Tuesday, October 29, 2013

Mwakilishi: Urais wa Muungano uwe wa zamu




Zanzibar. Katibu wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar (BLW), Yahya Khamis Hamad amesema Rasimu ya mwisho ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania lazima izingatie kuwa na utaratibu wa kupata Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa zamu kati ya Bara na Zanzibar.

Alisema mfumo huo mpya utasaidia kuimarisha misingi ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar na kutaka Tume ya Mabadiliko ya Katiba kuzingatia maoni ya wananchi waliopendekeza mfumo huo wakati wa utoaji wa maoni ya mabaraza ya Katiba.
Aliyaeleza hayo katika mahojiano maalumu na gazeti hili yaliyofanyika Chukwani Unguja jana na kutaka Wajumbe wa Bunge la Katiba kuweka kando misimamo ya vyama vyao na kuangalia masilahi ya kila nchi baina ya pande mbili za Muungano.

Hamad alisema mfumo wa urais wa zamu utaipa nafasi Zanzibar badala ya mfumo wa sasa unaotumika ambao unaonyesha Zanzibar itawachukua muda mrefu kutoa nafasi ya urais wa Muungano baada ya Rais Ali Hassan Mwinyi kuchukua nafasi ya Rais mstaafu Julius Nyerere aliyeondoka madarakani mwaka 1985. Alisema nafasi hiyo kuendelea kwake kupatikana kwa ushindani, huku wanasiasa kutoka Zanzibar kuonekana wakikabiliwa na nguvu haba za kiushawishi wakati siasa za Muungano zikihitaji nguvu na kuwekeza mitaji ya kisiasa na kiuchumi linaweza kuwanyima haki ya kushika nafasi hiyo.

Hata hivyo, alisema baadhi ya wanasiasa wa Bara wakianza kutajwa na wengine wakaonekana kufanya maandalizi ya kampeni hizo, upande wa Zanzibar wamebaki kimya kana kwamba hakuna wenye uwezo na nia ya kushika nafasi hiyo.
“Sioni sababu ya kuwa na sheria moja ya vyama vya siasa kama muundo wa Serikali tatu utapita, muhimu jambo hilo kuliangalia kwa manufaa ya pande mbili za Muungano,” alisema Hamad.

Hata hivyo, alisema iwapo Rasimu mpya ya Katiba itapitishwa na Bunge la Katiba na kuruhusiwa mgombea binafsi pia Katiba ya Zanzibar ya mwaka 1984 italazimika kuangaliwa upya ili kulizingatia suala hilo kwa vile ndiyo njia ya uimarishaji wa msingi ya demokrasia.
Chanzo: Mwananchi

No comments: