Sunday, October 27, 2013

WAZIRI NCHIMBI AFANYIWA VURUGU NA WANANCHI WAMFUNGIA BARABARA






Wananchi wenye hasira wakifunga njia kwa kutumia vyuma vya kingo vya daraja kuzuia msafara wa Dkt.Emmael Nchimbi kupita wakati akienda kwenye mkutano wa hadhara ambao baadae ulifanyika kwenye viwanja vya shule ya sekondari ya kutwa ya matarawe iliyopo katika manispaa ya Songea (picha na Gideon Mwakanosya)


Diwani wa kata ya Matarawe (CCM) Makene aliyesimama katikati akijaribu kuwatuliza wananchi wa kata hiyo ambao walifunga barabara itokayo mjini kwenda matarawe kwa zaidi ya masaa mawili wakimshinikiza mbunge wao Dkt. Nchimbi awasaidie kulipanua daraja ambalo wamedai kuwa limekuwa likisababisa ajari nyingi pamoja na vifo aliyesimama nyuma yake ni Dkt Nchimbi (picha na Gideon Mwakanosya).

HABARI KAMILI

na Stephano Mango, Songea
MSAFARA wa Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Dk. Emmanuel Nchimbi, umepigwa mawe na wananchi waliojitokeza kuzungumzia kero ya daraja la Matarawe, ambalo linadaiwa kusababisha vifo vya watu zaidi ya watatu mwezi Oktoba mwaka huu.
Tukio hilo limetokea jana saa 10:00 jioni hadi saa 12:00,  ambapo wananchi hao wakiwa na hasira walifanya fujo wakimshinikiza Nchimbi ambaye ni Mbunge wa Jimbo la Songea  Mjini awasaidie kupanua daraja  hilo ambalo kwa  muda mrefu limesababisha kutokea kwa ajali za mara kwa mara katika eneo hilo.

Wananchi hao wa Kata ya Matarawe,  Manispaa ya Songea, wakiwamo waendesha  pikikipiki maarufu kwa jina la ‘yeboyebo’  walifunga barabara kwa  zaidi ya saa mbili huku wakifanya fujo za kung’oa kingo za daraja, kuweka  magogo na mawe  katikati ya daraja na kuchoma matairi moto  ili kumzuia kiongozi huyo asiweze kupita na atoe majibu ya kina juu ya daraja hilo.

Hatua hiyo ilililazimu Jeshi la Polisi kuwatawanya  wananchi hao kwa kuwafyatulia mabomu ya machozi ili kukabiliana na uharibifu pamoja na kuruhusu msafara huo uweze kupita.

Aidha, kufuatia vurugu hizo, Jeshi la Polisi liliweza kuwashikilia watu wanane.
Hata hivyo Dk. Nchimbi alilazimika kusimama na kushuka kwenye gari lake  akiwa ameongozana na viongozi mbalimbali wa  chama na serikali akiwamo Mkuu wa Wilaya ya Songea, Joseph Joseph Mkirikiti,  ambapo aliwapa pole kwa ajali zinazotokea huku akiwataka kuwa na subira  wakati ombi lao linashughulikiwa.

“Natoa pole sana kwa msiba na ajali ambazo zimetokea nimewasikia, na ninaahidi  nitawajengea daraja  hili, kama nimeweza kujenga barabara hii kwa kiwango cha lami bila maandamano wala kufungiwa barabara nitashindwa daraja?” alihoji.

Nchimbi alisema kuwa vitu hivyo vinavyozungumzika hakuna haja ya kufanya maandamano na kuwataka wananchi hao kuhudhuria mkutano wake kwa kuwa anajua ufinyu wa daraja hilo na ameahidi kulifanyia maboresho zaidi.
Naye Diwani wa kata hiyo,  James Makene, aliungana na kundi la wananchi hao na kumueleza Nchimbi kuwa  hiyo ni changamoto ambayo wakazi wake  wamekuwa wakilia kwa kipindi kirefu.

Aidha, Kamanda wa Polisi wa mkoa huo, Deusdedit Msimeki, alisema kuwa kufuatia vurugu hizo tayari watu wanane wanashikiliwa na wanaendelea kuhojiwa zaidi ili kuwabaini vinara wengine waliosababisha  fujo hizo.
Chanzo: Tanzania Daima/ Mjengwablog
 


No comments: