Wednesday, October 30, 2013

Mbowe aonya wanasiasa kutumia nyumba za ibada



Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Freeman Mbowe, ametoa rai kwa viongozi wa dini kukemea watu wanaogeuza nyumba za ibada kama njia ya kutaka kufanikisha malengo yao ya kisiasa kwa kutoa michango ya fedha wanazozipata kwa njia ya ufisadi.

Kwa mujibu wa Ofisa Habari Mwandamizi wa chama hicho, Tumaini Makene, Mbowe alitoa wito huo mwishoni mwa wiki wakati akiongoza harambee ya kuchangia ujenzi wa jengo la Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Usharika wa Sono uliopo katika kijiji cha Masama-Sono, wilayani Hai.

Aliwataka viongozi wa dini zote nchini kukemea suala hilo na wawe makini na watu wa namna hiyo, badala ya kuangalia kiwango cha ukubwa wa fedha wanazotoa bali uhalali na usafi wa kile wanachochangia.
Mbowe aliwapongeza waumini wa usharika huo kwa kuamua kujenga kanisa hilo wao wenyewe, tangu mwaka 1994.

"Kwanza napenda kuwapongeza Watanzania wenzangu na waumini wa usharika huu wa Sono, kwa kuifanya kazi ya Mungu, mlipoamua kujenga jengo hili zuri kwa nguvu zenu wenyewe, polepole tangu mwaka 1994 na sasa bado mnaendelea, mkiwa mmemaliza sehemu kubwa ya kazi hii muhimu.

"Katika hatua hii ningependa pia kutoa rai yangu kwa viongozi wetu wa dini nchini. Nitajengea hoja zangu kutokana na mahubiri ya Baba Askofu Erasto Kweka. Kwa siku za hivi karibuni kumeibuka tabia ya watu kugeuza nyumba za ibada kuwa ni soko au mapango ya walanguzi.

"Watu wengine wanajulikana wamepata fedha kwa dhuluma, wizi, rushwa na ufisadi mwingi, fedha ambazo zingeweza kutumika kununulia dawa za watoto wetu hospitalini, dawa za akina mama hospitalini, kuboresha elimu yetu inayoporomoka na huduma zingine muhimu.

"Wanapita kwenye nyumba za ibada wakitumia kama sehemu za kujisafisha na kujitakasa kwa kutoa kiasi kikubwa cha fedha. Sisemi muwalaani na kuwafukuzilia mbali, bali muwaombee sana ili wawe wasafi, wakija kwenye nyumba za ibada, waje wakiwa safi ili hata wanachotoa kiwe na baraka, kwa sababu wakiendelea kutoa fedha zao chafu wanakosa hizo baraka," alisema.

Alisema anawasihi viongozi hao wasiingie kwenye mtego wa kuangalia ukubwa wa michango inayotolewa na watu kwenye nyumba za ibada, bali waangalie usafi wa hicho kinachotolewa, wasikubali mahali pa ibada kutumika kusafisha fedha chafu. Endeleeni kuwaombea wapate utakaso na kukiri dhambi zao.

Aliongeza kuwa yeye na wenzake hawapambani na serikali kwa sababu hawana adabu, bali wameamua kuwa sauti ya watu wengi wanyonge wasiokuwa na sauti katika kupata haki na matumaini katika nchi yao.

"Na ni vyema waumini wenzangu tukaelewana vyema, ninaposema vyama vya upinzani wajibu wake ni kuikosoa serikali na chama kilichopo madarakani kwa wakati huo, hatumaanishi tunapambana na serikali kwa sababu hatuna adabu, bali tumeamua kuwa sauti ya wanyonge wengi katika nchi hii.

Naye Askofu Mkuu mstaafu wa KKKT, Erasto Kweka, alimshukuru mbunge huyo kuwa pamoja na kutingwa na majukumu mengi, kuitikia wito wa kujumuika na waumini wa usharika huo na kuwatia nguvu katika ujenzi wa kanisa lao, akimtaka aendelee na moyo huo.

"Tunajua kutokana na majukumu yako, umejibidisha sana kufika hapa. Mungu aendelee kukutia nguvu na kukujengea moyo wa namna hiyo si kwa ajili ya kanisa tu, bali kwa ajili ya jamii nzima ya Watanzania inayohitaji utumishi wa watu wanaojitoa.
Takriban Sh. milioni 16 zilichangwa kwa fedha taslim na ahadi, katika harambee hiyo, ambapo waumini usharika huo walichangia jumla ya Sh. 7,956,800 huku mbunge huyo akichangia Shilingi milioni nane.
CHANZO: NIPASHE

No comments: