Thursday, October 31, 2013

Serikali kutorudisha majeshi ya Kongo

 

na Happiness Mnale
SIKU chache baada ya kutokea kwa kifo cha mwanajeshi wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), Luteni Rajabu Mlima, aliyekuwa katika operesheni ya kulinda amani Mashariki mwa Kongo (DRC), serikali imesema haitatetereka wala kurudi nyuma kwa kurudisha majeshi yake nchini.

Akizungumza jijini Dar es Salaam jana wakati wa kuaga mwili wa marehemu Mlima katika viwanja vya jeshi Lugalo, Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Shamsi Vuai Nahodha, alisema serikali itaendelea kutoa ushirikiano kwa wanajeshi waliobakia nchini humo ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa kulinda amani ya wananchi wa Kongo.

“Kama serikali tunasikitika kwa kifo cha mwanajeshi wetu, lakini hili halitufanyi kushindwa kuendelea kulinda raia wa Kongo na bado tunaendelea kutoa hamasa kubwa kwa wanajeshi waliobaki waendelee na majukumu yao kama kawaida.
“Kikubwa tutaendelea kutoa ushirikiano kwa familia ya marehemu kwa kuhakikisha shughuli zote za mazishi zinaenda sawa pamoja na kuwa nao karibu katika kipindi hiki kigumu cha majonzi,” alisema Nahodha.

Awali akisoma salamu za rambirambi kwa niaba ya Mkuu wa Majeshi Nchini (CDF), Davis Mwamunyange, Mnadhimu Mkuu wa Jeshi la Ulinzi, Luteni Jenerali, Samuel Ndomba, alisema marehemu Mlima alipigwa risasi Oktoba 27, saa 5:00 asubuhi, akiwa katika milima ya Cavana iliyoko mashariki mwa Kongo na kufa papo hapo.
Chanzo; Tanzania Daima


No comments: