Monday, October 28, 2013

CUF YAKOSOA OPERESHENI YA KUONDOA MAJANGILI

                                                          Picha hii ni ya Maktaba



Chama cha Wananchi (CUF) kimelaani vitendo vya wananchi kupigwa, kuteswa na wengine kupoteza mali zao wakati wa utekelezaji wa operesheni kuondoa majangili na wahamiaji haramu katika maeneo mbalimbali ya nchi.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa kwa vyombo vya habari Dar es Salaam jana na kusainiwa Naibu Mkurugenzi wa Habari na Haki za Binadamu na sheria wa CUF, Abdul Kambaya, operesheni hiyo imesababisha mtu mmoja kupoteza maisha na wengine kupoteza mali zao.

Alisema katika maeneo inapofanyika operesheni hiyo kama vile Katavi na Kilindi kumeripotiwa kutokea madhara makubwa ya wananchi kupigwa na mmoja kuuawa katika Kata ya Majimoto mkoani Katavi.
Pia alisema Diwani wa Kata Majimoto mkoani katavi aliyetambulika kwa jina moja la, Serengeti alipigwa na vikosi vinavyohusika kwenye operesheni hiyo pale alipo hoji iweke operesheni hiyo ifanyika kwenye Kata anayoiongoza bila ya kujulishwa ili aweze kutoa ushirikiano.

"Mkazi mmoja alipigwa risasi na Vikosi hivyo vinavyotekeleza Operesheni hiyo na Mchungaji wa Kanisa la Anglikana, Geofrey amekimbia kipigo na kuacha nyumba yake kukiwa na sh. 800,000 na Biblia ambazo zimechukuliwa," alidai Kambaya.
"CUF kinamuomba Rais Kikwete kulitazama jambo hili kwa undani na kuweza kuwasaidia wa nanchi kuondokana na adha kubwa wanayopata, " alisema Kambaya.
Aliongezea kuwa vikosi vinavyoendesha operesheni hiyo vijue kuwa si kila mwananchi ni mhamiaji haramu au jangili, hivyo kazi hiyo ifanyika kwa mujibu.

Alisema utaratibu unaotumika utashusha heshima ya vikosi vyetu vya Ulinzi ndani ya Taifa letu, lakini utaratibu huo utafanikiwa kujenga hofu na uadui baina ya wananchi na vikosi vyetu vya Ulinzi.

Alitoa wito kwa Taasisi za Haki za Binadamu na Mambo ya Sheria kuweza kufika Mkoa wa Katavi Kata ya Majimoto kwenda kujionea hali ilivyo .
Pia Taasisi zinazojishughulisha na kutoa Misaada ya Kibinadamu kama Msalaba Mwekundu na nyingine kwenda mkoani Katavi kutoa misaada kwa familia zilizoathirika na Operesheni hiyo.


No comments: