Wednesday, October 30, 2013

Wabunge waomba kuongezwa mishahara



•  Mnyika apinga, ataka posho zifutwe, Lissu awafunda 
 
na Mwandishi wetu
WAKATI watumishi wa umma wakitaabika na mishahara midogo, huku wakipendekeza marupurupu ya wabunge yapunguzwe, wabunge wa CCM juzi waliwaweka kitimoto viongozi wa Bunge wakitaka mishahara yao ipandishwe.

Madai hayo yanakuja zikiwa ni siku chache tangu Spika wa Bunge, Anne Makinda, naye kunukuliwa na vyombo vya habari akidai marupurupu ya wabunge ni madogo hatua inayowafanya wengi wao kuishi maisha magumu baada ya kupoteza ubunge.
Hata hivyo, kikao hicho kilikuwa na upinzani mkali baada ya wabunge wa CHADEMA, John Mnyika na Tundu Lissu kupinga hoja za wabunge wa CCM wakiwataka wawe na uchungu na wananchi.

Sakata hilo lilitokea juzi kwenye kikao cha wabunge na uongozi wa Bunge cha kupeana utaratibu wa ratiba za shughuli za Bunge (briefing). Baada ya wabunge kupata taarifa fupi ya ratiba walipata nafasi ya kujadili mambo yanayowahusu, hususani huduma kwa wabunge.

Sintofahamu ilikuja pale wabunge wa CCM walipotoa hoja ya kuwataka viongozi wa Bunge kuwaambia ni maslahi gani wanayapata kwa kuwachagua wao hadi sasa.
Chanzo chetu kilidokeza kuwa mbunge mmoja kutoka mkoani Tabora (jina tunalihifadhi) alihoji hilo na kuwataka viongozi wao kama wameshindwa kazi basi wajiuzulu kwa hiari huku akisema wabunge wana maslahi madogo, hivyo kuhitaji kuongezewa mishahara.
“Alitoa hoja ya kuahirisha kujadili hoja nyingine ili wajadili mishahara yao ambayo alidai ni midogo na kutaka iongezwe mara moja kwa kuwa wabunge wana hali ngumu sana,” kilisema chanzo hicho.

Baadaye alifuatia mbunge mwingine kutoka mkoani Dodoma ambaye alihoji juu ya posho wanazopata na kusema mshahara ni mdogo, hivyo akapendekeza malipo ya sh milioni 12 ili waweze kufikia viwango vya nchi nyingine kama Kenya.
“Lakini mbunge mwenzake kutoka mkoani Mara (anamtaja) alitoa hoja ya viongozi wa Bunge kukaa viti vya mbele ili wahojiwe na kama hawataki wafukuzwe kazi mara moja na kuchagua makamishina wengine pamoja na Spika na Naibu Spika,” kiliongeza.
Chanzo hicho kilisema kuwa wabunge hao walikuwa na umoja na kushikana kupigania posho na mishahara mikubwa zaidi wakisema hawatosheki.

Kwa mujibu wa chanzo hicho, Mbunge wa Ubungo, John Mnyika (CHADEMA), nusra atibue mjadala huo baada ya kuwapinga watoa hoja na kupendekeza posho za vikao zifutwe kama kweli wabunge wanaipenda nchi yao na wananchi wao.
Inaelezwa kuwa wabunge walipinga hoja yake kwa kuguna na kunong’ona wakiashiria kutounga mkono, hatua iliyomfanya mbunge mwenzake wa Singida Mashariki, Tundu Lissu (CHADEMA) kuingilia kati.

Lissu aliwaambia wabunge waache umbumbumbu wa kutosoma sheria ya utumishi wa Bunge kwa kuanza kutaka kumtoa spika na naibu wake madarakani, akisema wao sio sehemu ya uamuzi wa malipo kwa wabunge na kwamba malipo yao yapo mikononi mwa rais.

Kikao hicho kiliahirishwa kwa mahitaji kufanyika kwa kikao kingine rasmi kwa ajili ya kujadili maslahi ya wabunge, huku wabunge wakitaka spika awepo na Waziri Mkuu ili waweze kuwahoji juu ya malipo yao.
Wadadisi wa masuala ya siasa wanaiona hali hiyo kama hatua ya wabunge wengi kutokuwa na matumaini ya kurudi bungeni kwa kipindi kingine.

Kwamba wanashinikiza malipo makubwa ili fedha hizo ziwasaidie kwa ajili ya maandalizi ya kuhakikisha wanakuwa na hazina pindi wanapomaliza muda wao mwaka 2015.
Chanzo: Tanzania Daima

No comments: