Thursday, October 31, 2013

Jela Uhispania kwa uharamia



Wanaume sita wa kisomali wamepatikana na hatia ya kosa la uharamia nchini Uhispania baada ya jaribio lao la kuteka manowari ya kijeshi ya Uhispania katika ufuo Somalia Januari mwaka 2012.

Mmoja wa wanaume hao, alihukumiwa miaka 12 na nusu jela wakati wengine watano wakipokea kifungo cha miaka minane jela kila mmoja.
Wakati kesi hiyo ikiendelea kusikilizwa mjini Madrid, wanaume hao sita walikanusha kuwa maharamia wakisema kuwa walikuwa wavuvi waliokuwa wanataka usaidizi kutoka katika meli hiyo.

Wanaume hao hatimaye walisalimu amri.
Manowari ya kijeshi ya Uhispania, Patino, ilikuwa inashiriki katika harakati za Muungano wa Ulaya dhidi ya uharamia katika bahari hindi wakati wa jaribuo la watu hao kuiteka.
Kwa mujibu wa viongozi wa mashitaka wanaume hao walijaribu kuingia kwenye boti hiyo kwa lazima kabla ya saa tisa mchana saa za Uhispania.

Wasomali hao waliokuwa wamejihami kwa bunduki aina AK-47 na maguruneti walijaribu kuivamia meli hiyo lakini walifuatwa kwa kasi na manowari hiyo huku ufyatulianaji risasi ukizuka na kudumu kwa dakika mbili . Alisema mwendesha mashitaka.
Walianza kutoroka lakini walifuatwa na wanajeshi wa Uhispania na hatimaye wakasalimu amri.

Wanaume hao sita - Mohamed Abdullah Hassan, Mohamed Aden Mohamed, Issa Abdullah Issa, Abdillahi Mohamed Gouled, Mohamed Said Ahmed na Hamoud Elfaf Mahou – walihukumiwa kwa kosa la uharamia pamoja na kumiliki silaha .
Mmoja wa wanaume hao alipatikana na kosa la kuwa mwanachama wa genge la wahalifu na kupewa kifungo kirefu kuliko washukiwa wengine watano.

Wiki jana Umoja wa Mataifa ulisema kuwa visa vya uhaaramia vimepungua sana katika bahari hindi ikilinganishwa na hali ilivyokuwa mwaka 2006 kutokana na kuimarishwa kwa usalama.
Chanzo: BBCSwahili

No comments: