Saturday, November 2, 2013

Waziri Mkuu al-Maliki aomba msaada Marekani



Waziri Mkuu wa Irak Nuri al-Maliki anakutana na Rais Barack Obama mjini Washington wakati ambapo nchi yake inakabiliwa na wimbi kubwa la umwagikaji damu. Waziri Mkuu huyo ameenda Marekani kuomba msaada.
Waziri Mkuu wa Iraq Nuri al-Maliki
Rais Obama anasifika kwa kuvimaliza vita vya Iraq kwa kuyaondoa majeshi ya Marekani . Lakini Obama anakutana na mtu ambae bado anapigana vita hivyo-Waziri Mkuu Nuri al -Maliki.

Waziri Mkuu al-Maliki anakutana na Rais Obama wakati ambapo umwagikaji damu umefikia kiwango kisichokuwa na mithili nchini Iraq tokea mwaka 2008. Waziri Mkuu wa Iraq ameomba msaada wa Marekani ili aweze kukabiliana na hali hiyo miaka miwili baada ya majeshi ya Marekani kuondoka. Waziri Mkuu al- Maliki ameomba msaada wa zana zaidi za kijeshi sambamba na ushirikiano mkubwa zaidi katika mambo ya usalama baina ya nchi yake na Marekani .

Watu takriban 1000 wameuawa
Kwa mujibu wa taarifa ya wizara za afya, mambo ya ndani na ulinzi mwezi uliopita watu takriban 1000 waliuawa nchini Irak. Kati ya hao, 855 walikuwa raia,65 walikuwa polisi na wanajeshi 44. Watu wengine 1600 walijeruhiwa.Lakini taarifa ya Umoja wa Mataifa inaonyesha kwamba waliouawa ni wengi zaidi.

Mjumbe maalumu wa Umoja wa Mataifa Nickolay Mladenov amesema mauaji yanayofanyika kiholela yanaendelea mtindo mmoja. Waziri Mkuu wa Iraq ameifafanisha hali anayopambana nayo katika nchi yake inayotokana na mashambulio yanayofanywa na wapiganaji wenye uhusiano na Al-Qaeda na vita vikuu vya tatu.
Miaka miwili baada ya majeshi ya Marekani kuondoka Iraq nchi hiyo imesimama kwenye ukingo wa vita vingine vya kimadhehebu .Mauaji yameendelea leo(ijumaa) ambapo watu wanne waliuawa kaskazini mwa nchi hiyo.

Waziri Mkuu al-Maliki anatarajiwa kuiomba Marekani isaidie zaidi katika juhudi za kupambana na umwagijaki damu nchi mwake. Mwezi uliopita sehemu kadhaa za hadhara zilishambuliwa ikiwa pamoja na mikahawa, na bustani za mapimziko.Watu waliokuwa mazikoni pia waliwashambuliwa mara kwa.

Hata kwa Iraq mauaji yamezdi
Mtaalamu wa masuala ya Iraq kutoka Wakfu wa Ujerumani , Friedrich-Naumann ,Falko Walde amesema Iraq haijawahi kwua na utulivu tokea kuangushwa kwa Saddam Hussein.Ghasia zimetokea wakati wote lakini amesema hali ya sasa ni mbaya sana. Wizara ya mambo ya nje ya Marekani imesema watu wasiopungua 6,000 wameshaua mnamo mwaka huu nchini Iraq

Maafisa wa Ikulu ya Marekani wamesema Rais Obama atalijadili suala la usalama na Waziri Mkuu al-Maliki na kujaribu kutafuta njia za kupunguza umwagikaji wa damu nchini Iraq.
Mwandishi:Mtullya Abdu.afp,rtre
Mhariri: Yusuf Saumu

Kenya yapitisha sheria kali dhidi ya vyombo vya habari



Gazeti la Daily Nation la Kenya.

Vyombo vya habari vya Kenya vimekasirishwa na hatua ya bunge kuupitisha mswaada wa sheria unaoipa serikali nguvu za kuwapiga faini kubwa waandishi wa habari kwa kwenda kinyume na kile kinachoitwa 'maadili ya uandishi.'

Katika mswaada huo uliopitishwa katika kikao kilichokaa usiku sana siku ya Alhamis (tarehe 31 Oktoba), wabunge wameridhia kuundwa kwa Baraza la Rufaa ya Vyombo vya Habari na Mawasiliano linaloteuliwa na serikali na ambalo wamelipa uwezo wa kutoza faini ya hadi shilingi milioni 20 za Kenya (sawa na euro 173,000 ama dola 234,000 za Kimarekani) kwa wale watakaokutikana na makosa.

Sheria hiyo pia imelipa Baraza hilo la Rufaa nguvu za hata kumfungia mwandishi wa habari asifanye kazi zake.

Sheria hiyo, ambayo sasa inasubiri kusainiwa na Rais Uhuru Kenyatta, inaweka pia udhibiti mkali kwa matangazo ya redio na televisheni, ambapo vituo hivyo vinatakiwa kuhakikisha kuwa asilimia 45 ya kile wanachokitangaza kiwe kimetengenezwa nchini Kenya.

"Sheria ya ukandamizaji"
Jengo la Westgate wakati lilipokuwa likishambuliwa mwezi Septemba 2013. Jengo la Westgate wakati lilipokuwa likishambuliwa mwezi Septemba 2013.

Gazeti la Daily Nation la Kenya limesema mswaada huo "unaiweka Kenya kwenye kiwango sawa na Zimbabwe, Cuba, Ethiopia na Kuwait" na kwamba utairudisha nchi hiyo kwenye "zama za giza".

Gazeti hilo linaloheshimika nchini Kenya limesema katika tahariri yake ya siku ya Ijumaa (tarehe 1 Novemba) kwamba "ghafla moja, bunge limezifuta haki za vyombo vya habari" na kuiita hatua hiyo kuwa ni ya kuogofya ambayo inazua mashaka kwamba bunge hilo halitashindwa hata kuondoa uhuru wa mahakama hapo baadaye.

Kwa mujibu wa gazeti la The Star, sheria hiyo mpya ya vyombo vya habari utaipa serikali "uwezo mkubwa sana" juu ya vyombo hivyo, huku gazeti jengine, The Standard, limesema sasa demokrasia na uhuru wa maoni nchini Kenya "vimepigwa dafrau", likiongeza kwamba sheria hiyo ni ya "ukandamizaji."

Kisingizio cha usalama wa taifa
Wanajeshi wa Kenya wakati wa juhudi za kulikomboa jengo la Westgate, Nairobi, mwezi Septemba 2013. Wanajeshi wa Kenya wakati wa juhudi za kulikomboa jengo la Westgate, Nairobi, mwezi Septemba 2013.

Kupitishwa kwa mswaada huo kunakuja wakati kukiwa na mkururo wa kile kinachoitwa "hatua za kuimarisha usalama wa taifa" kufuatia mashambulizi ya hapo mwezi Septemba kwenye jengo la maduka la Westgate lililofanywa na wanamgambo wa al-Shabaab.

Vyombo vya habari vya Kenya viliingia kwenye mgogoro na mamlaka nchini humo kwa kutangaza picha zilizochukuliwa kwenye kamera za usalama jengoni humo, ambazo zinawaonesha wanajeshi wakichukua vitu kutoka baadhi ya maduka na kutoka navyo nje kwenye mifuko ya plastiki.

Mara tu baada ya kurushwa kwa picha hizo, mkuu wa polisi, David Kimaiyo, aliwaita waandishi wawili wa habari na mkuu wa kituo cha televisheni cha KTN kwa ajili ya kuwahoji.

Kimaiyo alikuwa amesema kwamba "uhuru wa habari una mipaka yake na kwamba polisi ilikuwa inawafuatilia kwa karibu waandishi wanaopotosha ambao wangelipandishwa mahakamani hivi punde.

Baadaye serikali ilifuta wito huo, baada ya kushambuliwa vikali na vyombo vya habari.

"Baada ya mashauriano ya kina, wito huo umefutwa," alisema afisa mmoja kutoka Wizara ya Ndani, akiongeza kwamba waandishi hao wa habari, Mohammed Ali na Allan Namu wanaoendesha kipindi cha habari za uchunguzi cha Jicho Pevu, na mkuu wao hawakupaswa tena kuhudhuria kwenye kituo cha polisi kwa mahojiano.

Mwandishi: Mohammed Khelef/AFP
Mhariri: Saumu Yusuf

Friday, November 1, 2013

MAGAZETINI LEO IJUMAA 01 NOVEMBA 2013










NAHODHA: HATURUDI NYUMA DRC




Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Bw. Shamsi Vuai Nahodha, jana ameongoza mamia ya waombolezaji kuaga mwili wa Luteni Rajab Mlima aliyeuawa Oktoba 27 mwaka huu.
Waombolezaji wakiwemo askari wa Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), walionekana kuwa na huzuni kubwa baada ya mwili huo kuwasili katika Uwanja wa Lugalo 521 KJ.

Akizungumza baada ya waombolezaji kutoa heshima za mwisho, Bw. Nahodha alisema Luteni Mlima amekufa wakati akitekeleza jukumu la ulinzi wa amani katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC).
Alisema Tanzania haishtushi na mauaji yanayotokea dhidi ya askari wake waliopo nchini humo wakiwa na jukumu zito la kulinda amani hadi hali itakapotulia.
"Tutaendelea kupigania amani ya DRC, vifo vinavyotokea dhidi ya askari wetu haviwezi kuturudisha nyuma," alisema.

Mnadhimu Mkuu wa Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ), Luteni Jenerali Samweli Ndomba, alisema Luteni Mlima aliuawa akiwa katika eneo la mapambano na vikosi vya waasi wa M23, katika Mlima wa Gavana, karibu na Goma.
Baada ya mwili wa Luteni Mlima kuwasili Lugalo, ndege mbili za kivita zilipita juu ili kutoa heshima ya mwisho. Maziko yake yalifanyika jana jioni makaburi ya Kisutu, Dar es Salaam

MFADHILI WA UGAIDI MBARONI



Jeshi la Polisi, Wilaya ya Kilindi, mkoani Tanga, limemkamata mfanyabiashara wilayani humo, Bw. Juma Kheri maarufu kwa jina la 'Chifu Abiola', akituhumiwa kufadhili kikundi cha kigaidi kilichokuwa na kambi tatu Kata za Lwande na Negero.

Akizungumza na Majira, Mjini Songe, Mkuu wa Wilaya hiyo, Bw. Suleiman Liwowa alisema Bw. Kheri alikamatwa siku tatu zilizopita na yupo mahabusu wilayani Handeni.
Hata hivyo, Bw. Kheri alipekuliwa katika nyumba anayoishi, duka la jumla na nyumba ya kulala wageni kuanzia 8:30 mchana hadi saa 12.30 jioni.

Bw. Liwowa alisema polisi walipata shida kubaini jina lake halisi, kwani alikuwa anatambulika kwa majina ya Juma Sahel, lakini baadaye wakabaini anaitwa Juma Abdallah Kheri.

"Hadi sasa bado anashikiliwa polisi Mjini Handeni, watu walikuwa wakimjua kwa majina mengine lakini hivi sasa jina lake halisi libebainika," alisema Bw. Liwowa.
Alisema watu wengine wanaohusishwa na vitendo vya ugaidi wamekamatwa kwenye Kijiji cha Gombero, Kata ya Kibirashi wilayani humo.

Aliwaomba wakazi wa Wilaya hiyo,wasiwachukie waumini wa dhehebu la Ansaar Sunna kwani si wahalifu bali waliokuwa wanafanya vitendo vya kigaidi ndiyo wahalifu.
"Serikali haipambani na Ansaar Sunna, bali wahalifu, sisi tunaheshimu dini zote hivyo mnapowaona waumini hao msije mkawafanyia vitendo vibaya," alisema Bw. Liwowa.
Aliongeza kuwa , awali hawakujua kama kundi lilo ni tishio lakini tangu wameanza kupambana nalo, wamebaini ukweli na nguvu yao ni kubwa.

Bw. Liwowa alisema hadi sasa kikundi hicho kimeweza kusambaratishwa lakini polisi bado wameweka kambi kwenye Kata za Negero na Lwande.
Mbunge wa Kilindi, Beatrice Shelukindo, alisema kundi hilo ambalo lilikuwa likifanya vitendo vya ugaidi katika Kata za Lwande na Negero, lisihusishwe na dini ya Kiislamu bali hao ni magaidi, majasusi na wanatakiwa kulaaniwa na kupingwa.

"Lile ni kundi la kigaidi si wahalifu wa kawaida, lakini naomba lisihusishwe na dini ya Kiislamu, sisi sote tunafahamu hakuna dini inayoruhusu vitendo vya ugaidi, kuvuruga amani," alisema
Chanzo: Majira