Wednesday, October 30, 2013

Tanzania yasita katika uanachama wa EAC.



Serikali ya Tanzania inakusudia kutoa uamuzi mgumu juu ya kuendelea na uanachama wa Jumuiya ya Afrika ya Mashariki baada ya wiki mbili, endapo itajidhihirisha sheria zilizounda jumuiya hiyo, zimevunjwa.

Kusudio hilo la serikali, limetangazwa bungeni mjini Dodoma na Waziri wa Ushirikiano wa Afrika ya Mashariki, Bw. Samwel Sita, wakati alipokuwa akijibu maswali ya wabunge Rukia Ahmed wa Viti Maalum (CUF) na John Komba wa Mbinga Magharibi.

Aidha, Mbunge wa Mbinga Magharibi, Bw. Komba akahoji ni kwanini Jumuiya hiyo hailaani kitendo cha baadhi ya nchi wanachama kuunda jumuiya nyingine ndani ya jumuiya hiyo.

Hata hivyo kufuatia maswali mfululizo kutoka kwa wabunge wengine, Waziri huyo wa Ushirikiano wa Afrika ya Mashariki, akaweka wazi kuwa serikali haijakaa kimya, bali imeaanza kuchukua hatua kadhaa, kukabiliana na hila zinazofanywa na wanachama wengine wa jumuiya.

Kamati ya bunge ya bajeti, imeishauri serikali kuangalia mfumo wake wa matumizi ya kawaida, kwa kuwa hauendani na ule wa matumizi ya maendeleo, kama yalivyopangwa kwenye bajeti kuu.

Ushauri huo umetolewa bungeni mjini Dodoma na Mwenyekiti wa Kamati ya Bajeti na Mbunge wa Bariadi Magharibi, Bw. Andrew Chenge, wakati alipokuwa akiwasilisha maoni ya kamati hiyo, kufuatia kuletwa kwa hoja yenye mpango wa maendeleo wa taifa kwa mwaka 2014/2015.

Aidha, kamati hiyo ya bunge imekosoa mfumo wa sasa bajeti ya serikali, kuwa umekuwa ni chanzo kimoja wapo kinachosababisha bajeti za maendeleo kushindwa kutekelezwa kwa asilimia 100.

Hawali akiwasilisha mapendekezo ya mpango wa maendeleo wa taifa kwa mwaka 2014/2015, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Mahusiano na Uratibu Bw. Steven Wasira amefafanua kuwa mpango huo utatoa umuhimu na kutambua vichocheo vilivyopo nchini, kikanda na dunia, na kuvitumia, ili kupata matokeo chanya kwa haraka.
Chanzo: VOA Kiswahili

No comments: