutetea haki za binadamu na jamaa wa watu hao wanasema hawajapewa ruhusa ya kuwaona wapendwa wao.
Waziri wa mambo ya ndani wa Kenya Joseph Ole Lenku, anasema wale ambao hawana vibali vya kuishi nchini watachukulia hatua zaidi.

Sitini na tisa wamepelekwa mahakamani kwa madai ya kuwepo nchini Kenya bila idhini au kumiliki stakabadhi gushi.
Mwandishi wetu Robert Kiptoo ambaye amezuru mtaa huo wa Eastleigh ametueleza kuwa msako wa polisi dhidi ya wahamiaji haramu na washukiwa wa ugaidi bado unaendelea .

Msemaji wa polisi nchini Kenya Masoud Mwinyi amekanusha madai kuwa polisi wanalenga jamii moja ama watu wa dini moja.
Mashirika ya kijamii na yale ya kutetea haki za kibinadamu yanalalamika kuwa yamenyimwa fursa ya kuwatembelewa washukiwa hao waliokamatwa.
Miongoni mwa waliokamatwa ni raia wa Kenya, Uganda, Sudan, Sudan Kusini ,hata hivyo idadi kubwa inatoka Somalia.

Aidha ripoti zinasema kuwa wageni wengi wamekimbilia miji mingine nchini Kenya kukwepa msako huo wa polisi lakini.
Serikali imetoa onyo kwa Wakenya kutowasaidi watu ambao wanawashuku kuwa wageni.

Serikali ya Kenya imeonya kuwa haitawavulimia wakimbizi mijini ikisema kuwepo kwao mijini kunahujumu usalama wa taifa.

Chanzo: BBC Swahili

No comments: